Jinsi Ya Kujua Kama Unachofanya Ni Sahihi Katika Maisha Yako.


Kila mtu anapokuja hapa ulimwenguni anakuwa amebeba maagizo maalum ambayo anatakiwa ayatekeleze kwa ajili ya kufanya ulimwengu kuwa sehemu bora ya kuishi. Njia nzuri ya kuweza kujua kile unachofanya kama ni sahihi ni kwa kuyafahamu maagizo uliyobeba ambayo hakuna mwingine zaidi yake anaweza kuyatekeleza. Na maagizo hayo unaweza kuyafahamu kwa kuanza kujitathimini kwa njia ya maswali kama je umeshatambua maagizo uliyoyabeba? Au je una kipaji, uwezo, shauku gani ambayo ni ya kipekee kwako na hakuna mtu mwingine wa aina yoyote anayo isipokuwa wewe tu? Au ya mwisho ambayo ni nzuri zaidi ni kwa kuangalia kile unachokifanya na kujiuliza je unachokifanya ndicho ulichokusudiwa au sababu ya wewe kuwepo hapa ulimwenguni?
Hapa ninakuletea viashiria ambavyo vitakusaidia kujitathmini kama kwanza upo katika kada au eneo sahihi lakini la muhimu zaidi ni lile unalofanya katika hilo eneo ndilo lile unalopaswa au sababu ya wewe kuwepo hapa ulimwenguni.
1. Unakuwa unapenda kile unachokifanya kwa kuwa kinakuvutia , kinakupa shauku na mvuto wa kipekee kukifanya
2. Unakuwa unataka kuwa bora sana katika kile unachokifanya. Na miongoni mwa asilimia kumi ya watu walio bora katika eneo au kada yako unataka na wewe uwepo
3. Unawapenda wale wote ambao wako katika eneo au kada uliyopo na pia unapenda kufikia mafanikio ambayo wao pia wameyafikia
4. Unapenda kujifunza kuhusiana na hilo eneo au kada yako kwa kusoma mambo yanayohusu kada yako, kuhudhuria semina au mihadhara ambayo inazungumzia mambo yanayohusu eneo au kada yako, kusikiliza program za sauti zilizorekodiwa kuhusiana na kada yako. Na zaidi hata iweje unakuwa huchoki kujifunza katika hilo eneo lako.
5. Kada au eneo sahihi kwako ni lile ambalo kwako ni rahisi kujifunza na pia ni rahisi kuweka katika matendo yale uliyojifunza. Ila kwa wengine inaonekana ni vigumu na kwako inakuwa kawaida sana kufanya.

SOMA; Haijalishi Umeshindwa Mara Ngapi…

6. Kutokana na kufurahia kile unachofanya unakuta muda unakuwa kama umesimama kwako na inaweza ikawa imekukolea sana hadi unasahau kula, kunywa hata kwenda mapumziko
7. Mafanikio unayoyapata katika eneo ndiyo inayokupa hamasa ya kipekee na furaha adimu. Na pia unakuwa huwezi kuacha kusubiri au kukaa muda mrefu bila kufanya kitu kikusogeze hatua moja mbele upate mafanikio mengine
8. Unapenda kufikiri kuhusu hilo eneo au kada yako na pia wakati haufanyi kitu unapenda kuzungumza kuhusu eneo au kada yako. Maisha yako yote yanakuwa yamezungukwa na mambo yanayohusu eneo au kada yako
9. Unapenda kuwa na mahusiano na kuwa karibu na watu zaidi ambao wapo katika eneo lako.
10. Na mwisho ni kuwa unapenda kufanya hayo unayofanya kwa maisha yako yote, hutaki kustaafu kuyafanya kwa kuwa unafurahia jinsi unavyoyafanya
Kwa kuweza kutambua eneo au kada yako sahihi ambayo unatakiwa uwe itakusaidia kupata mafanikio na hii itakusaidia kuelekeza moyo wako kufanya vizuri na vizuri zaidi.
Mwandishi: Goodluck Moshi
Mawasiliano:
Whatsapp: +255 753 201 994, Telegram: +255 658 201 994, Barua pepe: eng.gmoshi@gmail.com Facebook: Goodluck Moshi
Pia unaweza kutembelea blog yake www.stadizamafanikio.blogspot.com kujifunza zaidi.

0 comments: