Siri Ya Mfereji Wa Upendo Kuelekea Kwenye Bahari Ya Mafanikio

Upendo ni neno tunalolisikia kila mara. Upendo una nguvu zaidi ya nguvu ya kifo. Upendo kutafsiri n hauna ukuta. Upendo una sifa nyingi sana. Hauhesabu mabaya, haujivuni, husamehe, haulipizi kisasi, upendo hustahimili yote.
Kama ukipenda ukampenda mtu waswahili wanasema hata jalala lao utaliona zuri. Yaani hakuna ubaya utakaouona kwa mtu kama ukimpenda. Lakini hata akikuudhi kiasi gani utamsamehe kwakua unampenda sana.
Ukipenda wale wanaokuchukia, usipolipiza kisasi, usipowaonyesha ubaya wowote, kama wanakuchukia basi wanaweza kubadilika. Kama wasipobadilika basi wataondoka mahali ulipo. Upendo una nguvu sana.
Mahali palipo na upendo kuna maendeleo sana. Kama wanandoa, wanafamilia, wanaukoo au wanakijiji fulani wanapendana basi mambo yao mengi huenda vizuri. Kwakua kila mmoja yupo katika eneo lake kuhakikisha kuwa mwenzake anaishi kwa furaha. Ni rahisi kufanikiwa kama una upendo na hauna kinyongo na watu wengine.
Unawezaje kuwapenda hata wale wanaokuudhi?
“Kuna usemi wa Kiswahili unaosema “akuchomaye mchome” au “mpende akupendaye asiyekupenda achana naye” kuna baadhi ya watu hutafsiri vibaya usemi huu. Yaani mtu akimfanyia kitendo kibaya na yeye analipiza. Sio busara na sio jambo jema kumfanyia mtu ubaya hata kama yeye amekufanyia hivyo. Kwa kufanya hivyo utaongeza chuki na uadui.
Katika vitabu vya dini tunashauriwa kuwapenda wasiotupenda ili tupate thawabu. Kwakua kuwapenda wanaotupenda pekee kutawafanya wale wanaotuchukia wasibadilike kwakua sisi pia tunawachukia na hakutakuwa na mabadiliko hivyo hatupati thawabu kwa kuwachukia wanaotuchukia.
Lakini ukimpenda anayekuchukia basi ataona aibu tu. Sio kwa siku moja lakini baada ya muda mtu huyu anaweza kubadilika.
Naomba nikufundishe mbinu moja itakayopunguza kasi ya chuki na kuleta upendo ndani yako. Ukiamka tu, sema moyoni ninawapenda watu wote. Endelea kujikumbusha neno hili siku nzima. Kila unayeonana nae jiambie kuwa unampenda. Hata akiongea neno baya wewe jiambie moyoni kwa nguvu zote kuwa unampenda. Akikufanyia kitu kibaya, muhurumie huwezi kufahamu ana msongo wa mawazo kiasi gani. Badala ya kujenga chuki juu yake ambayo inaweza kukuletea madhara ya kiafya jiambie kuwa unampenda. Itakusaidia kupunguza vurugu na utaona moyoni mwako una amani.
Mara nyingi watu wenye chuki hupenda kupinga na kukebehi maneno au juhudi za mtu mwenye mawazo ya mafanikio. Watu hawa hufanya hivi mbele za watu ili kupata mashabiki na kukufanya wewe ujisikie vibaya. Hutamani ubishane nao na kugombana au baadae upate muda wa kutafakari yale unayotaka kufanya kuwa hayawezekani. Usiwape nafasi watu wa aina hii kukupotezea malengo yako. Usifanye mambo yako ili kuwaonyesha kama unaweza pia. Fanya kwaajili yako na kwaajili ya furaha ya moyo wako na ya wale ambao wako upande wako kuhakikisha unafikia pale unapotamani ufike. Kama hukufanikiwa kufikia pale ulipokusudia jipange vizuri na uendelee na mapambano. Lakini usimchukie mtu yeyote kwani ukiwa na chuki mafanikio kwako ni ndoto. Upendo na roho safi ni mfereji muhimu kuendea kwenye bahari ya mafanikio.
Makala hii imeandikwa na Esther Nguluwa.

Tangazo muhimu kuhusiana na blog zinazoendeshwa na AMKA CONSULTANTS.

Habari za leo mpenzi msomaji wa blog mbalimbali zinazoendeshwa na AMKA CONSULTANTS. Naamini unaendelea vizuri na harakati zako za kuboresha maisha yako. Na pia naamini TUPO PAMOJA ukiendelea kujifunza na kuhamasika kupitia makala mbalimbali zinazopatikana kwenye blog zako zinazoendeshwa na AMKA CONSULTANTS.
Kama unavyojua lengo kubwa la AMKA CONSULTANTS ni kukuwezesha wewe kuishi maisha bora sawa sawa na uwezo wako. Hapo ulipo una uwezo mkubwa sana wa kufanya mambo makubwa zaidi ya unavyofanya sasa. Ila mfumo wa elimu uliopitia na malezi uliyokulia vimekufanya ushindwe kufikia uwezo wako mkubwa.
Kama umekuwa unafuatilia blog zetu mbali mbali na ukawa unafanyia kazi yale ambayo umekuwa unajifunza, utakubaliana nami kwamba maisha yako umeona yanabadilika, hata kama ni kwa kiasi kidogo. Kama hiki ndio kinachotokea kwenye maisha yako basi nakusihi endelea kufanyia kazi na utazidi kuona mabadiliko makubwa zaidi.
AMKA CONSULTANTS ilianza na blog ya AMKA MTANZANIA na baadae zilianzishwa blog nyingine kutokana na mahitaji tofauti ya wasomaji wetu. Blog hizo ni KISIMA CHA MAARIFA, ambayo unalipia kuwa mwanachama, MAKIRITA AMANI na JIONGEZE UFAHAMU.
Kupitia blog hizi umekuwa unajifunza mambo mengi na mazuri sana. Kwa sababu makala zinazowekwa kwenye blog hizi zinatofautiana na zinalenga maeneo tofauti tofauti ya maisha yako ikiwemo kazi, biashara na hata maisha kwa ujumla.
Napenda kuchukua nafasi hii kuwajulisha wasomaji wote kwamba kutakuwa na mabadiliko kwenye blog hizi zinazoendeshwa na AMKA CONSULTSNTS. Makala ambazo zilikuwa zinawekwa kwenye JIONGEZE UFAHAMU sasa zitahamishiwa kwenye AMKA MTANZANIA na makala zilizokuwa zinawekwa kwenye MAKIRITA AMANI sasa zitahamishiwa kwenye KISIMA CHA MAARIFA. Na blog hizi mbili, MAKIRITA AMANI na JIONGEZE UFAHAMU zitafutwa.
Kwa nini mabadiliko haya?
Kama umekuwa msomaji mzuri wa blog hizi utakuwa uliona tatizo ambalo lilijitokeza kama mwezi mmoja uliopita. Wasomaji ambao walikuwa wanapokea makala za blog moja wapo kwa email ghafla waliacha kupata makala. Wakati huo makala zilikuwa zinatumwa kama kawaida. Kutokana na tatizo hili ilibidi kutafuta suluhisho la haraka ili wasomaji waendelee kupata makala zetu nzuri. Tulipata suluhisho la muda lakini halitadumu kwa muda mrefu, siku zio nyingi tutaingia tena kwenye tatizo kama lile. Na hii inatokana na sababu ya pili ya kuondoka kwenye blog hizi ambayo ni kuwa zimekuwa zinaendeshwa bure.
Blog inapokuwa imehifadhiwa bure na kutumia jina la bure, kuna baadhi ya vitu huwezi kuvibadili. Sasa hili linakwenda tofauti na kile ambacho nataka wewe msomaji ukipate. Kuna wakati nataka kufanya kitu ambacho ni cha tofauti lakini nashindwa kwa sababu blog imehifadhiwa bure na hivyo huwezi kubadili baadhi ya vitu.
Sababu nyingine ni kwamba nina sehemu kubwa ya kuhifadhi blog hizi ambayo ninailipia kila mwaka ambayo kwa sasa imehifadhi KISIMA CHA MAARIFA, sasa ni vyema kutumia sehemu hii ambayo tunailipia gharama kubwa kuweka mafunzo ambayo yataendelea kuboresha maisha yako.
Na sababu ya mwisho tunayoweza kujadili hapa ambayo imepelekea kufanya mabadiliko haya ni wewe msomaji uweze kupata makala zote nzuri kwenye blog chache. Ni kweli kuna umuhimu wa kutenganisha mambo lakini ni vyema wewe kama msomaji ukijua unapata makala zako zote nzuri kwenye sehemu chache ambazo unaweza kuzitembelea kila siku na kutumia muda wao vizuri.
KISIMA CHA MAARIFA ni kulipia, je sisi tuliokuwa tunapata makala bure ndio mwisho?
Ni kweli kabisa ili uweze kusoma makala kwenye KISIMA CHA MAARIFA inabidi uwe umejiunga na ulipie. Ila kwa sasa kwa kipengele hiki cha KURASA 365 ZA MWAKA 2015 wasomaji wote wataendelea kuzipata hata kama hawajajiunga na kulipia. Ila nakusihi sana kama bado hujajiunga na KISIMA CHA MAARIFA ufanye hivyo mara moja kwani unakosa mengi na utaendelea kukosa mengi. Bonyeza maandishi haya KUJIUNGA NA KISIMA CHA MAARIFA. Kuendelea kupata makala za KURASA 365 hakikisha unatembelea KISIMA CHA MAARIFA kila siku, na pia jiunge kwa kuweka email yako unapokuw akwneye KISIMA na utatarifiwa kila makala inapokwenda hewani.
Asante sana kwa kuendelea kujifunza na kufanyia kazi yale ambayo yanawekwa kwenye mitandao hii. Tunaendelea kukuahidi kwamba tutakuletea makala bora kabisa zitakazo boresha na kubadili maisha yako.
TUPO PAMOJA.
Makirita Amani,
makirita@kisimachamaarifa.co.tz

Ulizaliwa Uishi Wewe, Usiishi Kwa Ajili Ya Wengine.

Kila mtu alivyoumbwa kuna kitu alizaliwa ili aje kukifanya, analo jibu la changamoto fulani katika maisha haya tulimo. Ni wajibu wa kila mmoja kuweza kutambua hilo na kuishi hilo kusudi. Hakuna hata mtu mmoja aliyezaliwa ili aje kuwa kama mtu mwingine, ulizaliwa uwe wewe. Kila mtu ni wa pekee ana uwezo wa kufanya mambo kwa namna yake ambayo hakuna mwingine anaweza kufanya hivyo.
Hata mimi uandishi wangu wa makala hauwezi kufanana na wa mwingine, ninayo namna yangu ya kuandika ambayo Mungu aliiweka na naenenda kwa hiyo. Nikijaribu kuwa kama mwingine au kuiga nitashindwa tu, inabidi niwe mimi. Ni wajibu wa kila mtu kwa imani yake kuweza kugundua kile ameumbiwa kufanya.
Kuna mwingine amezaliwa kufundisha wengine tu, popote alipo ualimu wake utaonekana tu, yaani atafurahia kufundisha tu hata kama hamna kipato anapata lakini yeye kuna amani anaipata ndani mwake, kuna kile kitu unaweza kufanya bila kutanguliza malipo, kile ambacho usipofanya unasikia kama una deni, unaona haujatimiza wajibu wako sawasawa. Ukishagundua kusudi la wewe kuwepo ni wajibu wako wewe mwenyewe kulisimamia na kuliishi hilo, ukimshirikisha Muumba wako katika kila hatua.
Pengine baada ya kugundua kusudi lako ni lipi, unaweza kukutana na vikwazo vingi katika kuliishi hilo kusudi. Ndugu yangu tambua kwamba ni wewe na Mungu wako mnaelewa hilo kusudi hivyo usitegemee kila mtu akuelewe kirahisi, usishangae kuona uliotegemea wakuelewe wasipokuelewa. Na hiyo isiwe sababu ya wewe kuona labda umepotea au hauko sawasawa, hata mimi kuweza kuandika hata makala yenye maneno hata mia mbili tu haikuwa rahisi mwanzoni. Kuna wakati nilipompa mtu ambaye nadhani ni wa karibu aipitie na kunipa maoni nilipata maoni ya kukatisha tamaa sana, lakini uzuri ni kwamba wapo waliolewa na kunitia moyo. Lakini si vyema kumpuuza anayekupinga pia maana walikuwa na sababu zao za msingi pia, mwingine anakuambia hujawahi kusomea uandishi au wewe na ufundi wako na uandishi wa makala kama hizi vinahusianaje? Waliona hivyo , hawakubahatika kuona kile kimewekwa ndani mwangu Lakini mimi ndio nilijua kwa nini naandika, maana naamini siandiki ili kupoteza muda wangu bali kuna mtu akisoma anapata uwezo wa kusogea hatua moja mbele, kuna badiliko linatokea ndani mwake, kuna maisha ya mtu yanaguswa na kumfanya awe mtu bora zaidi, na ndiyo furaha yangu hiyo.
Hivyo haijalishi unakutana na nini, naomba kama kweli una uhakika ndicho kitu umeitiwa endelea kufanya, ng’ang’ana tu wapo watakaokuelewa baadae, kuna watu mtoto akizaliwa wanashindwa kuelewa kama anafanana na nani lakini kadri anavyoendelea kukua wanamtambua vizuri na kuzidi kumfurahia hata kama mwanzoni hawakumkubali.
Kuna mtu anajua kabisa anachokifanya sicho kitu anatakiwa kufanya lakini anafanya tu kwa kuwa kuna watu wanamtaka afanye hilo. Wakati mwingine hata mzazi anaweza kukutaka uwe mtu fulani kwa sababu zake binafsi na pengine nzuri tu. Mwingine anaweza kukutaka ufanye kitu fulani kwa manufaa yake. Ishi wewe vile ulikusudiwa kuwa, tumia hekima na busara kuwaelewesha wanaotaka uwe tofauti na ulivyo wakati wewe una uhakika hivyo ndivyo unavyopasa kuwa. Wakati mwingine ikibidi ni bora unyamaze na kuwaacha waone kwa vitendo kile unamaanisha maana hauwezi kujieleza kwa kila mtu.
Hivyo ni wajibu wako na uamuzi wako wewe kwa kuwa ndiwe unajua nini unataka, kuamua kwa dhati kusimamia na kufanya kile unafurahia kufanya, kile kinakupa amani moyoni, kile unakifanya bila kuhangaika au kutumia nguvu nyingi zaidi. Kumbuka kuogopa kufanya kitu unachokipenda kwa kuhofia watu watasemaje haikupi wewe furaha wala amani, bali itakufanya wewe kuwa mtumwa wa nafsi yako mwenyewe, hauishi wanavyotaka watu au jamii, unatakiwa kuishi kama Mungu alivyokukusudia uwe, Ukijaribu kutimiza matakwa ya wanadamu unatakiwa ujue kuwa wanabadilika kila leo, leo wanaweza kukukubali na kukupenda kwa kuwa unafanya hilo lakini using’ang’ane leo watu hao hao wakikugeuka.
Hivyo tafuta sana kujijua wewe ni nani? Kwanini upo? Ukilijua kusudi lako basi liishi hilo kusudi lako , ni kwa kufanya hivyo utaweza kupata ile amani ya kweli maishani mwako, na pia kwa kuishi lile kusudi uliloumbiwa hautumii nguvu nyingi sana ili kuwa hapo, ukishajitambua mambo mengine yote yanakuwa yasharahisishwa, ukiwa kwenye mkondo wa maji, maji yakiwepo yatakupitia tu. Wajibu wako ni kutafuta mkondo wa maji ulipo.
Makala hii imeandikwa na Beatrice Mwaijengo
Namba ya simu : +255 755 350 772

Yafahamu Mambo Muhimu Ya Kuzingatia Kwenye Eneo La Ujenzi Kabla Hujajenga Nyumba Yako

