Kabla Hujakubali Kila Unachoambiwa, Kumbuka Jambo Hili Moja Muhimu Sana.

Binadamu tunaweza kuwa tunaona kitu kimoja kwa namna tofauti kabisa , hii inatokana na kutofautiana mitazamo tu au yaweza kuwa ni kutokana na vitu ambavyo tumejifunza na kuzisikia sana, ndiyo vitu ambavyo tumeaminishwa kuwa vipi hivyo. Na sisi labda kwa ujinga au uvivu wa kutaka kuhoji au kuchimba mambo zaidi basi tumeamua kukariri hivyo na hatupo tayari kusikia kitu kilicho kinyume na tunachoamini. Hata akitokea mtu wa kutuelewesha au kutuambia kitu kipya tunakuwa hatupo tayari kujifunza hicho, hata tukisikiliza hatusikilizi kwa lengo la kujifunza au kuelewa bali tunasikiliza tu ili tuelezee msimamo wetu , tunavyoelewa sisi. Si jambo baya kuelezea kile unajua au kuelewa lakini ni vizuri kama utakuwa tayari pia kujifunza vitu vipya, naamini mwanafunzi hachagui nini afundishwe au asikie, lakini akifundishwa kama hajaelewa huuliza maswali kwa nia ya kueleweshwa zaidi na si kwa nia au lengo la kubishana.
SOMA; Jinsi Ya Kujua Kama Unachofanya Ni Sahihi Katika Maisha Yako.
Tukiangalia katika wakati tulionao wa maendeleo ya sayansi na teknolojia, kuna vitu vingi vizuri sana tu lakini vipo na vibaya vilivyokuja na hii teknolojia, Hivyo kwa sababu hizo nilizosema mwingine anaweza kuona kuwa kukua kwa teknolojia kuna madhara sana, hakufai, mfano huu utandawazi wengi wanauona kama jambo baya lisilofaa kabisa, na wengi wanatumia nguvu nyingi sana kujaribu kufanya kila mtu aone kuwa ni kitu kisichofaa kwa jamii, na wanaposema hivi wana sababu za msingi za kuamini wanavyoamini, maana kuna mambo mengi yasiyofaa yanaendelea mitandaoni, watu wanaiga mambo yasiyofaa humo na hata maadili ya jamii yanamomonyoka, lakini kwa kuwa tu wapo wanaoona hivyo haimaanishi kwamba ni kweli utandawazi ni mbaya na hauna faida, zipo faida nyingi tu za utandawazi ikiwa utautumia vizuri unaweza kunufaika sana tu. Wapo watu wengi wamefaidika sana na mitandao hii ya kijamii kwa kukutana na watu wapya ambao wamewafundisha vitu vingi, watu wamenufaika kiroho na hata kijamii kwa namna ambavyo wametumia mitandao hii ya kijamii, maana kupitia hii hauhitaji kuonana na mtu ili muweze kufundishana au hata kujadilia baadhi ya mambo, pia inasaidia hata kutunza muda na hata gharama za kukutana au kumfuata mtu mahali fulani kwa ajili ya majadiliano, naweza kuwa hospitali, barabarani na nikasoma vizuri au hata kuhudhuria mafundisho au hata ibada bila shida kabisa.
SOMA; Kuna Watu Hawa Ambao Hawawezi Kukuelewa, Wajue Na Waepuke Ili Uweze Kufikia Mafanikio.
Pia katika maisha haya iwe kazini , nyumbani au popote ulipo unaweza kukutana na mtu akakuambia kuwa mtu fulani ni mbaya sana au ana sifa hizi na hizi na pengine akakupa mabaya tu ya huyo mtu, akajitahidi kukuelezea na kukufanya umuone mtu huyo hafai kabisa katika jamii, au hafai kuwa rafiki yako kabisa na pengine si mtu hata wa kufanya naye biashara n.k, Sasa hapo ni wajibu wako wewe kama mtu unayejielewa na kuelewa kuwa sisi binadamu hatupo kama watu wanavyosema tupo, au kwa kuwa fulani ameniona mimi sifai au mimi ni mzuri haimaanishi kwamba kila mtu ataniona hivyo, hivyo hata kama umeambiwa nini kuhusu mtu fulani hebu usiende kwake ukiwa na hiyo picha uliyopewa, bali amua kuona mwenyewe kama kweli yupo kama ulivyoambiwa au yuko tofauti na vile, maana ukienda kwa namna ulivyoambiwa unaweza kujikosesha fursa nyingi sana kwa ujinga wako wa kutotumia akili na maarifa uliyopewa na Muumba wako, mtu mwingine anaweza kukuambia mtu fulani yupo hivi kwa kuwa tu ana chuki na huyo mtu au pengine hata hamjui huyo mtu, au alisikia tu watu wakisema hivyo lakini hajathibitisha mwenyewe
Tambua kuwa hatuwezi wote kuona jambo lilelile sawasawa maana kila mtu ni wa pekee, hivyo ni vyema kuheshimu mtazamo wa kila mtu lakini usiutumie mtazamo wa mwingine kama ndio mamlaka ya mwisho ya wewe kuona. Hivyo hata kama umeambiwa kitu fulani hakifai hakikisha kuwa unatumia akili zako na utashi wako kufanya uchunguzi kuona kama kweli kitu hiki kipo kama unavyoambiwa kipo, ni muhimu kutambua kuwa binadamu tunaona vitu vilevile kwa tofauti, ndio maana kuna mtu ni mzuri kwangu lakini wewe waweza kumuona mbaya au hafai kwa kuwa kila mtu ana vigezo vyake vinavyomfanya aone anavyoona, usiishi kwa kufanya yale uliyoambiwa bali ishi kama vile unavyotakiwa kuishi na Muumba wako, umuone kila mtu kuwa bora, mwenye uwezo wa kufanya jambo la maana maishani, usimkadirie mtu kwa kusikia maneno ya kuambiwa kamwe maishani.
Imeandika na Beatrice Mwaijengo
Mobile number: +255755350772

0 comments: