Mambo 20 Niliyojifunza Kwenye Kitabu Kinachoitwa FLIGHT PLAN The Real Secret Of Success.

Habari rafiki, ni matumaini yangu waendelea vizuri. Wiki hii tunaendelea na utaratibu wetu wa kushirikishana mambo 20 niliyojifunza kwenye kitabu. Leo tunaangazia kitabu kinachoitwa FLIGHT PLAN The real secret of success. Kitabu kimeandikwa na mwandishi mashuhuri wa vitabu Brian Tracy. Kitabu kinaitwa Flight Plan au kwa Kiswahili Mpango wa ndege au mpango wa kusafiri kwa ndege. Mwandishi anayafananisha maisha na safari, safari ambayo unaweza kutumia usafiri wowote unaotaka, aidha, gari, pikipiki, kwa miguu au ndege. Mwandishi ameandika kitabu hiki ili kumwezesha msafiri achague njia ya kusafiri kwa ndege ili kufika mapema kwenye kusudio lake. Anaelezea kwamba safari ya ndege ndiyo yenye uhakika wa kufika haraka kuliko njia nyingine. Lakini pia anatoa hatua muhimu za kufanya ili uweze kusafiri kwa ndege. Moja wapo ni kujua unakwenda wapi halafu ndiyo uanze kuchagua aina ya ndege uitakayo. Kitabu hiki ni kizuri na cha kipekee pia.
Karibu tujifunze zaidi.
1. Fanya kazi muda wote wa kazi.
Kuanza kazi na kuimaliza ni changamoto kwa watu wengi. Unakuta unafanya kazi fulani, mara umeacha, umeshika kitu kingine, mara umepokea simu, mara umeanza kuchati, halafu ndio unairudia tena ile kazi. Unagusagusa tena hapo, mara unachepuka kwenye mambo mengine, au unaanza kupiga soga za mambo yasiyo ya maana, au una anza kupiga stori mara za michezo mara stori za siasa, halafu siku inaisha. Kama kweli unataka mpango wako uwe kama wa safari ya ndege ni lazima ufanye kazi uimalize ndio ufanye vitu vingine, weka nguvu zako zote kwenye shughuli hiyo. Mfano ndege ikishapaa, hua haina vituo huko angani, ikianza safari ni mpaka imefika kwenye lengo, na rubani wa ndege anakua makini muda wote kufanya marekebisho pale yanapohitajika. Na ndio maana kama ndege umeambiwa itatumia dk 45 toka Uwanja wa KIA kwenda Dar, itatumia dakika hizohizo. Lakini hebu panda daladala uone, au Coaster, unaweza kuchelewa zaidi ya hata saa moja kwa safari za karibu, safari za mbali unaweza kuchelewa hata masaa 3 zaidi ya yale yaliyokua yamepangwa. Jifunze kufanya mpango wako uwe mpango wa ndege ambayo haisimami mpaka imefika kwenye lengo. Work all the time you work.
2. Chagua mustakabali wako (choose your destination). Siri ya hakika ya mafanikio, ni kwamba maisha ni kama safari ndefu ya ndege, lazima kwanza uanze kuchagua unakotaka kufika, halafu uchague ndege na kukata tiketi halafu ndipo uondoke kuelekea kwenye lengo lako. Hauanzi na kuchagua ndege wakati hujui unakwenda wapi. Aina ya ndege utakayopanda itategemea na unakotaka kwenda. Hivyohivyo mpango unategemea lengo. Unapokua na uhakika wewe ni nani, ni nini unataka, na wapi unataka kwenda utakua na mafanikio mara 10 ya mtu wa kawaida ambaye anaamini maisha ndiyo yanaamua yeye apate nini.
3. Fikiri kwa mrengo wa kutoa suluhisho na si kuendeleza tatizo. Watu hodari ni watu wenye kutoa suluhisho zaidi. Wanafikiria suluhisho ni nini, na nini kifanyike, na sio kufikiri tatizo na nani wa kulaumu. Watu hodari Ni watu wenye mtazamo wa mbele zaidi, wakifikiria zaidi ni hatua gani zichukuliwe haraka ili kudhibiti uharibifu au madhara yanayoweza kusababishwa na tatizo lililotokea. Kua hodari leo kwa kuanza kua na mtazamo wa suluhisho kuliko kutafuta nani mchawi anayepaswa kubeba lawama au kuadhibiwa.
4. Chukua hatua ya Kwanza.
Tofauti ya msingi kati ya ukuu (greatness) na ukawaida (mediocrity) ni katika kuchukua hatua ya kwanza. Watu wakuu (great people) wao wanaweka malengo makubwa, wanapangilia hatua zinazotakiwa kufikia kwenye lengo halafu wanachukua hatua ya kwanza. Wanaanza na hatua ya kwanza. Upande mwingine kwa watu wa kawaida, wanakua na matumaini, ndoto, matarajio, na shauku kadhaa, pengine kama vile watu wakuu/waliofanikiwa wanavyokua. Ila sasa Hofu ya kushindwa na kupoteza/hasara inawazidi nguvu wakati wanapotakiwa kufanya maamuzi ili kuchukua hatua ya kwanza, mwishowe wanarudi nyuma.
5. Kama ukifanya vile ambavyo waliofanikiwa wanafanya, ukafanya tena na tena mpaka ikawa tabia yako basi hakuna kitakachoweza kukuzuia wewe kupata matokeo wanayoyapata.
6. Kupata zaidi, lazima uwe zaidi (To have more, you must first be more). Kwa maneno mengine ukitaka kutengeneza maisha tofauti ni lazima uwe mtu wa tofauti kwanza. Lazima ujifunze na kukua na kupata uzoefu muhimu ambao utakupa hekima na ufahamu wa kuishi maisha ya viwango vya juu. Hakuna njia ya mkato
7. Kila mtu anaanzia chini. Kila unayemuona ambaye yuko juu katika tasnia (field) yako kuna wakati walianzia chini kabisa au hata hawakuwepo kabisa kwenye hiyo tasnia. Lakini Leo hii wamefika hapo juu na wanaingiza kipato kikubwa ambacho ni mara kadhaa ya kipato cha mtu wa kawaida. Habari njema ni kwamba vyote ambavyo wengine wamefanya wakafanikiwa hata wewe unaweza kufanya kama tu utaamua kujifunza ni jinsi gani vinafanyika. Hakuna aliye bora kukuzidi na hakuna aliye nadhifu kuliko wewe, walichokuzidi nacho ni kwamba wao walianza mapema kufanya hivyo vilivyowafanya kufikia hapo. Pengine ungeanza na wao ungekua mbali zaidi. There are no limits except those that you impose on yourself with your own thinking.
8. Katika nyanja yeyote uliyochagua itakuchukua miaka 7 kufikia nafasi ya juu. Watu wengi hawapendi kuusikia huu ukweli, lakini huo ndio ukweli, kwamba eneo lolote, liwe biashara, kazi au ufundi, itakuchukua miaka saba ili uweze kufuzu na kubobea katika viwango vya juu kabisa. Itakuchukua miaka saba biashara yako kufikia mafanikio ya juu. Wengi tukisikia hivi tunakata tamaa na kuacha kujiboresha, tukisahau kwamba hata tukiacha muda ndio unakwenda, hata usipofanya chochote hiyo miaka 7 itapita tu, sasa si bora ukafanya kitu ili baadaye ufaidi matunda ya kuutumia muda vizuri. Maana hata usipoutumia muda utakwenda tu.
9. Moja ya tamaa zenye nguvu kwa binadamu ni kutaka kupata kitu bure, au kwa gharama ndogo sana. Hili ni janga kubwa sana, ndio maana watu wengi wanafikiria njia za kufanikiwa haraka haraka na kwa njia rahisi. Na ndio maana unaona wimbi la vijana kwenye michezo kama kamari na mingineyo mwishowe wanaishia mikono mitupu huku hali zao za mwisho zikiwa mbaya kuliko awali. Ukitaka kumshawishi mtu siku za leo mmpe matumaini ya kufanikiwa haraka haraka bila kuvuja jasho. Hata dini nyingi zenye wafuasi wengi siku za leo ni zile zinazowashawishi watu kua watapata mafanikio ya haraka. Hakuna cha bure. No free lunch
SOMA; Naomba Ufanye Changamoto Hii Ya Siku Kumi, Utabadili Sana Maisha Yako.
10. Jiandae kulipa gharama.
Hakuna kirahisi wakati wa kuanza jambo. Kila ufanikishaji mkubwa ni matokeo ya mamia na maelfu ya juhudi ndogo ndogo ambazo hakuna mtu anayeziona au kuzitambua. Kila tajiri unayemuona ni matokeo ya juhudi, ufanyaji kazi kwa bidii na uzoefu wa muda mrefu. Wakati mwingine hata likizo au mapumziko kwao ilikua ni ngumu, kwa maneno mengine walikubali kulipa gharama. Tatizo kubwa linalokumba watu wengi ni kutokutaka kutia bidii ya vitu ambavyo watu wengine hawavioni. Watu wanataka kila wanachofanya waonekane na wapongezwe. Waliofanikiwa ni wale wanaojitoa sadaka (sacrifice) kwenye mambo ambayo ni nadra sana kukuta wakipongezwa maana mambo hayo wengi hawayaelewi.
11. Maboresho yote ya utu wa nje yanaanzia ndani. Ukitaka kua bora nje lazima uanze kujiboresha ndani, maana ulimwengu wako wa nje ni matokeo ya ulimwengu wako wa ndani. Anza kuboresha jinsi unavyowaza, badili imani ulizonazo ambazo si sahihi, badilisha mtazamo wako, badili jinsi unavyofanya maamuzi n.k. Ukiweza kubadilisha ulimwengu wako wa ndani ulimwengu wa nje na huo utabadilika ili kuakisi mabadiliko yaliyotokea ndani.
12. Ubora wa maisha yako ya baadaye utaamuliwa na uchaguzi na maamuzi unayofanya leo, hususani uchaguzi na maamuzi unayofanya katika yale maeneo ambayo ni ya muhimu katika kufanikisha malengo yako na kufikia hatima ya maisha yako. Uchaguzi wa aina ya kazi au aina ya kampuni ya kufanyia kazi, au aina ya biashara utakayoanza, vinaweza kubadilisha kabisa mwelekeo wa maisha yako. Hivyo unapaswa kutumia muda wa kutosha kufikiri na kuridhika kabisa na uchaguzi unaotaka kufanya kabla ya kufanya uamuzi wa mwisho.
13. Msingi wa utajiri ni thamani. Kama lengo lako ni kufanikiwa kifedha, kuna njia moja pekee ya kuweza kupata mafanikio hayo ya kudumu, na njia hiyo ni kuongeza thamani. Mafanikio ya muda mrefu ya utajiri wa kudumu yanatokana nakuongeza thamani katika maisha ya watu. Mafanikio hayo yanatokana na kuwahudumia watu kwa kuwapatia bidhaa na huduma ambazo wanazihitaji na wako tayari kuzilipia ili kuzipata.
14. Unapokua na lengo la kufanikiwa kifedha anza kwa kutengeneza orodha ya njia ambazo utaweza kuzitumia ili kupata matokeo. Jinsi unavyokua na machaguo mengi ndivyo utakavyoweza kufanya maamuzi mazuri zaidi. Kwa Mfano:
· Unaweza kufikia lengo kwa kuanzisha biashara mpya
· Unaweza kununua biashara ambayo ipo inaendelea
· Unaweza kua bora sana kwa kile unachokifanya na kua unalipwa ghali zaidi, na kwa uangalifu ukawa unawekeza na kuweka akiba pesa zako kwa kipindi cha muda mrefu
· Unaweza ukawa unawekeza kwenye mali zisizohamishika (real estate) kama nyumba na ardhi/viwanja, inaweza kua ni kwa kununua nyumba na kuzifanyia ukarabati na maboresho halafu unaziuza kwa bei ya juu zaidi n.k
15. Matumaini sio Mkakati (Hope Is Not a Strategy). Fanya uchunguzi kabla ya kuwekeza muda wako, fedha au hisia zako kwenye kazi, biashara au mahusiano. Usiishie tu kua na matumaini kwamba kila kitu kipo sawa au kitakua sawa. Pata ushauri kwa wale ambao tayari wameshaipita ile njia unayotaka kuipitia na wamefanikiwa. Jifunze kutoka kwa wataalamu, tafuta wale ambao wameshafikia pale unapotaka kwenda uliza wamefikaje hapo. Jifunze na weka mkakati wa kujiboresha zaidi.
16. Uwezo wako wa kufikiri ndio mali yenye thamani zaidi. Thamani ipo katika Uwezo wako wa kufikiri kua wewe ni nani na unataka nini hasa. Zaidi ya asilimia 80 ya mafanikio yako yatakua ni matokeo ya uwezo wako wa kufikiri vizuri na kwa usahihi. Uwezo wako wa kuweka malengo yanayoeleweka, yanayopimika ambayo una shauku kubwa kuyafikia, yenye kuendana na uwezo na vipaji ulivyo navyo, itakua ni hatua kubwa ya kwanza ya wewe kufikia kwenye mustakabli na mafanikio ya maisha marefu. Tunachotakiwa kujifunza ni kutengeneza huo uwezo wa kufikiri, kuweka malengo na kuweza kuyasimamia
17. Fanyika/kuwa mshauri wako mwenyewe (Become Your Own Consultant)
Hebu jaribu kufikiri wewe ni mshauri na umeitwa kuja kumshauri wewe mwenyewe (to advise yourself) kwenye jambo fulani ambalo ni la muhimu wewe kulifanya ili uweze kufikia mustakabali wako. Ukiwa kama mshauri wako mwenyewe, jilazimishe kuwa tulivu, kuwa mpole na uwe na mtazamo chanya katika kupokea ushauri unaojipatia. Jenga tabia hii ya kujishauri mara kwa mara, kabla hujafanya maamuzi yenye athari aidha chanya au hasi kwenye maisha yako kaa chini jipatie ushauri. Hebu piga picha kwamba wewe ndio unamshauri mtu mwingine kwenye hilo jambo, ungetoa ushauri gani, fanya hivyo kwa uhalisia na bila upendeleao wowote. Halafu jitahidi sasa kuupokea ushauri huo hata kama ni mchungu tekeleza. Don’t fall in love with your ideas, especially your initial ideas. Always be open to the possibility that there is a better way to achieve the same goal.
18. Omba/Uliza kile unachotaka. Katika biashara, maisha yako binafsi au kazini, kumbuka vigezo na sheria/taratibu viliwekwa na mtu fulani na vinaweza kubadilishwa na mtu fulani. Hii inaweza kua mshahara, mazingira ya ajira, vigezo vya mkataba wa kazi, gharama za bidhaa au huduma, gharama za kukodisha sehemu ya biashara, vigezo na masharti ya mikopo n.k hivi vyote viliwekwa na watu. Kama haufurahii kitu hapo usiwe mgumu kuuliza/kuomba. Kitu cha tofauti na kilichopangwa. Usiogope jibu la hapana. Kumbuka kabla ya kuomba/kuuliza kitu jibu hua ni hapana. Na kama hata baada ya kuomba jibu limekua hapana, basi ulichopoteza hapo ni hizo sekunde chache tu ulizo tumia kuomba. Ila kama jibu litakua ndiyo, hii inaweza kubadili maisha yako. The Bible says, “You have not because you ask not.” Never be afraid to ask.
SOMA; Kauli Mbili Za Kuacha Kutumia Leo, Maana Zinaashiria Kushindwa.
19. Mali yako isiyoshikika (Your Intangible Assets). Uwezo wako wa kutengeneza kipato (earning ability) ndiyo mali yako hadimu isiyoshikika. Ni vigumu kuikadiria au kuipima. Watu wawili wanaweza kua na akili sawa na wakawa wamepata matokeo sawa wakati wakiwa shuleni, tena inawezekana wamesoma chuo kimoja, na kozi moja, na kuanza kazi pamoja. Miaka kumi baadaye unakuta mmoja wapo amepandishwa cheo mara kadha na anapata kipato mara 5 au 10 zaidi ya mwenzake. Kwanini hii inatokea? Kwa ufupi ni kwamba hawa watu wanatofautiana katika uwezo wao wa kutengeneza kipato (earning ability. Uwezo huo unaweza kuwa unaongezeka thamani au unashuka thamani. Unapoweka juhudi za kudumu katika kujifunza, kuendelea kuongeza maarifa na ujuzi ili kuongeza thamani popote pale unapokua, uwezo wako wa kuingiza kipato unaongeza thamani yake. Kwa maneno mengine ni kwamba lazima kipato chako lazima kiongezeke.
20. Tengeneza mpango mbadala (Plan B). Endapo mpango wako wa kwanza utashindwa kufanya kazi, kusonga kwako mbele kwa haraka kutategemea mpango mbadala au Plan B. Kamwe usidhanie (assume) kila kitu kitaenda sawia kama kilivyo kwenye mpango wa kwanza. Kama upo bado shuleni, kama Plan A ni kuajiriwa, basi weka na Plan B, ili ukifika mtaani, ajira ikishindikana uwe una chakufanya yaani hiyo Plan B. Changamoto ni kwamba hata hiyo Paln A wengi hawana, ndiyo maana Plan B nayo inakua ngumu. Unakutana na mtu kamaliza chuo mwaka umeisha hana ajira, ukimuuliza unafanya nini sasa, anasema anasubiria bado serikali haijatoa nafasi za ajira, au mwingine anaporomosha malalamiko lukuki kwa serikali ilivyoshindwa kutoa ajira kwake na wenzake. Ukiona mtu wa namna hiyo ujue kakosa Plan B. Always develop a “Plan B” in case your first plan doesn’t work out. Never assume that everything will turn out the way you expect
Asanteni sana
Tukutane wiki ijayo
Makala hii imeandikwa na Ndugu Daudi Mwakalinga mwandishi, mhamasishaji na mshauri katika masuala ya kilimo. Unaweza kuwasiliana naye kwa simu 0763 071007 au barua pepe daudimwakalinga@yahoo.com au dd.mwakalinga@gmail.com

Mambo Ya Kuzingatia Na Njia Bora Za Uwekezaji Wa Majengo Kwa Gharama Nafuu.

Nina kila sababu ya kumshukuru mungu kwa afya njema niliyonayo ambayo inaniwezesha kumudu kufanya yote ikiwemo kuandika makala hii kwa wasomaji wa JIONGEZE UFAHAMU, Chochote unachokifanya huwa ni msukumo wa ndani kutokana na hamasa kubwa uliyonayo ya kufikia malengo yako, mara nyingi umekuwa ukipata wazo la kujenga aina fulani ya jengo kwa makazi, ofisi au biashara na hujui uanzie wapi, napenda nikukumbushe msomaji wa makala hii kuwa biashara ni ushindani, ili ushinde lazima uwe bora/tofauti dhidi ya wengine, leo nimekuletea njia bora za wewe kuzitumia ili zikusaidie kutimiza ndoto zako kwa ubora zaidi.
Wazo la uwekezaji wa majengo
Kama ilivyo kwenye safari yoyote ile lazima kuwe na mipango na mikakati madhubuti ya kufika mahali husika, haijalishi utatumia usafiri gani lazima iwepo dira itakayokuongoza. Ndivyo ilivyo hata kwenye ujenzi, unataka kujenga nyumba ya kupangisha, hoteli, shule, zahanati, ofisi mbalimbali, mgahawa, makazi ya mifugo, gereji, kiwanda au stoo ya kuhifadhia bidhaa na malighafi mbalimbali lazima upate dira itakayokidhi hitaji husika kabla hujatoa kiasi chochote katika uwekezaji wako. Katika ujenzi ramani huwa ndiyo dira kuu inayowaongoza anayewekeza na mafundi wanaojenga. Kuna faida kubwa sana katika ujenzi wa kutumia ramani pasipo kujali unajenga jengo kubwa au dogo, hii husaidia kupata taswira mapema kabla hujaanza kuwekeza. Usinunue ramani mitaani, tumia wasanifu majengo ili wakushauri kulingana na eneo lako na aina ya uwekezaji unaotaka kuwekeza.
Makadirio ya gharama za ujenzi
Watu wengi wameshindwa kuwekeza kutokana na kipengele hiki na walioanza wamejikuta wakiishia njiani pasipo kutimiza ndoto zao kutokana na kutokuwa na mikakati madhubuti ya kifedha. Uwekezaji wowote hugharimu fedha na muda. Kabla ya kufanya uwekezaji huu tafadhali wasiliana na wakadiriaji majenzi ambao ni wataalamu wa uwekezaji na wachumi majenzi uwape wazo lako na namna unavyotaka uwekezaji wako uwe. Hawa ni watu wa ajabu sana, watakushauri namna gani ya kufanya ili uwekeze kulingana na kipato chako pasipo kubadili wazo lako na kukidhi ndoto zako kwa wakati muafaka kulingana na eneo husika la uwekezaji. Hii itakusaidia kuratibu fedha kabla na wakati wa ujenzi na namna utakavyoendesha mradi huo na hatimaye kupata faida baada ya ujenzi huo kukamilika. Pia Kupitia wakadiriaji majenzi wanaweza kukushauri kutafuta vyanzo vingine vya mapato kukidhi aina ya uwekezaji wako.
SOMA; Vitu Vya Msingi Vya Kuzingatia Ili Uweze Kuwa Mwekezaji Mzuri
Namna ya kuwapata mafundi bora
Watu wengi wamenitafuta pale mambo yao yameshaharibika, hajui aanzie wapi kutatua tatizo hilo, hatimaye hujikuta akiongeza gharama zaidi ya mara tatu vile angepaswa kutokana na uhalisia wa mambo yalivyoharibika kutokana na kuwatumia mafundi wasiokidhi ubora. Kwenye ujenzi ni hatari sana kutumia watu wa hovyohovyo kwa kuwa ujenzi ni gharama na wakati mwingine hugharimu hata uhai wa watu na mali zao kitu ambacho hakikubaliki. Kama kazi yako ni ndogo na ya fedha kidogo tafadhali tafuta mafundi wazuri waliofundishwa na makandarasi katika fani husika, iwe tofali, bomba, umeme, milango, paa, madirisha au rangi na mengineyo. Pia kama ujenzi ni mkubwa tafuta mkandarasi anayekidhi vigezo husika. Endapo utawatumia wasanifu majengo na wakadiriaji majenzi katika hatua za awali watakushauri hayo yote kwa kuwa wanajua nini unachohitaji katika uwekezaji wako. Pia endapo utapewa mafundi na watu unaowaamini ni vizuri ukawasaili kulingana na aina ya ramani uliyonayo kama wataimudu au laa! Usiendeshwe na hisia bali akili iwe timamu katika kufikiri na kuamua kutenda ili usilie na kujuta kutokana na mafundi wasio waaminifu na wasiokidhi viwango.
Kabla ya kujenga zingatia haya
Tatizo ni nini: Hali ya sasa imekuwa mbaya sana kutokana na ujenzi holela unaoendelea hapa nchini na hasa miji mikubwa inayoendelea na kukua kwa kasi. Maeneo mengi hayajapimwa kwa matumizi husika na hata yaliyopimwa hayakidhi viwango husika kwa sasa. Kutokana na ongezeko kubwa la watu mijini hasa kwenye miji mikubwa limesababisha tatizo kubwa la matumizi na migogoro ya ardhi hali iliyosababishwa na watu kununua maeneo yasiyopimwa maarufu kama “skwata”. Serikali ya Tanzania imeshindwa kwenda sambamba na kasi ya maendeleo yaliyopo hali inayosababisha kila mwananchi kufanya vile anavyofikiri. Hapa nazungumzia upangaji mji na miji, ni serikali pekee ndiyo ina mamlaka ya kazi hii ya kupanga miji. Leo kuna idadi kubwa ya watu wanaohitaji ardhi kwa matumizi tofauti tofauti hivyo hujikuta wamenunua mahali panapokinzana na matumizi ya watu wengine. Upangaji miji hutofautisha matumizi ya maeneo ya makazi, biashara, kilimo, mifugo, viwanda, maeneo ya wazi na huduma za jamii (zahanati, shule, masoko, makanisa, misikiti, viwanja vya michezo). Wengi wamefariki na wengine wamelia na wapo watakao fariki kwa presha katika hili, kwa ujumla hili ni tatizo kubwa ambalo mzizi wake ni udhaifu wa serikali na uelewa mdogo wa watu wake.
SOMA; Ili Upate Mafanikio Ya Kudumu, Wekeza Kwenye Ardhi Na Majengo.
Nini cha kufanya: popote unaponunua ardhi jiulize mambo mengi sana, hasa maeneo ya “skwata”, tafakari kuhusu miundombinu iliyopo ili ikuongoze kufanya maamuzi.
Kama unanunua skwata, tumia tape mita na siyo hatua kupima urefu na mapana ya maeneo hayo, dalali anakwambia ni 20 kwa 20 na wewe unamwambia fundi wako kiwanja chako ni 20 kwa 20 miguu haina uhalisia na vipimo vya metriki mtazungumzia jambo moja lakini uhalisia ni tofauti kwa sababu watu hawalingani urefu wa miguu.
Kama unaponunua tayari kuna miundombinu hasa ya barabara, zingatia matumizi ya barabara hizo, kama barabara hiyo ina zaidi ya kilometa 20 na inaunganisha maeneo makuu basi jenga mbali zaidi ya mita 30 kutoka barabara hiyo. Na kama barabara ni chini ya kilometa 5 inaunganisha makazi ya watu unapaswa uache umbali usiopungua mita 3 kutoka barabara hiyo na pande zote za jirani angalau mita 2 ndipo ujenge kuta zako. Pia zunguka eneo hilo zaidi ya mita 500 kutoka eneo lako kutazama kama kuna alama inayokutambulisha kama kuna miundombinu yoyote iliyofukiwa kukatisha eneo hilo. Miundombinu inayofukiwa huwekwa alama kila baada ya mita 100 kuonesha mwelekeo wake (miundombinu ya maji safi na maji taka, mafuta, gesi na nyaya za mawasiliano). Ukifanya hivyo utaepukana na dhana ya kubomolewa kutoka kwa mamlaka husika za miundombinu jambo ambalo ni hatari na linaloumiza uchumi wa watu. Hakuna fidia utakayolipwa katika hayo kwa kuwa umeikuta miundominu hiyo.
Pia waeleze na kuwaelimisha wengine ili wajenge kwa mpangilio kuepusha kukosekana kwa njia kutoka nyumba moja na nyingine na viongozi wa mtaa washirikishwe katika kusimamia ujenzi huu usio rasmi kuhakikisha kila anayetaka kujenga aache njia inayokidhi mahitaji ya wengine. Yapo mengi ya kuzingatia kulingana na eneo husika na namna gani utajenga unachotaka kuwekeza (nyumba ya makazi, biashara, shule, zahanati, ofisi mbalimbali, hoteli, migahawa gereji na stoo za malighafi)
Mwandishi wa makala hii ni mwanataaluma na mshauri wa ujenzi.
Anapatikana kwa: Simu: +255 685 729 888, Email: kimbenickas@yahoo.com

Vitu Vya Msingi Vya Kuzingatia Ili Uweze Kuwa Mwekezaji Mzuri

Baada ya kujua ujasiriamali ni nini na sifa za kuwa Mjasiriamali bora, Leo tutajifunza uwekezaji ni nini na vitu vya kuzingatia ili uweze kuwa mwekezaji mzuri. Watu wamekuwa wakipata mtaji, au fedha lakini wanaogopa kuwekeza kwa sababu hawajui wapi pa kuanzia.
Uwekezaji ni nini?
Uwekezaji ni kitendo cha kutumia rasilimali, labda rasilimali fedha na kuitengeneza, kuijenga au kununua rasilimali nyingine kwa matarajio kwamba hiyo rasilimali utakayokuwa umeijenga au umeinunua itakuingizia fedha au pato baadaye katika namna ambayo itarudisha zile fedha ambazo ulizitumia na kukuletea faida zaidi. Unatakiwa kuijenga rasilimali ili irudishe pato au fedha uliyotumia katika uwekezaji na kupata faida.
Unaweza kuwekeza rasilimali muda wako, rasilimali fedha, na rasilimali nguvu yako na nk.
Vitu Vya Msingi Vya Kuzingatia Ili Uweze Kuwa Mwekezaji Bora au Mzuri
  1. Mtu Mwenye Uwezo Wa Kupata Taarifa;
Hii ni sifa ambayo inamsaidia mwekezaji kupata fursa zaidi katika uwekezaji. Katika uwekezaji taarifa ni fursa kubwa sana, unaweza kupata taarifa kupitia intaneti ukapata taarifa nyingi juu ya uwekezaji au ukasoma vitabu, ukajifunza kupata taarifa kupitia watu waliofanikiwa katika uwekezaji ambao unaufanya au unatarajia kuufanya.
  1. Mtu Mwenye Uwezo wa Kupima Majanga;
Hapa inahusisha faida na hasara ni namna gani au jinsi gani mwekezaji anaweza kuchukua risk au hatari, uwezo wa kupima kabla ya kufanya maamuzi, sasa mwekezaji akiwa ana uwezo wa kupima majanga atakuwa katika nafasi nzuri ya kukabiliana na changamoto na hapo atakuwa amepata sifa za kuwa mwekezaji mzuri.
SOMA; Hivi ndivyo unavyoweza kununua Hisa katika soko la Hisa la Dar es salaam (DSE)
  1. Mtu Mwenye Uwezo wa Kutengeneza Mtandao;
Mwekezaji anatakiwa awe na uwezo wa kujenga mahusiano na watu. Huwezi kufanikiwa bila watu, inahitaji utengeneze mtandao mkubwa wa watu ujenge mahusiano bora ili uweze kupata wateja wazuri baadae kulingana na uwekezaji wako ambao unaufanya au unatarajia kuufanya.
  1. Mtu Mwenye Tabia ya Kujifunza ;
Kama wewe ni mwekezaji halafu huna sifa ya kujifunza kila siku basi wewe ni rahisi kufeli, mfano kuna uwekezaji wa hisa ,uwekezaji wa hisa unahitaji kujifunza kila siku jinsi thamani ya fedha inavyobadilika kila siku. Hivyo mwekezaji anatakiwa kupata taarifa kila siku ambazo zitamsaidia kukabiliana na changamoto au jinsi ya kuboresha uwekezaji wako.
Kwa hiyo, Kila binadamu ni mwekezaji, uwekezaji katika biashara unawekeza rasilimali fedha, ambayo itakuletea faida zaidi. Usisubiri mpaka upate rasilimali fedha ndio uanze kuwekeza Anza kuwekeza SASA katika uwekezaji wa akili, wekeza katika ubongo wako kwani chakula cha ubongo ni maarifa.
Huna mtaji, anza kuwekeza katika rasilimali muda wako, akili yako, rasilimali nguvu yako nk. soma vitabu mbalimbali, sikiliza vitabu vilivyosomwa, hudhuria semina, jifunze kwa waliofanikiwa.
‘’ Maarifa ni kila kitu katika uwekezaji na ubongo wako ni injini ya mafanikio’’
Makala hii imeandikwa na Deogratius Kessy ambaye ni mwandishi, mhamasishaji na mjasiriamali, unaweza kuwasiliana naye kupitia namba 0717101505 au kwa barua pepe deokessy.dk@gmail.com au unaweza kutembelea tovuti yake www.actualizeyourdream.blogspot.com

Maisha Ni Safari Na Jinsi Unavyoweza Kufika Salama Safari Hii.

Habari ndugu msomaji wa makala za JIONGEZE UFAHAMU. Ni matumaini yangu u mzima. ni mwisho wa wiki sasa, kumbuka kufanya tathmini ya mambo uliyoyafanya wiki nzima, pitia malengo yako ya wiki hii kama yote yametimia na ongeza juhudi kukamilisha mipango yako ili uweze kufikia malengo ya mwaka uliyojiwekea. Napenda nikukumbushe kuwa kila siku unayoianza ni siku ya kipekee, haitaweza kurudia tena maishani mwako, ni zawadi nzuri sana ambayo Mungu amekupa. Tumia kila siku vizuri, uwe na furaha na uguse maisha wengine pia.
Maisha ni safari. Sio mara ya kwanza kuusikia usemi huu. Naomba leo nikupe mtazamo mwingine kuhusu usemi huu.
 
Siku za hivi karibuni nilikua nasafiri safari ndefu kiasi. Safari yangu ilikuwa ni ya kutoka Kigoma kuelekea Dodoma lakini nilipanda magari yanayoenda mpaka Dar-es-salaam. Nilivyoingia kwenye gari tu saa kumi na mbili asubuhi baada ya dakika chache nilipitiwa na usingizi. Baada ya muda nilishtuka na nikaona asilimia kubwa ya abiria wakiwa wamesinzia. Baada ya mwendo mrefu sana kama masaa saba nilihisi kuchoka tena nikasinzia.
Nilipoamka kama kawaida kuna baadhi ya abiria walikua wamesinzia, wengine walikua wanasimama na kukaa ili kupunguza uchovu waliokuwa nao. Makondakta wa gari walifanya hivyo pia. Kuna wakati walikua wakirudi kwenye viti vya mwisho wa basi wanalala kidogo halafu baada ya muda wanaenda tena mbele kuongea na dereva.
SOMA; Najua Umeshasikia Hili Mara Nyingi, Sio Vibaya Ukasikia Tena Na Leo.
Safari hii ilikuwa ndefu na ilimchosha kila mmoja aliyekua ndani ya basi. Hata bila kuuliza unagundua kuwa kila mtu amechoka. Abiria wengi walikua wamekunja sura zao wakijigeuza upande huu na upande ule, hayo yote yaliashiria uchovu waliokuwa nao.
Lakini cha ajabu, wakati wote huo dereva alikua halali wala hapumziki. Nilifikiria kwa muda jinsi ambavyo dereva alivumilia. Dereva katika akili yake alikua akifikiria furaha ya kutufikisha salama kule tulikokua tunaelekea. Sisi tulipokua tunalala bado yeye hakuwaza kuhusu usingizi na kuona kama sisi tunafaidi. Kama ingekuwa hivyo angetuamsha wote ili anapokuwa akiendesha gari na sisi tusilale kama yeye ambavyo halali. Lakini basi achana na sisi abiria, hata makondakta wa gari hilo nao walikua wakipumzika. Lakini dereva hakujali kwakua alikua akifahamu lengo lake lilikua ni kuendesha gari na kutufikisha kule tunakokwenda salama. Akikutana na vikwazo ajue jinsi ya kuvikwepa bila kushauriwa na mtu yeyote pembeni, lengo kuu ni kutufikisha salama kule tuendako.
Yaani kwa kifupi dereva yeye aliangalia lengo ambalo ni kusafirisha abiria na kuwafikisha salama kule wanakoenda .
Tunajifunza nini?
Ni vizuri kuwa dereva wa gari linaloitwa maisha yako. Ukiona unasinzia, unataka upumzike, unaangalia kama wengine wamepumzika, unawalazimisha wengine wakusaidie kuendesha gari lako ambalo ni maisha yako, unategemea maoni ya wengine ili ulifikishe gari lako salama ujue kuwa upo kwenye hatari ya kusababisha ajali ya maisha yako. Kama ambavyo kuna kanuni na sheria za barabarani ndivyo ambavyo kuna kanuni mbalimbali katika maisha ya kila siku.
Dereva alikua akiongea na kondakta na mara nyingine abiria , lakini pia trafiki aliokuwa akionana nao njiani. Lakini nia yake, lengo lake lilikua ni kufika alikokua amepanga kwenda ambako alikuwa anakufahamu. Hakuna aliyeweza kumtoa nje ya kusudio lake. Pale alipokutana na vikwazo alivuka vikwazo hivyo yeye mwenyewe bila kutegemea msaada wa mtu yeyote Yule. Gari lilipoharibika, fundi alilirekebisha lakini bado yeye alibaki kuwa dereva.
SOMA; Uadilifu, Kioungo Muhimu Cha Kufikia Mafanikio.
Ni vyema kuwa imara na wenye malengo yasiyoyumbishwa kama dereva huyu. Katika safari hii ya maisha utahitaji mawazo, msaada kutoka kwa wengine, utakutana na vikwazo na mambo mengine mengi njiani. Lakini haya yote yasikutoe nje ya malengo yako uliyonayo. Hakikisha wewe ndiye unayeshikilia usukani wa maisha yako kuanzia mwanzo hadi mwisho wa safari yako ili uweze kufurahia pale unapokuwa umefikia malengo yako na sio malengo ya wengine.
Kama una swali, maoni au ushauri usisite kuwasiliana nami.
MWANDISHI: ESTHER NGULWA
MAWASILIANO: 0767 900 110 / 0714 900 110
Whatsaap: 0652 025244
Face book: ESTHER ESTHER
estherngulwa87@gmail.com

Jinsi Ya Kujua Kama Unachofanya Ni Sahihi Katika Maisha Yako.


Kila mtu anapokuja hapa ulimwenguni anakuwa amebeba maagizo maalum ambayo anatakiwa ayatekeleze kwa ajili ya kufanya ulimwengu kuwa sehemu bora ya kuishi. Njia nzuri ya kuweza kujua kile unachofanya kama ni sahihi ni kwa kuyafahamu maagizo uliyobeba ambayo hakuna mwingine zaidi yake anaweza kuyatekeleza. Na maagizo hayo unaweza kuyafahamu kwa kuanza kujitathimini kwa njia ya maswali kama je umeshatambua maagizo uliyoyabeba? Au je una kipaji, uwezo, shauku gani ambayo ni ya kipekee kwako na hakuna mtu mwingine wa aina yoyote anayo isipokuwa wewe tu? Au ya mwisho ambayo ni nzuri zaidi ni kwa kuangalia kile unachokifanya na kujiuliza je unachokifanya ndicho ulichokusudiwa au sababu ya wewe kuwepo hapa ulimwenguni?
Hapa ninakuletea viashiria ambavyo vitakusaidia kujitathmini kama kwanza upo katika kada au eneo sahihi lakini la muhimu zaidi ni lile unalofanya katika hilo eneo ndilo lile unalopaswa au sababu ya wewe kuwepo hapa ulimwenguni.
1. Unakuwa unapenda kile unachokifanya kwa kuwa kinakuvutia , kinakupa shauku na mvuto wa kipekee kukifanya
2. Unakuwa unataka kuwa bora sana katika kile unachokifanya. Na miongoni mwa asilimia kumi ya watu walio bora katika eneo au kada yako unataka na wewe uwepo
3. Unawapenda wale wote ambao wako katika eneo au kada uliyopo na pia unapenda kufikia mafanikio ambayo wao pia wameyafikia
4. Unapenda kujifunza kuhusiana na hilo eneo au kada yako kwa kusoma mambo yanayohusu kada yako, kuhudhuria semina au mihadhara ambayo inazungumzia mambo yanayohusu eneo au kada yako, kusikiliza program za sauti zilizorekodiwa kuhusiana na kada yako. Na zaidi hata iweje unakuwa huchoki kujifunza katika hilo eneo lako.
5. Kada au eneo sahihi kwako ni lile ambalo kwako ni rahisi kujifunza na pia ni rahisi kuweka katika matendo yale uliyojifunza. Ila kwa wengine inaonekana ni vigumu na kwako inakuwa kawaida sana kufanya.

SOMA; Haijalishi Umeshindwa Mara Ngapi…

6. Kutokana na kufurahia kile unachofanya unakuta muda unakuwa kama umesimama kwako na inaweza ikawa imekukolea sana hadi unasahau kula, kunywa hata kwenda mapumziko
7. Mafanikio unayoyapata katika eneo ndiyo inayokupa hamasa ya kipekee na furaha adimu. Na pia unakuwa huwezi kuacha kusubiri au kukaa muda mrefu bila kufanya kitu kikusogeze hatua moja mbele upate mafanikio mengine
8. Unapenda kufikiri kuhusu hilo eneo au kada yako na pia wakati haufanyi kitu unapenda kuzungumza kuhusu eneo au kada yako. Maisha yako yote yanakuwa yamezungukwa na mambo yanayohusu eneo au kada yako
9. Unapenda kuwa na mahusiano na kuwa karibu na watu zaidi ambao wapo katika eneo lako.
10. Na mwisho ni kuwa unapenda kufanya hayo unayofanya kwa maisha yako yote, hutaki kustaafu kuyafanya kwa kuwa unafurahia jinsi unavyoyafanya
Kwa kuweza kutambua eneo au kada yako sahihi ambayo unatakiwa uwe itakusaidia kupata mafanikio na hii itakusaidia kuelekeza moyo wako kufanya vizuri na vizuri zaidi.
Mwandishi: Goodluck Moshi
Mawasiliano:
Whatsapp: +255 753 201 994, Telegram: +255 658 201 994, Barua pepe: eng.gmoshi@gmail.com Facebook: Goodluck Moshi
Pia unaweza kutembelea blog yake www.stadizamafanikio.blogspot.com kujifunza zaidi.

Kuna Watu Hawa Ambao Hawawezi Kukuelewa, Wajue Na Waepuke Ili Uweze Kufikia Mafanikio.

Ni kawaida kuona watu wakikushangaa kwa kuwa unafanya hicho unachokifanya maana wanakuwa hawakuelewi. Hawaoni kwa nini unafanya hicho kitu, wanakosa sababu ya msingi ya kuwafanya wakuelewe kwa wewe kushikilia hicho kitu. Wakati mwingine hata wewe unaweza kuwa unawashangaa kwa nini hawakuelewi, hivyo unakuta wote wawili hamuelewani kwa kuwa hamuoni kitu kilekile sawasawa.
Unaweza kukutana na mtu anakuuliza kwa nini unafanya hiyo kazi wakati wanaoweza kufanya au wanaoonekana kuifanya ni wa aina fulani tu au wana sifa fulani na wewe hauna sifa hizo? Hivyo wanashindwa kukuelewa kabisa na hata ukijitahidi kuwaeleza hauwezi kueleweka kwao, maana wamechagua kuona hivyo, japo wapo baadhi wanaweza kukuelewa kwa kadri unavyozidi endelea. Kuna mtu mwingine anajua na amekariri kuwa shughuli fulani hufaa kufanywa na watu wa aina fulani tu kwa kuwa ndivyo alivyoambiwa na kuaminishwa hivyo. Na yeye akakubali kuamini hayo, hadhani kama anaweza kukutana na mtu anayeweza kumfanya aone alichoaminishwa siyo kweli, pia na yeye hayuko tayari kupokea taarifa iliyo kinyume na hiyo, hataki kubadili namna anavyotazama jambo hilo, kaamua hivyo ni ngumu kumbadili mtazamo huo maana yeye ndiye mwenye uamuzi wa kuamua kubadili anavyotazama mambo.
SOMA;  Tatizo La Kuweka Kinyongo...
Kuna mwingine anaweza akaamua kukuangalia kwa jinsi alivyokuona jana au anaweza akaamua kushikilia jana yako na hata akionana na wewe leo anakataa kukuona wewe wa leo, yeye kamshikilia yule yule. Akili yake na ufahamu wake vimebaki kwenye jana yako na historia yako, hivyo hata akiona unafanya kitu kingine tofauti na kile alikuona ukifanya anaona kuwa hauwezi, hawi tayari hata kukupa nafasi ya kufanya hicho kitu bali yeye anatoa uamuzi na hukumu kwa kuangalia jana yako. Kuna mwingine labda anajua mambo yako mabaya tu hivyo leo akiona unafanya mazuri na akaona watu wakikubali kile unafanya bado yeye atahakikisha anawaambia watu vile ulivyokua jana ili waweze badili wanavyokuona leo, na akikutana na watu ambao hawajielewi ni rahisi kuwabadili lakini akikutana na mtu mwenye kuelewa kuwa jana yako haiwezi kuwa leo, atampuuza tu na kuendelea kukuona anavyokuona leo. Na mara nyingi watu wengi wamekuwa wakivutwa chini na watu walioamua kuwaona kama walivyokuwa jana, walioshindwa kukubali na mtu wanayemuona leo, na wanajitahidi hata kuwashawishi watu wengi waamini wakuhukumu leo kwa ile jana yako. Kwa dunia yetu wengi ni wepesi wa kuamini vile ulivyokuwa jana kuliko ulivyo leo, mtu anaweza kukubali aliyoambia kuhusu jana yako leo, kuliko wewe anayekuona leo, anaamua na kuchagua kukuona hivyo, inachukua muda watu hawa kuja kukuelewa.
Kitu cha msingi katika maisha haya ni vyema kuishi vile ulivyo leo, usiishi ili kuwafanya watu fulani wakukubali au kukuelewa, ishi wewe ulivyo leo hata kama wapo wengi wanaokuona kivingine au walioshikilia jana yako, usiwaangalie hao, bali wewe endelea kuishi maisha yako, kufanya yale unayafanya kwa usahihi ili mradi haumkosei muumba wako na wala hauvunji sheria za nchi, maana ni ngumu kubadili watu wanavyokuona na kukutafsiri lakini ikiwa unaishi uhalisia wako, hauigizi , watakuelewa tu hata kama ni baada ya muda mrefu.
Imeandika na Beatrice Mwaijengo
Mobile number: +255755350772

Ili Upate Mafanikio Ya Kudumu, Wekeza Kwenye Ardhi Na Majengo.

Daima namshukuru mungu kwa namna ambavyo amekuwa akinipa pumzi pasipo malipo, Baraka hizi ndizo zinazonisukuma niweze kuwatazama wengine kama sehemu yangu ya maisha hapa duniani. Ndugu Mtanzania mwenzangu ambaye umekuwa ukitumia muda mwingi kufikiri namna gani utatoka hapo ulipo na kuweza kufikia ndoto zako, usikate tamaa endelea kusonga mbele kwa kuwa unajua unakoenenda, ni furaha isiyo kifani ikiwa unasafiri na unajua unakokwenda na unatambua lengo la safari hiyo ni nini. Leo naungana na wale wote ambao lengo lao ni uwekezaji katika ardhi na majengo. Napenda kukushirikisha ili upate njia rahisi ya wewe kufikia malengo kwa njia ya ardhi au majengo kwa kuwa nimekuwa katika sekta hii kwa muda na nimewasaidia wengi katika hili.
Kwa nini uwekeze kwenye ardhi na majengo
Katika Tanzania hali ya sasa ni rahisi kwa uwekezaji huu lakini inazidi kuwa ngumu katika siku zijazo kutokana na maendeleo ya kiuchumi na kisiasa, ndiyo; uwekezaji wowote ule hutegemea hali ya uchumi ikiambatana na sheria, sera na taratibu za wakati huo. Idadi ya watu inaongezeka kwa kasi sana tofauti na miaka iliyopita, hivyo ongezeko hilo huenda sambamba na mahitaji ya kibinadamu kama vile makazi na huduma mbalimbali za kijamii, mahitaji hayo hufanyika kwenye ardhi na majengo, hivyo hali ya sasa inahitaji sana ardhi na majengo kwa matumizi mbalimbali nchini kote iwe mijini au vijijini, hali hii ya uhitaji husababisha gharama ya ardhi kupanda kwa haraka sana kwa kuwa bidhaa hiyo ni adimu na ina ukomo (ardhi haiongezeki wala haizalishwi).
SOMA; Njia Kumu(10) Za Kupata Utajiri Na Mafanikio.
Inasikitisha kuona mtanzania anayetaka kujikwamua kiuchumi anakuwa mpangaji kwenye nyumba ya kuishi na hata kwenye ofisi za biashara zake. Wengi Hujikuta wakiyumba pale gharama hizo zinapobadilika mara kwa mara kutoka kwa wamiliki kutokana na uhitaji mkubwa wa makazi na ofisi za biashara. Pia wengi huyumba kibiashara kutokana na kuhamahama kwa ofisi jambo ambalo huwa usumbufu kwa wateja. Amua kumiliki ardhi, amua sasa kujenga ili umiliki ofisi za biashara zako au makazi na kuwapangisha wengine.
 
Fursa zilizopo kwenye ardhi na majengo
Udalali wa nyumba na viwanja
Haijalishi upo wapi na upo katika hali gani ya uchumi kazi hii unaweza kuifanya, uwe mjini au kijijini pia unaweza fanya endapo utaamua kutenda kwa uadilifu. Unaweza kuwa dalali wa viwanja, mashamba na nyumba kwa kununua au kupangishwa, hapa dalali unajipatia fedha kwa kazi ya kuwaunganisha mteja na mwenye mali, kazi kubwa hapa ya dalali ni kuitangaza bidhaa hiyo kwa makubaliano ya mwenye mali na mteja kulingana na hitaji husika. Fungua ofisi yako na uisajili kwa mamlaka husika ili upate fursa kubwa zaidi na hata ufanye kazi na makampuni ya ndani na nje ya nchi yanayohitaji huduma hii. Usifanye kazi hii kwa ubabaishaji bali kwa weledi na ndipo utakapoona mafanikio yako.
Ununuaji na uuzaji wa viwanja na majengo
Katika njia hii unaweza kununua ardhi au nyumba kwa bei rahisi baada ya kufanya marekebisho kadhaa unaweza kuiuza kwa gharama ya juu zaidi tofauti na ulivyonunua. Kwa wale waliopo vijijini wanaweza kununua mashamba/mapori na kuyaongezea thamani/kuyasajili kulingana na eneo husika baada ya miezi au miaka kadhaa unaweza kuuza kwa thamani kubwa zaidi tofauti na ulivyo nunua na huu ndiyo uwekezaji unaolipa zaidi. Watu wengi wamenufaika sana kwa uwekezaji huu na hata wameweza kufanya makubwa zaidi ya walivyotarajia.
SOMA; Hivi ndivyo unavyoweza kununua Hisa katika soko la Hisa la Dar es salaam (DSE)
Kuongeza thamani za viwanja na majengo
Kwa bahati ni watanzania wachache sana wanaoifahamu njia hii ya uwekezaji, miongoni mwa watanzania wachache niliokutana nao walijilaumu sana kuwa wamechelelewa kupata wazo hili na eti wamechelewesha mafanikio yao. Napenda nikueleze msomaji wa makala hii kuwa hujachelewa na wala hujawahi, amua sasa kuwekeza. Katika njia hii unaweza kununua shamba ukaliwekea miundombinu ya kilimo cha aina fulani ya kuboresha shamba hilo baadae ukalikodisha kwa wahitaji wa aina hiyo ya miundombinu uliyoiweka, pia unaweza kununua kiwanja ukaweka miundombinu ya uwekezaji wa aina fulani ili kuvutia wawekezaji wengine katika ardhi hiyo, pia unaweza nunua nyumba kwa bei rahisi ukaiboresha au ukaibadili matumizi kulingana na hali ya uhitaji wa mahali husika. Katika njia hii ya uwekezaji ukishaongeza thamani ya mali yako unaweza kuikodisha au kuiuza kwa wahitaji au wawekezaji wengine. Kwa njia hii watu wengi wameingia ubia na makampuni makubwa hasa taasisi za fedha kwa kuwakodisha na kuwauzia maeneo na majengo yao na hali wao wakiendelea kunufaika ilihali wametulia au wanafanya mengine huku kipato kinaingia kutokana na kodi hizo.
Umiliki wa rasilimali ardhi na ofisi za biashara
Mwisho kabisa, hatimaye utakuwa ni mmiliki wa ardhi ndani ya nchi yako mwenyewe itakayokupa fursa nyingi ya kufanya maendeleo ya kiuchumi na kijamii. Inasikitisha Mtanzania unaishi kama mkimbizi ndani ya nchi yako kwa kuhamahama mahali pasipo na ulazima. Wewe unapanga mambo yako namna utakavyoijenga biashara yako hapo ulipopanga ofisi wakati huohuo pia mmiliki wako anawaza namna gani atakuondoa ili aweke ofisi zake au ampe mwingine mwenye uwezo wa kumlipa zaidi yako. Ondokana na haya masahibu kwa kumiliki makazi na ofisi zako mwenyewe. Kumiliki inawezekana amua sasa ili upange maendeleo yako kwa uhakika na ufasaha zaidi.
Mtaji utapata wapi?
Napenda nikupe habari njema msomaji wa makala hii, tumia akiba yako kutimiza ndoto zako pia taasisi na mashirika mengi hapa nchini yanahitaji watu wenye malengo haya ili iwawezeshe katika kutimiza ndoto zao, pia taasisi nyingi za kifedha na mashirika mengi hapa nchini yameanza kushindana kutafuta watu wenye malengo kama haya ili iwawezeshe katika uwekezaji huu. Pia hata mashirika mengi hapa nchini yameanza kuwasaidia wananchi kwa kujenga na kuwauzia nyumba wafanyakazi wake na hata wadau wengine wanao hitaji. Uwekezaji huu huchochea ukuaji uchumi wa nchi kwa haraka sana tofauti na uwekezaji mwingine. Unachofanya wewe ni kuandika nia na lengo la aina ya uwekezaji unaotaka kufanya na namna gani utakavyonufaika katika uwekezaji huo na taasisi hiyo namna ambavyo utakavyorudisha fedha hizo (business plan). Ni rahisi sana, wengi wametumia njia hizi za kuomba fedha kwa mashirika na taasisi za kifedha kwa masharti nafuu na kuweza kufanya makubwa tofauti na walivyofikiri.
Nakusihi msomaji wa JIONGEZE UFAHAMU, Wekeza kwenye ardhi na majengo upate mafanikio ya kudumu ukuze uchumi wa wako na uchumi wa nchi.
Mwandishi wa makala hii ni mwanataaluma na mshauri wa ujenzi.
Anapatikana kwa: Simu: +255 685 729 888, Email: kimbenickas@yahoo.com

Mambo 20 Niliyojifunza Kwenye Kitabu Kinaitwa SELF-IMPROVEMENT 101.

Habari rafiki, ni matumaini yangu waendelea vizuri. Wiki hii tunaendelea na utaratibu wetu wa kushirikishana mambo 20 nilijifunza kwenye kitabu. Leo tunajifunza kutoka kwenye kitabu kinaitwa SELF-IMPROVEMENT 101. Kitabu kimeandikwa na mwandishi aliyebobea kwenye maswala ya uongozi, mwandishi anayeheshimika katika eneo lake la kutengeneza viongozi, sio mwingine mwandishi huyo ni John Maxwell.
Kitabu hiki kinahusu jinsi ya kujiboresha wewe binafsi, ukitaka biashara yako ikue lazima ukue wewe kwanza maana Biashara haiwezi kukua kukuzidi wewe mmiliki. Lakini pia mwandishi anasema kwamba unapojiboresha na vinavyokuzunguka ghafla vinakua bora. Na wengi hawatambui hili, wanahangaika kujaribu kuboresha wengine au biashara zao mwishowe wanashindwa. Sasa njia rahisi ya kufikia mafanikio ni kujiboresha wewe, na njia nzuri ni kuchagua kua mwanafunzi wa kudumu.
Usikome kujifunza, soma vitabu, majarida, hudhuria semina na tafuta mtu (mentor) aliyefanikiwa katika eneo unalotaka kujiboresha jifunze kwake. Heshimu mentor wako na pia fanyia kazi anachokuelekeza, usionyeshe kwamba una uwezo wakati unahitaji kujifunza. Mwishoni anasema gharama ya kutojiboresha ni kubwa sana kuliko ya kujiboresha. Lipa gharama sasa hivi, maana gharama ya baadaye ni kubwa sana.
Kwa ufupi kitabu hiki ni kizuri sana. Hupaswi kukosa mambo ya wiki hii.
Karibu tujifunze mambo mengine.
1. Ukuaji lazima uwe wa kukusudia, kama unataka kukua lazima ukusudie. Tunaweza kutamani maisha yetu yawe bora lakini tukaishia kutamani, tukifikiri ukuaji unatokea tu kama ajali. Kuna tofauti ya kutamani (wish) na kukusudia (intention). Kukusudia kunaambatana na utendaji. Growth must be intentional— nobody improves by accident.
2. Kila mtu anafikiria kuibadilisha dunia, na hakuna anayefikri kujibadilishe yeye mwenyewe kwanza. Watu wengi wanapambana na mabadiliko (fight against change) hasa kama yanawagusa kibinafsi. Unapaswa kutambua kwamba mabadiliko hayaepukiki, lakini pia kwa upande mwingine mabadiliko ni uchaguzi. Unaweza kuchagua kukua au kupambana na ukuaji. But know this: people unwilling to grow will never reach their potential.
3. Tofauti ya Waliofanikiwa na wasiofanikiwa haipo katika uwezo wao na watu wengi hawatambui hilo. Watu hawa Wanatofautiana kwenye shauku (desire) ya kufikia uwezo wao. Maana shauku hii ndiyo inayowasukuma kujifunza ili kukua kufikia uwezo wao. And nothing is more effective when it comes to reaching potential than commitment to personal growth.
4. Watu wengi hua tunasherehekea pindi tunapopata diploma au digrii (shahada) zetu na tunajisemea “Asante Mungu imepita hiyo” Ngoja sasa nipate kazi, maana nimemaliza kusoma/kujifunza. Lakini Fikra za mtindo huu hazitakupeleka mbali zaidi ya kuishia kua mtu wa wastani tu. Unapomaliza shule yako sio mwisho wa kujifunza, ndio kwanza kunakua kumekucha. Maana ukienda mtaani unagundua kumbe kuna vitu vingi sana ambavyo hukuweza kujifunza pindi ulipokua shuleni. If you want to be successful, you have to keep growing. The happiest people I know are growing every day.
5. Chagua maisha ya ukuaji (Choose a life of growth). Njia pekee ya kuboresha maisha yako ni kujiboresha wewe mwenyewe. Kama unataka kukuza shirika au kampuni lazima ukue kama kiongozi. Kama unataka kua na watoto bora lazima uwe baba bora kwanza. Kama unataka kupata mke/mume bora lazima wewe binafsi uwe bora kwanza. Hakuna njia ya uhakika ya kuwafanya watu wanaokuzunguka kua bora. Watu wengi wanasumbuka kweli kuboresha watu wanao wazunguka lakini wanashindwa. Kitu pekee ambacho kweli unao uwezo wa kukiboresha ni wewe mwenyewe. Na maajabu ni kwamba ukifanya kitu hicho (kujiboresha) kila kitu kinachokuzunguka ghafla kinakua bora. So the bottom line is that if you want to take the success journey, you must live a life of growth. And the only way you will grow is if you choose to grow.
6. Anza kukua leo. Sio kile utakachofanya, bali ni kile unachofanya sasa hivi ndio kinachojalisha. Usisubiri kuanza Kukua kesho, anza leo. Watu wengi ambao hawajafanikiwa wana ugonjwa unaoitwa “siku moja” nitafanya hiki au kile, wakati wangeweza kuanza mara moja kufanya vitu vyenye kuleta thamani kwenye maisha yao, lakini hawafanyi na kuishia kusema ipo siku nitafanya. The best way to ensure success is to start growing today. No matter where you may be starting from, don’t be discouraged; everyone who got where he is started where he was.
7. Ukuaji hautokei moja kwa moja (Growth is not automatic). Unaweza kua mdogo mara moja tu, lakini unaweza kua mchanga (Immature) kwa muda usiojulikana, hii ina maana ukuaji hauji automatic. Sio kwa vile umri unakwenda basi ufikiri ndio unakua, sio hivyo. Unaweza kua na miaka 50 lakini bado ukawa mchanga. Ukuaji unahitaji kuweka juhudi za dhati. The sooner you start, the closer to reaching your potential you’ll be.
8. Ukuaji wako wa leo ndio utakaofanya kesho yako iwe bora. Kila unachofanya leo kinajijenga kwenye kile ulichofanya jana, na vyote (vya jana na leo) ndivyo vitakavyoamua kesho yako itakua vipi. Growth today is an investment for tomorrow.
9. Ukuaji wako ni wajibu wako. Ulipokua mdogo wazazi wako walikua na wajibu kwako, hata elimu na ukuaji wako ilikua ni wajibu wao. Lakini sasa umeshakua mtu mzima, wewe ndio unabeba wajibu mzima wa maisha yako. Usipofanya ukuaji wako kua wajibu wako, basi ujue kamwe haitatokea.
10. Kamwe usiridhike au kubweteka na mafanikio uliyoyapata. Adui mkubwa wa mafanikio yako ya kesho ni mafanikio yako ya leo. Maana unapojiona umefanikiwa leo na kubweteka, unakua unahujumu mwenyewe mafanikio yako ya kesho. Kule kufikiri kwamba “umefika” unapofanikisha lengo kuna madhara sawa na kuamini kwamba unajua yote. Hii inaondoa hamasa au shauku ya kujifunza zaidi. Huu ni ugonjwa na watu wengi wanaumwa na huu ugonjwa. Lakini watu waliofanikiwa hawapumziki na kusema sasa nimefika, wanatambua kwamba kushinda kama ulivyo kushindwa ni jambo la muda kidogo (temporary), kwa hiyo wanafahamu fika wanapaswa kuendelea kukua zaidi na zaidi ili kuendelea kua na mafanikio. Don’t settle into a comfort zone, and don’t let success go to your head. Enjoy your success briefly, and then move on to greater growth.
11. Unapaswa kuwa mwanafunzi wa kudumu. Kama tulivyoona kwamba adui mkubwa wa mafanikio yako ya kesho ni mafanikio yako ya leo, ili kuweza kuvuka hiki kikwazo lazima uwe mwanafunzi wa kudumu. Ukiwa mwanafunzi wa kudumu hutabweteka na mafanikio uliyoyapata, utagundua kwamba vipo vingi sana vya kujifunza, na hapo ulipo bado sana hujaweza kufikia uwezo wako ulionao. Watu wengi walio fanikiwa wanasonga mbele kwenye mafanikio kwenye muda uleule ambao wengine wanaupoteza. Kumbuka unapopoteza muda, kuna mwingine muda huo anautumia kujiboresha na kusonga mbele, na kamwe hamtaweza kua sawa, lazima awe mbali tu.
12. Tengeneza mpango wa Kukua/kujiboresha (develop a plan for growth). Ufunguo wa kua na maisha ya kujifunza na kujiboresha bila kukoma umejificha kwenye mpango maalumu wa kujifunza. Weka mpango wa kila siku, andika mpango wako mahali, kwenye mpango wako andika vitu ambavyo unataka kujifunza, andika pia na njia utakazotumia kujifunza. Inaweza kua ni kwa kusoma, kuhudhuria semina, kufanya maongezi na wale waliofanikiwa kwenye eneo unalotaka kujifunza n.k Ukimaliza kazi iliyobaki ni kuwa na nidhamu ya kutendea kazi mpango huo. Usiruhusu udhuru. No excuse
13. Kama ulichokifanya jana bado kinaonekana ni kitu kikubwa basi ujue leo umefanya kidogo tu au haujafanya kabisa. Mara nyingi utasikia watu wakisifia uwezo wao au mafanikio yao ya siku za nyuma. Utasikia “ yaani mimi nilikua kichwa balaa, nilikua naongoza darasani” au “yaani enzi zangu ungenikuta kwenye ubora wangu nilikua ni shiiida” Sasa ngoja ni kwambie kitu Ukiona unajisifia kuhusu jana ujue leo hujafanya kitu.
14. Kwa kujiboresha wewe dunia nayo inakua bora. Usiogope unapokua kwa taratibu, cha kuogopa ni kusimama tu sehemu moja, au kudumaa. Sahau makosa uliyofanya lakini usisahau yale uliyojifunza kutoka kwenye hayo makosa. Jinsi gani unaweza kua bora kesho? Ni kwa kua bora leo. Anza kujiboresha leo
15. Wakati mzuri wa kupanda mti ulikua ni miaka ishirini iliyopita, ila wakati mwingine mzuri na sahihi wa kupanda mti ni leo. Yamkini unatamani ungeanza mapema , au pengine unatamani ungepataga mwalimu mzuri au mshauri mzuri miaka kadhaa iliyopita. Hakuna hata moja hapo lenye kuleta maana. Kuangalia nyuma na kuanza kulalamika hakutakusaidia wewe kusonga mbele. Muda ulionao sasa ndio una uwezo wa kuutumia kubadilisha maisha yako.
16. Adui mkubwa wa kujifunza ni kufahamu/kujua. Lengo la kujifunza ni kutenda na sio kufahamu/kujua, kwani ukishajua na kukaa nacho tu kina faida gani? Wengi wanaingia kwenye mtego wa KUJUA, pengine una digrii yako au masters yako, unafarijika kwamba unajua vitu vingi hivyo unaona huna cha kujifunza tena. Unaishia kusema kwa maneno mimi ni graduate au mimi nina master.. so what? Tunachotaka kuona ni utendaji na sio maneno yako. Unapojifunza zaidi ndipo unagundua kumbe hujui vingi na utaendelea kuwa na hamasa ya kujifunza. Huwa napenda kujifunza kutoka kwa tajiri Warren Buffet, japo ana umri zaidi ya miaka 84, na ni tajiri wa 3 wa ulimwengu, lakini haachi kujifunza kwa kubweteka kwa mafanikio aliyonayo, sasa wewe ni nani wakati hata kwenye kitongoji chako tu kwenye orodha ya watu matajiri haupo.
17. Kama unachokifanya hakina mchango kwako au kwa wengine basi hebu kaa chini uhoji uthamani wa hicho unachokifanya, na uhalali wa wewe kuendelea kukifanya kama hakina thamani kwako wala kwa wengine.
18. Wafanye marafiki zako kua waalimu wako, tengeneza marafiki ambao wanaokupa changamoto na kuongeza thamani kwako, na wewe pia ujitahidi kuongeza thamani kwao.
19. Kama wewe una kipaji sana, unaweza kua na wakati mgumu kufundishika. Kwanini? Kwa sababu watu wenye vipaji mara kadhaa hudhani kwamba wanajua kila kitu. Na hivyo kufanya vipaji vyao kushindwa kuongezeka/kutanuka zaidi. Kufundishika haina maana sana kuhusu uwezo au uwezo wa akili kama ilivyo kuhusu mtazamo. Kufundishika ni ile shauku au nia ya kusikiliza, kujifunza, na kutendea kazi. Ni kule kua na njaa ya kugundua na kukua. Teachability is the willingness to learn, unlearn, and relearn.
20. Kipaji peke yake hakitoshi kukufanikisha. Unaweza kuwa na kipaji na wala kisikusaidie. Tumeona watu wengi wenye vipaji ambao wameishia kuzika vipaji vyao kwa sababu moja kubwa ambayo ni Kutokufundishika. Wengi wamekua wakidhani ukiwa na kipaji basi mafanikio umepata. Kua na kipaji ni kitu kimoja tena cha kawaida sana, maana kwa taarifa tu ni kwamba kila mtu ana kipaji chake. Kua na kipaji ni kitu kimoja na kuweza kukifikisha kipaji chako hatua ya juu ni kitu kingine. Ujuzi ambao ni wa muhimu sana ambao unapaswa kua nao ni kujifunza jinsi ya KUJIFUNZA (learning how to learn), ukifaulu hapo lazima kipaji chako kitakupeleka hatua za juu.
Asanteni sana tukutane wiki ijayo. Kama utapenda kupata kitabu hiki Nitakupatia bure kabisa, niandikie email kupitia dd.mwakalinga@gmail.com
Makala hii imeandikwa na Ndugu Daudi Mwakalinga mwandishi, mhamasishaji na mshauri katika masuala ya kilimo. Unaweza kuwasiliana nae kwa simu 0763 071007 au email daudimwakalinga@yahoo.com au dd.mwakalinga@gmail.com Tembelea blog yake www.kilimobiasharablog.blogspot.com na ujifunze mengi kuhusu kilimo.

Usimtafute Mtu Mwaminifu Bali Kuwa Mwaminifu Wewe, Wengine Watajifunza Kwako.



Uaminifu ni jambo la muhimu sana na wengi wetu tumekuwa wepesi wa kuona wengine si waaminifu kwa kuwa wameenda kinyume na tulivyotegemea iwe. Mfano ni rahisi sasa kusikia wengi wetu tukilalamikia viongozi wanaokosa uaminifu kwa kufanya vitendo visivyofaa au hata kuingia mikataba isiyo na manufaa kwa wengi , ni kweli ni habari mbaya, haifurahishi na inaumiza sana tu katika hali ya kawaida.  Lakini tunasahau kuwa hata katika maisha yetu ya kawaida watu wengi wamekosa uaminifu sana, mfano mashuleni na hata vyuoni unakuta watu wengi wanafaulu mitihani yao lakini si kwa njia sahihi, si kwa kufanya kama ipasavyo kufanya ili wafaulu bali njia na mbinu zinazotumika si njema na si sahihi sana machoni pa watu na hata jamii kwa ujumla, lakini kwa kuwa wengi wanafanya hayo na wanaona yakiwafanikisha wanaona ni kitu sahihi tu.
Au tuna waalimu ambao hawasahihishi mitihani kwa haki bali wanapewa kitu fulani kidogo ili waweze pindisha matokeo ya mitihani na kwa kuwa labda mtu huyo amekuwa akifanya hivyo kwa muda mrefu anaona ni kitu sahihi au kwa kuwa haijulikani na wengi basi anaona yu sahihi tu.  Lakini kuna wanafunzi wenyewe ndio wanaowafuata walimu na kuomba wapewe majibu au namna ya kuweza kufaulu mitihani yao kwa urahisi kwa kuwapa kitu kidogo, na kwa kuwa pengine mtu anakuwa amefanya yeye kama yeye anajua yu salama na sahihi wala hasikii kuhukumiwa ndani mwake na ikitokea amesikia hivyo anapuuzia tu.
Maofisini wafanyakazi wengi wamekuwa si waaminifu pia, hasa kwenye swala la muda, wengi wanatumia muda wa kazi kufanya mambo ambayo hayana tija kwa waajiri wao, muda ambao mwajiri anawalipa wao wanafanya mambo ambayo hayamwingizii mwajiri faida, wengine wanachelewa sana kufika ofisini, au wanawahi kutoka kabla ya muda na kwa kuwa labda hakuna mtu anayemfuatilia basi anajiona yuko sahihi kufanya hivi, lakini kuna wengine akisikia tu bosi hayupo siku hiyo basi atachelewa kufika ofisini au atachelewa sana au anaweza wahi kutoka kwa kuwa hakuna mtu wa kumfuatilia au kumuulizwa kwa nini anafanya hivyo. Wengine pia wamekuwa wadanganya waajiri wao kwa kuwapa taarifa zisizo sahihi, mfano mtu ameagizwa akanunue kitu fulani dukani akifika huko ataongeza bei na hata kutengeneze risiti bandia ili tu aweze kuchukua kipato zaidi na kwa kuwa hana mtu wa kuweza kuligundua hilo basi anaona yu salama, wengi wananunua hata vitu visivyo na ubora ilimradi tu aweze kupata kitu  kidogo na kufikisha taarifa za uongo kwa mwajiri wake.
Imefikia hatua hadi majumbani mwetu uaminifu umekosekana yaani watu wamezoea tabia mbaya mpaka imeonekana ni sahihi, mfano unakuta hata mama pale nyumbani yupo tayari kumdanganya mumewe juu ya matumizi fulani ili mradi tu aweze kutimiza malengo yake , au mwingine anafikia hatua ya hata kuwatesa watu wa nyumbani mwake kwa kuwapa vitu vilivyo chini ya kiwango ili mradi tu aweze kufanya yake, watu wengi wamekosa uaminifu kabisa.
Kitu cha kushangaza watu niliowataja hapo juu ni watu wa kwanza kulaumu viongozi na serikali kwa ujumla kuwa imekosa uaminifu, wanasahau kwamba nao ni sehemu ya serikali, wanasahau kwamba nao popote pale walipo wana wajibu wa kuwa mawakili wa uaminifu, wanatakiwa kuwa waaminifu popote pale walipo haijalishi ni eneo gani, pale utakapokuwa mwaminifu kuna mwingine atajifunza kitu kwako, wapo utakaowafanya wajione kuwa nao wana wajibu katika hilo, watagundua kuwa hao watu waaminifu wanatengenezwa kuanzia huku majumbani mwetu, jiulize kama wewe si mwaminifu je wanao watakuwaje? Jiulize ni mbegu gani unapanda kwa jamii inayokuzunguka?  Unaweza kuamua kuanzia leo, kutimiza majukumu yako kwa uaminifu hata kama hakuna mtu anayekuomba ripoti, ni kwa faida yako ndugu, amua leo kuwahi kazini, ukifika fanya kazi kwa uaminifu, achana na mipango isiyo ya kiaminifu maana inakufanya uishi kwa wasiwasi na siyo salama kwa afya yako pia, ukiacha mbali hasara nyingine nyingi tu.
Anza wewe kuwa mwaminifu na wengine watajifunza kwako.

Imeandikwa na Beatrice Mwaijengo
Mobile number: +255 755 350 772
Email: bberrums@gmail.com