Na Kimbe Nickas
Mwonekano wa Tanzania ya sasa na ya miaka kumi iliyopita ni tofauti sana, mafanikio haya ni kutokana na msukumo mkubwa wa maendeleo ya sekta mbalimbali ukiwemo uwekezaji wa ardhi na majengo unaoshika kasi kubwa ndani na pembezoni mwa miji mikubwa ya Tanzania. Ndugu msomaji wa makala hii usiachwe nyuma bali uwe sehemu ya mafanikio ya kubadili uchumi wa nchi yetu na uchumi wako binafsi, kama wewe ni miongoni mwa watu wengi wanaojiuliza wawekeze kwenye biashara gani itakayokufanya uwe huru kiuchumi na kijamii, jibu ni rahisi sana, isikilize nafsi yako na itendee haki kwa kuwajibika. Nina mengi ya kukushirikisha lakini Leo nakupa mambo muhimu ya kuzingatia kwenye eneo la uwekezaji kabla hujajenga unachotaka kujenga. Mambo haya yatakusaidia kufanya tathmini na hatimaye kufanya maamuzi sahihi ya aina gani ya uwekezaji uweze kufanya, hapa namaanisha aina na matumizi ya majengo kama vile ofisi, maduka, nyumba ya kuishi, mgahawa, hoteli, zahanati au shule.
Mzunguko wa watu
Mzunguko wa watu huathiri kwa kiasi kikubwa maendeleo ya uchumi na jamii katika eneo lolote, mara nyingi maeneo yenye mzunguko mkubwa wa watu ni maeneo yenye huduma bora za kijamii na kiuchumi. Maeneo haya watu huingia na kutoka kutafuta huduma muhimu za kimaisha. Maeneo yenye ofisi za serikali, taasisi mbalimbali, viwanda, makampuni binafsi na umma huwa na mzunguko mkubwa wa watu. Huduma hizo huvuta watu kutoka sehemu mbalimbali kuingia ili kukidhi mahitaji yao ya kimaisha yanayopatikana maeneo hayo. Unapowekeza maeneo kama haya unapaswa kuangalia mapungufu yaliyopo ili kukidhi mahitaji ya watu wa eneo hilo, mfano, kama hakuna hoteli utajenga hoteli, hakuna pakingi utajenga pakingi. Muhimu ni kuangalia namna gani utaondoa tatizo na utakidhi mahitaji ya wengi huku kwa upande wa pili unajijengea uwezo wa kuwa mwenye mafanikio kifedha kwa kuwa umewekeza kilicho sahihi kwa wakati huo.
SOMA; Kama Umewekeza Kwenye Majengo Yafahamu Magonjwa Sugu Yanayo Athiri Majengo.
Aina za nyumba zilizopo
Popote unapotaka kuwekeza nyumba yako lazima utajifunza kitu kutoka kwa waliotangulia kujenga kwenye eneo hilo, mazuri na mapungufu mengi utayaona, yapo mengi ya kujifunza endapo utakuwa makini na kuzingatia ubora, mpangilio na mwonekano wa nyumba za jirani. Lengo la kutathmini nyumba zilizopo ni kuchukua yale mazuri na kuepuka kurudia mapungufu yaliyojitokeza kwa wengine. Mfano, nyumba nyingi za hivi karibuni zimejengewa vyumba vya biashara yaani frem, na wengi wameiga hivyo, lakini wanasahau kuwa wapo wafanyabiashara wengi wanao hitaji aina tofauti ya “fremu” hizo kukidhi mahitaji yao ya kibiashara, tambua kuwa kuna taasisi, kampuni na mashirika mbalimbali yanayohitaji majengo ili kuwafikia wateja wao waliopo sehemu mbalimbali za nchi. Hivyo ili uwe na uwanja mpana wa kupata wateja kwenye majengo ya biashara, lazima ujenge nyumba itakayokidhi mahitaji mbalimbali ambayo pia ni rahisi kwa kubadili matumizi pasipo ubomoaji wowote. Hakikisha ujenzi utakaofanya unaongeza thamani katika eneo hilo, hii ndiyo sababu mojawapo ya wewe kutumia wataalamu kwenye mipango yako ya uwekezaji ili wakushauri namna gani ya kujenga kutokana na mabadiliko makubwa yanayojitokeza kwa sasa. Jitahidi kuwa bora zaidi ya wengine ili upate wateja zaidi na mafanikio zaidi.
Miundombinu iliyopo
Kabla ya kununua ardhi au kuanzisha ujenzi wako ni muhimu sana ukazingatia na kutathmini miundombinu iliyopo ili isisababishe ukinzani wowote wa ujenzi wako unaotaka kufanya. Kwa mujibu wa katiba tuliyonayo, ardhi yote ya jamhuri inasimamiwa na rais wa jamhuri, hivyo kama kuna miundombinu yoyote yenye manufaa kwa wengi jaribu kuikwepa maana kwa namna yoyote ile utaondoka wewe ili miundombinu hiyo iendelee kuwanufaisha wengi. Zingatia sana hifadhi za barabara, misitu, nishati za umeme na miundombinu iliyofukiwa. Miundombinu iliyofukiwa juu ya ardhi huwekwa alama (bikoni) kila baada ya umbali fulani kuonesha mwelekeo wa miundombinu hiyo. Pia maeneo yenye miundombinu ya uhakika huwa ni kivutio kikubwa kwa watu tofauti na maeneo ambayo bado hakuna miundombinu ya uhakika.
Fanya uthamini binafsi
Jijengee utaratibu wa kufanya tathmini kabla ya kufanya uwekezaji wowote ule, kabla ya kununua eneo au nyumba jipe muda wa kutosha wa kufikiri na kufanya tafiti ili uwe na taarifa sahihi la eneo husika. Tathmini yako izingatie ulinganifu wa bei za manunuzi au gharama za ujenzi, matumizi rasmi ya eneo hilo, umiliki rasmi wa eneo hilo, hata ramani ya nyumba yako lazima izingatie mazingira ya eneo husika. Jipe muda wa kutosha kupata taarifa sahihi kabla ya kufanya maamuzi ya kununua au kujenga, Hii itakusaidia wewe kufanya uwekezaji wako kihalali na kwa kufuata taratibu zote, pia utaepuka gharama kubwa kutokana na udanganyifu wa watu au faini kutoka kwa mamlaka husika endapo utakiuka jambo lolote kwa kukosa taarifa sahihi.
Zione mamlaka husika za kisheria na usimamizi
Daima unaponunua au kuwekeza nyumba au kufanya chochote kwenye ardhi zione mamlaka husika ili upate taratibu rasmi za kufuata ili malengo yako yatimie pasipo misuguano na mamlaka hizo za serikali. Hakuna jambo linalokosa taratibu za kimfumo, hata kwenye ujenzi zipo mamlaka zinazosimamia mfumo na vibali kabla na wakati wa ujenzi na baada ya ujenzi. Pia taratibu hizo hutofautiana kutokana na sera na taratibu za kimfumo za mamlaka za usimamizi wa eneo husika. Watu wengi hawajui kuhusu taratibu hizi, hujikuta wameletewa barua za kusimamisha ujenzi wao (stop order) pasipo kujua nini cha kufanya. Ni muhimu sana ukazifahamu taratibu za mahali husika kabla hujaamua kujenga, tofauti na hivyo utabomolewa na kujikuta umepoteza fedha nyingi pasipo msaada wowote.
Washirikishe wataalam wa Ardhi na ujenzi
Ni muhimu sana kuwashirikisha wataalamu wa fani husika ili wakushauri namna gani uweze kufikia lengo lako huku ukitabasamu kwa furaha. Watu wengi wamejikuta wapo kwenye majuto makubwa baada ya kutapeliwa fedha zao na watu wasio na ufahamu wowote kuhusiana na ardhi na ujenzi wa nyumba. Watafute sasa maana wanapatikana kila mahali, wathamini ardhi (land valuer) watakusaidia namna gani ya kumiliki ardhi yako, wasanifu majengo(Architects) watakuchorea ramani ya nyumba yako, wakadiriaji majenzi (Quantity Surveyors) watakusaidia kupanga na kusimamia gharama za ujenzi wako, wahandisi (ujenzi, umeme na maji) watasimamia ujenzi wa nyumba yako. Hawa wote kwa pamoja ni timu yenye uwezo wa kuhakikisha mjasiriamali unapata ulichotarajia kupata kwa uhalisia wake. Kama unataka mafanikio ya kweli watumie wataalamu kwenye mambo yako.
Tuendelee kuwa pamoja kupitia JIONGEZE UFAHAMU tufike kwenye kilele cha mafanikio, pia endelea kufuatilia makala zijazo ili ujifunze zaidi.
Mwandishi wa makala hii ni mwanataaluma na mshauri wa ujenzi.
Anapatikana kwa: Simu: +255 685 729 888, Email: kimbenickas@yahoo.com

Sehemu 7 Ambazo Unatumia Kupoteza Rasilimali Muda Wako

Muda au wakati ni rasilimali ambayo ikipotea hairudi tofauti na rasilimali fedha ambayo ukipoteza utaitafuta lakini ukipoteza muda huwezi kuupata hata kwa fedha. Mtunzi wa kitabu cha The Secret Code of Success ambaye ni Noah St. John anasema muda ni rasilimali ambayo huwezi kununua hata mabilioni ya Bill Gates hayawezi kununua hata dakika moja ya jana.
Hivyo basi, kumbe muda ni rasilimali muhimu ambayo hatuwezi kununua. Utajiri ambao tumepewa duniani bure kwa watu wote matajiri na masikini ni rasilimali muda. Wote tuna wakati sawa wa masaa 24 kwa siku. Kwa hiyo kila mtu duniani ni Tajiri wa muda au wakati. je unautumiaje utajiri wa rasilimali muda wako hapa duniani?
Zifuatazo ni Baadhi ya Sehemu Ambazo Unatumia Kupoteza Rasilimali Muda
1. Kuangalia Tv
Watu wengi wamekuwa wakipoteza muda sana kuangalia tv, mtu anapoteza masaa matatu mpaka matano kuangalia tv akifuatilia tamthilia kwenye tv. Kuangalia vipindi ambavyo havina tija kwako vipindi ambavyo havina matokeo chanya kwako, kiongozi wa kanisa Katoliki duniani papa francis, ana miaka 25 sasa hajawahi kuangalia tv yaani luninga mara ya mwisho kuangalia tv ilikuwa ni tarehe 15 mwezi saba mwaka 1990. Je tunajifunza nini kutoka kwa kiongozi huyu? Kama yeye ni kiongozi mkubwa wa kanisa hilo duniani mbona hajapungukiwa wala hajapitwa kwa nini wewe usiweze?
2. Kufuatilia Udaku
Unapoteza muda kumfuatilia msanii Fulani leo amefanya nini badala ya kutumia muda huo kuboresha maisha yako. Watu wengi ni wazuri kufuatilia magazeti ya udaku, habari za udaku, mitandao au blog za udaku kuliko kufuatilia blog nzuri zinazotoa elimu ya jinsi kuboresha maisha yako moja wapo ni hii unayosoma makala hii nzuri. Utumie muda wako kufuatilia vitu vya maana ambayo vinabadili fikra yako acha kuwa mtumwa wa kila siku wa kufuatilia habari za udaku.
SOMA; MUDA–Kitu Chenye Thamani Kubwa Ila Kisichothaminika Na Wengi.
3. Kufuatilia Mitandao ya Kijamii kwa Faida Hasi
Kuwa katika mitandao ya kijamii kama vile facebook, twitter, na kadhalika siyo mbaya, je uko katika mitandao hiyo ya kijamii kwa malengo gani? Unatumiaje muda wako katika mitandao hiyo ya kijamii kila dakika uko online kwenye mtandao zaidi ya mmoja unapata muda wapi wa kufanya kazi yako kwa ufanisi? Tenga muda wako vizuri kataa kabisa kuwa mtumwa wa kisaikolojia ukikaa kidogo bila kuingia unahisi unapitwa na habari wenzako wanaingiza siku wewe unafuatilia habari.
4. Kukaa Vijiweni
Wimbi la watu kukaa vijiweni na kupoteza muda linaongezeka kila siku ukipita kona hii utakuta watu wamekaa makundi vijiweni wakijadili serikali pengine sijui chama Fulani wamefanya hivi ni mambo mengi yanayojadiliwa kwenye magenge ya watu. Watu hawana kazi za kufanya wanapoteza muda bure na wala hajutii kwa muda anaoupoteza. Tumia muda huo kujifunza namna gani unaweza kubadili maisha yako. Acha kauli hizi za kusema ngoja niende kwa Fulani au kijiweni nikapoteze muda kidogo.
5. Kubishana
Hii ni sehemu moja wapo ambayo watu pia wanapoteza rasilmali yao nzuri ya muda katika kubishana. Watu wanabishania vyama vya siasa, timu za mipira kuna wengine wanabishana katika mpira mpaka wanapigana hii ni kwa sababu kila mmoja anataka asikilizwe kile anachosema yeye katika timu yake ndio sahihi. Unapoteza muda kushabikia vitu wakati huna hata hisa moja katika vitu hivyo unavyobishania ambavyo havikusaidii kuboresha maisha yako kabisa zaidi ya kukusababishia hasara ya kuendelea kuwa mtumwa wao.
SOMA; Lakini Nitapitwa.... (Sababu Ya Kijinga Inayokufanya Upoteze Muda)
6. Umbea na Majungu
Unapoteza muda kuongea maneno ya uchonganishi juu ya mtu Fulani unapiga umbea na majungu. Unaongea maneno ambayo yanaleta majeraha katika maisha ya watu, unapandikiza chuki kwa watu kwa kupiga majungu unapoteza muda wako bure kupiga umbea na majungu bila malipo yoyote ni hatari sana tumia muda wako kujenga na kuongea thamani yako katika jamii ya yako na acha kuwa mtu wa umbea na majungu kila siku.
7. Kuhudhuria Vikao au Mikutano Ambayo Haikupi Faida
Kuna vikao vingi sana katika jamii zetu, mikutano mingi ya kila siku ambayo haina matokeo chanya kwetu bali ni kupoteza wakati wako. Leo nakuomba sema HAPANA kwa vikao au mikutano ambayo haikupi faida yoyote ambavyo vinakula muda wako bure ambao muda huo ungeweza kutumia vizuri kuboresha maisha yako au hata kuongeza thamani katika jamii yako.
Hivyo basi, acha kutumia muda wako kudhurura ovyo yaani kutembea bila sababu ya msingi, tumia muda wako vema, muda ni mali katika karne hii usikubali mtu akupotezee muda kwa kitu ambacho hakina manufaa kwako fanya kile ambacho unatamani kufanya kwa muda huu katika Nyanja zote usisubiri ruhusa ukiendelea kusubiri ruhusa ndio unazidi kupoteza muda na umri pia unakwenda omba samahani kuokoa muda, Muda siyo rafiki na maisha ni mafupi .
Makala hii imeandikwa na Deogratius Kessy ambaye ni mwandishi, mhamasishaji na mjasiriamali, unaweza kuwasiliana naye kupitia namba 0717101505 au kwa barua pepe deokessy.dk@gmail.com au unaweza kutembelea tovuti yake www.actualizeyourdream.blogspot.com

Tabia Ya Mtu Ni Kama Kikohozi, Na Jinsi Ya Kujua Tabia Ya Mtu Kabla Hujamwamini.

Mara nyingi watu wengi hujaribu kuficha uhalisia wao kutokana na mazingira fulani ambayo wanaona wakikunjua makucha yao wataonekana vibaya, wengi wamefanikiwa kwenye eneo hili kwa kiasi fulani ila hushindwa kumaliza kama walivyotarajia. Katika maisha yangu nimefanikiwa kuishi na makundi ya aina mbalimbali nichukulie mfano mdogo wa kundi niliowahi kuishi nalo; wakati naanza maisha mapya kabisa ya jeshi la kujenga taifa 2009 wakati huo wanafunzi wa kidato cha sita walikuwa hawaendi tukiacha kipindi cha miaka ya nyuma na sasa wanavyoenda, na nakukumbuka majengo mengi yaliyajengwa tukiambiwa wanakuja kwa mjibu wa sheria wakati sisi tulikuwa wa kujitolea... wakati naingia kuna watu niliwaona hawezi kabisa kuongea na kuna watu walikuwa waongeaji sana, na kuna watu niliwaona kwa macho wana tabia nzuri na kuna watu niliwaona wana tabia mbaya lakini jinsi siku zilivyokuwa zinaenda wale niliowaona hawezi kuongea ndio walikuwa wasemaji wazuri kuliko wale walioonekana wanaweza kuongea na wale walioonekana wana wapole na tabia njema walikuja kuonekana ni wabaya kuliko wale walioonekana wabaya japo sio wote... nataka kusema nini hapa baada ya mfano huo japo umeanza kujiuliza sasa huyu Samson haya mambo ya Jeshi ameyatolea wapi TULIA KWANZA.
Tabia ya mtu nzuri haiwezi kufunikwa na tabia mbaya hata kama utachukua muda kumwelewa lakini matendo yake na zungumza yake itakuonyesha huyu ni mtu wa namna gani, anaweza akajitahidi kuendana na kundi alilolikuta lakini utashangaa ikifika eneo fulani anaonekana sio mwenzao, naona hujanielewa ni hivi kama umepanda gari na askari wa usalama barabarani amevaa tu kiraia halafu dereva/konda akaanza kufanya upuuzi utamwona akinyanyua mdomo yeye mwenyewe kumkemea hata kama mtakemea wote lakini kemea yake itakuwa tofauti.
SOMA; Matatizo Yote Ya Mahusiano Yanaanzia Hapa... Sehemu Ya Pili(2)
Tabia ya mtu mbaya pia huwezi kuifunika kwa tabia nzuri, japo utaweza kufanya mbinu ya kuiweka vizuri mwisho wa yote utabaki kuonekana wewe sio mtu mzuri maana ubaya wa mtu haupo kwenye macho bali ndani ya moyo wa mtu ndipo zinapotoka takataka zote hata akifanya nini ukweli utabaki palepale, ndio maana wengi wanasema aisee fulani nilimwona ni mpole na anajituma lakini siku hizi amekuwa ana tabia mbaya sio amekuwa na tabia mbaya ni kitu kilichokuwa ndani yake na kama hakuwa nacho ujue uharibu umeanza muda mrefu ndani ya moyo wake sasa hayo unayoyaona ni matokeo tu ya matunda ya kile kilichoanza siku nyingi kabla mwingine hajakiona.
Ukiona mtu uliyemwamini amebadilika ghafla jua sio ghafla ni katabia chake sema alivaa tu kasura cha uzuri wa nje ila ndani kwake sura halisi ndio hiyo tabia unayoiona, ni sawa na rafiki yako umempa taarifa kuwa utamtembelea kwake leo au wiki ijao nakwambia hata kama ni mchafu kiasi gani siku hiyo lazima ajitahidi kufanya usafi wa hali ya juu iwe kwa kufanyiwa ama kufanya yeye lazima ahakikishe mgeni wake aone hayo ndio maisha anayoishi.
SOMA; Maisha Ni Mchezo Na Sheria Za Kuushinda.
Unapata picha gani hapa? wengi kumbe maisha wanayoishi hawayapendi ila hawataki kuyaacha wameng'ang'ana kuishi maisha ya kinyonga lakini tatizo lao limebaki palepale. Kwa hiyo tunaona unaweza kujizua kukohoa (kubanja) kutokana na mazingira uliopo ila mwisho wa saa bila wewe kujua utaachia tu kikohozi chako tena kwa kishindo kikubwa kuliko awali.
Sasa basi mtu usiyemjua yaani mmefahamiana naye muda mfupi usipende kumwamini asilimia zote hata mimi usijilazimishe kuniamini hata kama unaniona naandika maneno mengi mazuri hii isikufanye ukaniamini haraka nenda taratibu mpaka uhakikishe moyo wako umeniamini, ndio maana wengi wakitokewa na jambo baya kuhusu mtu aliyemwamini kwa haraka utasikia aisee moyo wangu ulikuwa unakataa kabisa nisimpe kitu fulani ama nisimwambie kitu fulani, hivi hujawahi kuona unamuulizia mtu fulani kwenye makazi yake ama kazini kwake unatajiwa na alivyo, mfano; aisee unamuulizia yule kijana mwizi mwizi sana wa vitu vya watu, unamuulizia yule dada anayetoa sana mimba au unamuulizia yule kaka anayetembea sana na wadada yaani huyo kaka malaya sana jana tu ameingia hapa na mabinti wawili tofauti tofauti wa tatu wamegongana na mwenzake wameleteana fujo kweli... yaani badala ya kuelekezwa unapewa shutuma zake.. hiyo tunasema huwezi kuzuia kikohozi kwa kukibana muda mrefu hata kama mtu atavaa sura ya ubaya kama sio mbaya itajulikana tu.
Mwisho nikuase kwamba usihangaike kumjua mtu wala kumfuatilia sana habari zake... zipo nje nje tu ndio maana ukimgusia tu kwa kumsifia kitu fulani watu wanaguna wanajua unachoongea hujui chochote.
Makala hii imeandikwa na Samson Ernest, waweza wasiliana nami kwa njia ya WhatsApp 0759808081, email; samsonaron0@gmail.com
Nakutakia siku njema yenye mafanikio makubwa kiroho na kimwili.

Una Nini Cha Tofauti Mpaka Watu Wakufuate Na Kukusikiliza? Jua Hapa.

Katika dunia ya sasa ni kawaida sana kukutana na mtu akimthamini na kumjali mtu kwa kuwa ipo faida anaipata au ananufaika kwa njia moja au nyingine. Mfano huenda ni katika eneo lako la kazi, pengine bosi wako kwa kuwa tu wewe ni mfanyakazi mzuri basi ataonekana kukubali na kukuheshimu sana tu kumbe anafanya hayo kwa kuwa tu ipo faida anaipata kwa uwepo wake mahali pale pa kazi, pengine usipokuwepo naye nafasi yake itakuwa hatarini maana ni mapengo mengi unayaziba na kumfanya aonekane kuwa bora sana mahali pake pa kazi, unampa thamani mahali pale, hivyo naye anaonekana kukuthamini tu kwa kuwa ana anachopata kwako. Ile thamani uliyo nayo inamlazimisha kukujali na hata kukutumia zaidi.
Au kwa wanafunzi unapokuwa shuleni unakuta kuna mwenzio ana uwezo zaidi kwenye somo fulani hivyo unakuta mtu yule anategemewa na wengi na anaweza kuonekana kupendwa na wengi kwa kuwa anawasaidia wengi kuweza kufanya vizuri kwenye masomo anayowasaidia kuwafundisha ili waweze kuelewa zaidi, ukiangalia kwa kawaida unaweza ona kama yule mtu anapendwa na wengi, lakini ukiangalia zaidi utagundua pale hapendwi mtu bali kipo kitu cha thamani ambacho kinapendwa kwa mtu yule, kipo kitu watu wanakifuata kwa mtu yule ambacho pengine kwa wakati ule hakuna mahali pengine tena wataweza kupata kitu hicho, hivyo naweza sema wanakuwa hawana namna mbadala ya kupata huduma ile, wanalizimika kumkubali mtu yule hata kama hawampendi, wanalazimika kumsikiliza na wanakubali kufundishwa naye maana hakuna mwingine anaweza kufanya lile.
SOMA; Katika Kula Ujana Usifanye Mambo Haya Matano, Utajutia Maisha Yako Yote.
Pengine unaweza kukutana na mtu ukamshangaa na usimwelewe kwa kuwa anaambatana na mtu fulani, pengine wewe ukiangalia kwa macho yako ya kawaida unakuwa huioni thamani ya huyo mtu, huoni cha maana alichonacho cha kumfanya mtu mwingine asitake kuwa mbali naye, unajitahidi sana kukiona hicho lakini huoni, lakini wewe ukiwa katika hali hiyo kuna mwingine ameona thamani kwa huyo mtu, na anajua namna ya kuipata, hivyo anahakikisha anamtumia huyo mtu kuweza kupata kile mtu anacho, anamtumia yule mtu kuweza kufika pale anaelekea, usiishie kushangaa ni kwa nini mtu fulani anamkubali sana yule, usiwe mwepesi kumpuuza au kuona amepotoka wakati huelewi hasa ni kwa nini anafanya vile. Kama ukiwa mwelewa na mjanja mwenye nia ya kujifunza na kueleweshwa utatumia hekima na busara ili kuweza kuona kile mwenzio anaona kwa huyo mtu, utauliza na ukielekezwa uwe tayari kuheshimu hata mawazo ya wengine, uweze kuona thamani hata kwa wengine, hata kama wewe unadhani unajua kila kitu lakini tambua wapo wengine pia wanaoweza kuwa na uelewa kuliko wewe.
Wakati mwingine unaweza kukutana na mtu na ukamshangaa kwa nini anaambatana na mtu fulani maana wewe kwa viwango vyako na vipimo vyako unaona yule mtu si sahihi au hana sifa za kuweza kuwa na mtu yule na pengine unaweza kujaribu hata kumshawishi asiwe na mtu yule, pengine hata kwa kumweleza ni jinsi gani unaona hafai kwa kuelezea yale mabaya yake au madhaifu yake lakini cha ajabu unashangaa pamoja na hayo bado mtu yule anaendelea na msimamo wake wa kuambatana na mtu yule. Tambua yule ni mtu mwenye uelewa wa kutosha naamini ni yeye anaelewa ni kwa nini anaambatana na mtu yule, anajua ni kwa nini anashirikiana na mtu yule kwenye shughuli zake, yeye ndiye anajua ameona nini kwa mtu yule, pengine wewe huoni thamani kwa mtu yule, lakini yeye ameiona hiyo na hiyo ina nguvu kuliko sauti yako ya kumwaminisha kinyume, sauti yako anaona kama kelele tu, unatakiwa ujiulize unavyomwambia hayo wewe unaonekanaje kwa mtu huyo? Kwanini aamini unayosema? Una nini cha kukufanya aamini unachosema? Je una sababu za msingi za kuona yule mwingine hafai? Huyo ambaye hafai unamwelewaje? Unamfahamu sawasawa?
SOMA; Ushauri Kwa Waajiriwa Wapya Wote Wa Mwaka Wa Fedha 2014/2015
Tambua kuwa mtu yule yule unayemuona hafai , ipo sehemu anafaa sana kwa kuwa wale watu wameona kinachofaa au wameona thamani kwa mtu yule, huenda wamechagua kuiona thamani au mazingira yamewalazimisha kuona hivyo , maana hata kama hawamkubali au kumpenda lakini ndiye anayeweza jambo fulani ambalo wanalihitaji ili kuweza kufikia malengo yao katika maisha yao, hivyo wanalazimika kuwa na mtu yule, kumtumia mtu yule kama ngazi ya kufika kule. Kila mtu anaweza kumuona mtu yule yule kwa tofauti, inategemea kama una mtazamo gani juu ya wengine, kuwa na mtazamo chanya, tarajia kuona thamani hata kwa wengine, na ukiiona kama inakufaa itumie, usione aibu kusaidiwa hata na mtu unayeona hafai au hana hadhi ya kukusaidia au kukuelekeza jambo fulani, kumbuka Muumba wetu anaweza kumpa hata yule unayeona hafai thamani na ukalazimika kwenda kuhitaji huduma yake hata kama umemdharau sana, hata kama ulishaona hawezi kukuhudumia.
Katika maisha unavyoishi hebu jiulize una nini? Kwanini watu wakae chini wakusikilize? Unacho cha kuwasikilizisha? Kwanini niache wote nije kwako? Nitapata nini cha maana au cha tofauti?
Imeandikwa na Beatrice Mwaijengo
+255 755 350 772

Kama Umewekeza Kwenye Majengo Yafahamu Magonjwa Sugu Yanayo Athiri Majengo.

Kama ilivyo kwa viumbe hai kuathiriwa na mazingira wanayoishi ndivyo ilivyo kwa viumbe visivyo hai ikiwemo majengo. Majengo huweza kuhimili mazingira kutokana na namna yalivyobuniwa na kujengwa katika mazingira yaliyopo. Hata ujenge majengo mazuri na makubwa kiasi gani, kama hayajabuniwa na kujengwa kutokana na mazingira husika majengo hayo huwa hatarini na watumiaji wa majengo hayo huwa kwenye majanga mazito kwa kujua au kwa kutokujua. Mbaya zaidi huwa hasara kwa mmiliki wa jengo husika. Kwa mujibu wa taaluma na ufahamu nilionao unaweza kujenga majengo mahali popote iwe ardhi tambalale, mabondeni, milimani, kando ya mito na hata baharini maadamu ikidhi ubunifu na ujenzi uzingatie mazingira husika. Kwenye makala zijazo nitaeleza hayo kwa ufasaha zaidi, lakini leo naomba uyafahamu magonjwa yanayoathiri majengo yako ili uweze kuyakinga na yadumu kwa muda mrefu kwa kuwa ujenzi ni uwekezaji na hugharimu fedha nyingi.




Nyufa
Nyufa ni uwazi unaosababishwa na utengano wa mihimili ya jengo uliokuwa muunganiko hapo awali. Nyufa zinapotokea kwenye jengo tambua kuwa jengo lako lipo katika tabu fulani, nyufa ni lugha kuu ya majengo kumjulisha mtumiaji kuwa lipo kwenye kashkashi. Nyufa husababishwa na matokeo mengi na utagundua tatizo kutokana na mwelekeo wa nyufa hizo na mahali ulipotokea. Kama nilivyoeleza hapo awali udhaifu wa majengo ni matokeo mabovu ya ubunifu na ujenzi kwa mazingira husika. Unachopaswa kufanya hapa ni kugundua tatizo na kuliweka sawa ndipo uzibe ufa. Watu wengi huishia kuziba ufa pasipo kushugulikia chanzo chake, kitendo hiki ni sawa na kuuficha ufa ili usiendelee kuuona machoni lakini tatizo linabaki palepale.
SOMA; Mambo Ya Kuzingatia Na Njia Bora Za Uwekezaji Wa Majengo Kwa Gharama Nafuu.
Kutitia kwa majengo
Ni kawaida kutitia kwa majengo lakini linapozidi kiwango huwa ni tatizo na hatari kwa watumiaji. Tatizo hili husababishwa na ukadiriaji hafifu wa tabia za udongo kwenye kiwanja cha jengo husika. Mara nyingi jengo hutitia kutokana na aina tofauti za udongo kwenye kiwanja kimoja au kimo cha msawazo wa msingi kuwa tofauti, pia ubunifu hafifu wa udongo kulingana na uzito wa jengo husika. Hatari kuu huwa kwenye majengo marefu na kwenye vyoo vya shimo. Cha kusikitisha mara zote serikali yetu huwajengea watoto wetu vyoo vya mashimo lukuki mashuleni jambo ambalo ni hatari kutokana na udhaifu wa muundo wa vyoo hivyo. Ni muhimu kutenganisha shimo na chumba cha choo kwa usalama wa watumiaji ili tusiendelee kupoteza watu na kufunga shule eti vyoo vimebomoka.
Majengo kupitisha maji
Maeneo mengi ya Tanzania yamezungukwa na vyanzo vya maji ambavyo ni bahari mito na maziwa hali inayosababisha ardhi yake kusharabu maji karibu majira yote ya mwaka na mbaya zaidi wakati wa mvua. Maeneo mengi ya pwani majengo mengi yameathiriwa na tatizo hili na hata limekuwa kero kwa wakazi na watumiaji wa majengo hayo. Majengo hupitisha maji kwa njia ya sakafu na kuta mithili ya chujio au chemchemu. Mara nyingi utagundua kwa kuona ardhi yake imetota maji wakati wote wa majira ya mwaka. Pia majengo mengi ya maeneo haya yanaoza na kutitia kwa haraka na hata mashimo ya vyoo vya maeneo hayo huinuka kwenda juu na siyo chini jambo ambalo ni hatari kwa afya za wakazi. Katika hali hii kuta na sakafu huoza kwa haraka kutokana na maji yaliyopo chini ya ardhi kuwa na kemikali mbalimbali zilizopo kwenye maji hayo. Katika mazingira haya lazima yatumike malighafi sahihi za kuzuia maji hasa wakati wa ujenzi.
SOMA; Kama Utashindwa Kufanya Chochote Utakachojifunza, Basi Fanya Hiki Kimoja Tu, Na Maisha Yako Yatagusa Wengine.
Kuoza kwa kuta
Moja ya masahibu yanayoyakumba majengo ni kuoza kwa kuta za tofali au chuma. Hali hii hutokana na unyevunyevu na kemikali mbalimbali kupitia maji kukaa kwa muda mrefu kwenye kuta hali inayoathiri ubora wakuta hizo. Pia hali hiyo husababishwa na kumea kwa mimea au kupanda maua kwenye viambaza vya kuta ambapo baadhi ya mimea hiyo kusababisha ukungu wa kijani kwenye kuta ambao huzalisha fangasi mbalimbali wanaokula kuta. Pia kitendo cha kumwagilia maua kwenye kuta huozesha kuta haraka. Kinga kuta zote zithiathiriwe na hali ya hewa na maji pale inapolazimu na Usiruhusu mimea kumea kwenye viambaza vya kuta.
Kuoza kwa paa
Unapaswa kutambua kuwa kila kilichoumbwa kina mwisho, ndivyo ilivyo hata kwenye majengo, kila aina ya malighafi iliyotumika hufika mwisho wake kwa wakati tofauti kulingana na ubora na namna yalivyotumika katika ujenzi. Kuoza kwa paa hutegemea ubora na aina ya malighafi zilizotumika bila kusahau na kimo cha mwinuko wa paa hilo. Paa huathiriwa na hali ya mazingira ya eneo husika, mfano paa zilizopo ukanda wa pwani huthiriwa na chumvichumvi zinazobebwa na mikondo ya upepo uvumao kutoka baharini hali inayosababisha paa kuoza haraka, pia hali ya mwinuko ukiwa mdogo husadia paa kuhifadhi takataka mbalimbali ikiwemo majani ya mimea, hali hii ya uchafu kukaa muda mrefu huozesha paa haraka. Unapaswa kuweka paa lenye ubora kulingana na mazingira halisi. Inasikitisha kuona hadi leo hii bado kuna nyumba za serikali zimeezekwa vigae vya asbestos ambavyo ni hatari na vimepigwa marufuku kwa matumizi ya binadamu.
Kusinyaa na kutanuka kwa milango na madirisha
Kuna shida sana hapa, watu wengi hujikuta wakiwalalamikia sana mafundi kuwa hawafai na wamewatia hasara. Kuna aina nyingi za malighafi zinazotumika kutengenezea milango na madirisha, kila aina ya malighafi hizo zina faida na hasara zake. Karibu aina zote za malighafi zina tabia ya kusinyaa na kutanuka kutokana na hali ya hewa (jotiridi) ya mazingira nyumba zilipo. Tumia mbao ngumu (treated hardwood) ili kuondokana na tatizo hili, usitumie mbao mbichi zitakusumbua sana siku zijazo. Kwa wale wanaotumia madirisha na milango ya vioo na aluminiam ni lazima wayapachike na kufitisha kwenye mbao na siyo moja kwa moja kwenye kuta ili kuruhusu hali ya kusinyaa na kutanuka, usipo fanya hivyo aluminiam hupinda na kuleta shida ya kufunga na kufungua. Pia kama unatumia madirisha haya ya vioo (sliding windows) ni lazima yawe makubwa ili kuruhusu hewa kuingia na kutoka kwa haraka kwa kuwa madirisha haya hufunguka nusu tu. Kumbuka kuweka vitasa sahihi kulingana na matumizi, Zingatia sana haya kwa kuwa kila unachoweka kwenye nyumba ni fedha hivyo usiache watu wafanye hovyohovyo tu, ni kero na hasara, wewe na wateja wako hamtafurahia mazingira ya nyumba hiyo.
Mwandishi wa makala hii ni mwanataaluma na mshauri wa ujenzi.
Anapatikana kwa: Simu: +255 685 729 888, Email: kimbenickas@yahoo.com

Ushauri Kwa Waajiriwa Wapya Wote Wa Mwaka Wa Fedha 2014/2015

Habari mpenzi msomaji , na karibu tena katika usomaji wa makala kupitia tovuti hii kama ukitumia vema makala hizi za kila siku zinazotolewa na blog hii hakika utaboresha maisha yako kwa namna moja au nyingine.
Awali ya yote nitumie fursa hii kuwapongeza wote walioajiriwa mwaka wa fedha 2014/2015 katika sekta mbalimbali. Mara nyingi watu huwa wanajisahau sana pale tu wanapopata ajira. Leo napenda kukushauri mambo ya msingi ya kufanya ili uendelee kuboresha maisha yako.
Vitu ambazo unatakiwa kuvifanyia kazi ni;
1. Kuweka Akiba
Huwezi kufikia uhuru wa kifedha kama wewe ni mtu ambaye hujui kuweka akiba, mtu ambaye ukipata mshahara unatumia wote na kusubiri mwingine mwezi ujao. Hii ni tabia mbaya sana ambayo itakuletea athari kubwa sana mbeleni akiba haiozi hivyo basi ya kupasa kuweka akiba weka asilimia 10 ya mshahara wako katika akaunti maalumu ambayo itakusaidia ukiwa na dharura.
Umuhimu wa akiba utaujua pale tu utakapopata tatizo au dharura katika maisha kwani matatizo yapo kila siku na hakuna binadamu ambaye hana tatizo kila mtu ana matatizo yake hivyo basi anza sasa kuweka akiba ili ufikie mafanikio hapo mbeleni unapokuwa huna ajira.
SOMA; Kama Unataka Kumaliza Matatizo Yako Ya Fedha Fanya Kitu Hiki Kimoja.
2. Usitegemee Chanzo Kimoja Cha Mapato
Kuendelea kutegemea chanzo kimoja cha mapato yaani ajira ni hatari sana .hivyo basi nakushauri mbinu mbadala ya kuwa na vyanzo vingine vya mapato tofauti na ajira ambayo unayo kwa sasa buni miradi mbalimbali ambayo itakusaidia na kukupelekea kuwa na uhuru wa kifedha. Anza maandalizi sasa ya kuandaa kuwa na vyanzo vingine vya mapato tofauti na ajira.
3. Ishi Chini ya Kipato Chako
Hili limekuwa ni tatizo kwa watu wengi kuishi juu ya vipato vyao ,watu wamekuwa wanaishi maisha ya kuiga sana bila kuangalia kipato chake ni kidogo maisha ya kushindana ni mabaya sana. Kwa mfano unakuta mtu kipato chake ni laki mbili lakini mtu huyo anaishi maisha juu ya laki mbili hapo ndipo tatizo linapoanzia.
Kuishi juu ya kipato chako kitakupelekea kwenye madeni na kushindwa kufanya shughuli za kimaendeleo kabisa kwa sababu tu unaishi maisha ambayo siyo yako ishi maisha yako mwenye na wala hupaswi kuiga.
4. Kuwa na Nidhamu ya Pesa
Hata uwe na hela kiasi gani kama huna nidhamu na pesa ni tatizo sana, acha tabia ya kununua vitu kwa hisia kwa sababu tu Fulani kanunua na wewe unapata shauku ya kuwa nacho usitumie pesa ovyo tumia tu kwa mahitaji muhimu sana, punguza au acha kabisa starehe ambazo zinamaliza pesa zako kila siku acha kuwa mtumwa wa kisaikolojia wa uvutaji wa sigara, ulevi nakadhalika.
5. Endelea Kujifunza Kila Siku
Kumaliza shahada au stashahada siyo wa kusoma au mwisho wa kujifunza. Unahitajika kujifunza kila siku ,unahitajika kukua kila siku kesho uwe zaidi ya leo ulivyo sasa, ongeza maarifa chanya kila siku katika maisha yako. Chakula cha ubongo wako ni maarifa na akili yako ni kiwanda cha maarifa soma, soma, soma vitabu kadiri uwezavyo vitabadili maisha yako ,jifunze kwa waliofanikiwa utafika mbali kuliko kuendelea kuridhika na kujiona kuwa umeshamaliza chuo huna haja tena ya kujifunza.
SOMA; Kozi 1100 Unazoweza Kujifunza Bure Kupitia Mtandao.
Kwa hiyo , ili uweze kufika safari yako ya kimafanikio ya kupasa uwe na malengo na mipango juu ya maisha yako kuishi bila malengo ni sawa na kusafiri safari ambayo hujui unapokwenda ni wapi. Jali sana afya yako kwani katika safari ya mafanikio kitu cha kwanza cha kuzingatia ni afya. Kumbuka kujilipa pia 10% ya kipato chako pay yourself first hivyo basi zingatia kujilipa kwanza wewe kwani wewe ndio unafanya kazi na unawalipa watu wengi lakini unajisahau kujilipa na hela unayojilipa ifanyie uwekezaji ili ikusaidie.
Makala hii imeandikwa na Deogratius Kessy ambaye ni mwandishi, mhamasishaji na mjasiriamali, unaweza kuwasiliana naye kupitia namba 0717101505 au kwa barua pepe deokessy.dk@gmail.com au unaweza kutembelea tovuti yake www.actualizeyourdream.blogspot.com

Hatua Saba (07) Muhimu Za Kukamilisha Malengo Yako Makubwa.

Watu wengi hufikiri kuwa na lengo lilio fasaha pamoja na kuwa na mtazamo chanya kuhusiana na ukamilishaji wa lengo ndio msingi mkuu wanaohitaji ili kuweza kuwa na furaha pamoja na kufanikiwa. Lakini kumbe hata kabla hujaanza safari yako ya kukamilisha lengo lako ni muhimu kuwa na mipango hatua kwa hatua inayokuhakikishia uwezekano mkubwa wa kukamilisha lengo lako.
Hapa ninakuletea hatua saba zitakazokuwezesha kukamilisha lengo lolote ambalo unajiwekea
1. Amua ni nini hasa unakihitaji katika kila eneo la maisha yako. Unahitaji kufafanua lengo lako katika lugha rahisi kiasi kwamba mtoto mdogo aweze kuelewa. Mfano unaweza kusema lengo lako ni kuwa na fedha nyingi, lakini uwingi wa fedha unazotaka haujaweka ni fedha nyingi kiasi gani. Sasa kutokuwa fasaha katika lengo kunakupelekea kutokuwa na hamasa na kufanya maamuzi ya kukamilisha lengo.
2. Andika lengo lako na lifanye liwe linaweza kupimika. Lengo ambalo halijaandikwa linakuwa ni lengo ambalo halijahuishwa au halijapewa nguvu ya kuwa hai. Ukilifanya lipimike maanake unakuwa umetengeneza tageti unayotaka kuifikia.
SOMA; Jinsi Ya Kutengeneza Kipato Cha Ziada Ukiwa Unaendelea Kufanya Unachofanya Sasa.
3. Weka ukomo wa kukamilisha. Unahitaji kuwa fasaha ni lini unahitaji kukamilisha lengo husika. Sehemu ya ubongo inayoitwa “subconscious” inapenda kuwa na ukomo na hii inakusaidia kuwa na nguvu na kukupa hamasa ya kuelekea kufanikisha lengo husika
4. Ainisha vikwazo ambavyo unahitaji kuvivuka ili kukamilisha lengo. Fahamu kitu gani kinaweza kwenda tofauti. Fahamu ni kitu gani kipo kati yako na lengo. Fahamu kwa nini bado haupo katika lengo lako.
5. Tambua maarifa na ujuzi wa ziada ambao utahitaji ili kuweza kufikia lengo lako. Ili kuweza kufanikiwa kukamilisha malengo ambayo hujawahi kuyakamilisha hapo kabla unahitaji kujifunza na kuwafanya vitu vya tofauti ambavyo hujawahi kufanya kabla.
6. Watambue watu ambao utawahitaji wakusaidie au waungane nawe ili uweze kufikia malengo yako. Kufikia malengo makubwa unahitaji kuwa natimu ya watu wengi wa kukusaidia. Kwa hiyo unahitaji kuwa na ufasaha ni watu wa aina gani hasa unaowahitaji ili uweze kuwa na timu ambayo itakupa msaada unaouhitaji.
7. Tengeneza orodha ya maelezo kwa kila kipengele ambavyo nimeanisha hapo juu na uweke mpangilio katika mfuatano yaani kipi kinaanza na kipi kinafuata na pia ni muhimu kuwa na kipaumbele. Ni muhimu kujua kipi unahitaji kwanza, kipi ni muhimu.
Baada ya kukamilisha hatua hizo saba ni muhimu kufanya kila siku japo kwa udogo sehemu ya kufikia lengo lako.
Mwandishi: Goodluck Moshi
Mawasiliano:
Whatsapp: +255 753 201 994, Telegram: +255 658 201 994, Barua pepe: eng.gmoshi@gmail.com Facebook: Goodluck Moshi
Pia unaweza kutembelea blog yake www.stadizamafanikio.blogspot.com kujifunza zaidi.

Kabla Hujakubali Kila Unachoambiwa, Kumbuka Jambo Hili Moja Muhimu Sana.

Binadamu tunaweza kuwa tunaona kitu kimoja kwa namna tofauti kabisa , hii inatokana na kutofautiana mitazamo tu au yaweza kuwa ni kutokana na vitu ambavyo tumejifunza na kuzisikia sana, ndiyo vitu ambavyo tumeaminishwa kuwa vipi hivyo. Na sisi labda kwa ujinga au uvivu wa kutaka kuhoji au kuchimba mambo zaidi basi tumeamua kukariri hivyo na hatupo tayari kusikia kitu kilicho kinyume na tunachoamini. Hata akitokea mtu wa kutuelewesha au kutuambia kitu kipya tunakuwa hatupo tayari kujifunza hicho, hata tukisikiliza hatusikilizi kwa lengo la kujifunza au kuelewa bali tunasikiliza tu ili tuelezee msimamo wetu , tunavyoelewa sisi. Si jambo baya kuelezea kile unajua au kuelewa lakini ni vizuri kama utakuwa tayari pia kujifunza vitu vipya, naamini mwanafunzi hachagui nini afundishwe au asikie, lakini akifundishwa kama hajaelewa huuliza maswali kwa nia ya kueleweshwa zaidi na si kwa nia au lengo la kubishana.
SOMA; Jinsi Ya Kujua Kama Unachofanya Ni Sahihi Katika Maisha Yako.
Tukiangalia katika wakati tulionao wa maendeleo ya sayansi na teknolojia, kuna vitu vingi vizuri sana tu lakini vipo na vibaya vilivyokuja na hii teknolojia, Hivyo kwa sababu hizo nilizosema mwingine anaweza kuona kuwa kukua kwa teknolojia kuna madhara sana, hakufai, mfano huu utandawazi wengi wanauona kama jambo baya lisilofaa kabisa, na wengi wanatumia nguvu nyingi sana kujaribu kufanya kila mtu aone kuwa ni kitu kisichofaa kwa jamii, na wanaposema hivi wana sababu za msingi za kuamini wanavyoamini, maana kuna mambo mengi yasiyofaa yanaendelea mitandaoni, watu wanaiga mambo yasiyofaa humo na hata maadili ya jamii yanamomonyoka, lakini kwa kuwa tu wapo wanaoona hivyo haimaanishi kwamba ni kweli utandawazi ni mbaya na hauna faida, zipo faida nyingi tu za utandawazi ikiwa utautumia vizuri unaweza kunufaika sana tu. Wapo watu wengi wamefaidika sana na mitandao hii ya kijamii kwa kukutana na watu wapya ambao wamewafundisha vitu vingi, watu wamenufaika kiroho na hata kijamii kwa namna ambavyo wametumia mitandao hii ya kijamii, maana kupitia hii hauhitaji kuonana na mtu ili muweze kufundishana au hata kujadilia baadhi ya mambo, pia inasaidia hata kutunza muda na hata gharama za kukutana au kumfuata mtu mahali fulani kwa ajili ya majadiliano, naweza kuwa hospitali, barabarani na nikasoma vizuri au hata kuhudhuria mafundisho au hata ibada bila shida kabisa.
SOMA; Kuna Watu Hawa Ambao Hawawezi Kukuelewa, Wajue Na Waepuke Ili Uweze Kufikia Mafanikio.
Pia katika maisha haya iwe kazini , nyumbani au popote ulipo unaweza kukutana na mtu akakuambia kuwa mtu fulani ni mbaya sana au ana sifa hizi na hizi na pengine akakupa mabaya tu ya huyo mtu, akajitahidi kukuelezea na kukufanya umuone mtu huyo hafai kabisa katika jamii, au hafai kuwa rafiki yako kabisa na pengine si mtu hata wa kufanya naye biashara n.k, Sasa hapo ni wajibu wako wewe kama mtu unayejielewa na kuelewa kuwa sisi binadamu hatupo kama watu wanavyosema tupo, au kwa kuwa fulani ameniona mimi sifai au mimi ni mzuri haimaanishi kwamba kila mtu ataniona hivyo, hivyo hata kama umeambiwa nini kuhusu mtu fulani hebu usiende kwake ukiwa na hiyo picha uliyopewa, bali amua kuona mwenyewe kama kweli yupo kama ulivyoambiwa au yuko tofauti na vile, maana ukienda kwa namna ulivyoambiwa unaweza kujikosesha fursa nyingi sana kwa ujinga wako wa kutotumia akili na maarifa uliyopewa na Muumba wako, mtu mwingine anaweza kukuambia mtu fulani yupo hivi kwa kuwa tu ana chuki na huyo mtu au pengine hata hamjui huyo mtu, au alisikia tu watu wakisema hivyo lakini hajathibitisha mwenyewe
Tambua kuwa hatuwezi wote kuona jambo lilelile sawasawa maana kila mtu ni wa pekee, hivyo ni vyema kuheshimu mtazamo wa kila mtu lakini usiutumie mtazamo wa mwingine kama ndio mamlaka ya mwisho ya wewe kuona. Hivyo hata kama umeambiwa kitu fulani hakifai hakikisha kuwa unatumia akili zako na utashi wako kufanya uchunguzi kuona kama kweli kitu hiki kipo kama unavyoambiwa kipo, ni muhimu kutambua kuwa binadamu tunaona vitu vilevile kwa tofauti, ndio maana kuna mtu ni mzuri kwangu lakini wewe waweza kumuona mbaya au hafai kwa kuwa kila mtu ana vigezo vyake vinavyomfanya aone anavyoona, usiishi kwa kufanya yale uliyoambiwa bali ishi kama vile unavyotakiwa kuishi na Muumba wako, umuone kila mtu kuwa bora, mwenye uwezo wa kufanya jambo la maana maishani, usimkadirie mtu kwa kusikia maneno ya kuambiwa kamwe maishani.
Imeandika na Beatrice Mwaijengo
Mobile number: +255755350772