Jinsi Ya Kuondokana Na Hofu Ya Kupata Ajali.
Habari za leo msomaji wa JIONGEZE UFAHAMU. Ni imani yangu kuwa ulikua na wiki nzuri. Ni mwisho wa wiki ambapo
tunakutana tena ili kujiongezea maarifa ya maisha.
Leo tutaangalia suala la ajali za vyombo vya usafiri.
Katika miezi ya karibuni kumekuwa na ajali za mara kwa mara
za vyombo vya usafiri hasa mabasi. Maisha ya watu wengi yamepotea na watu
wamepata ulemavu pia, ikiwa ni pamoja na kuumia kwa baadhi ya wasafiri. Watu
hawa inawezekana ni ndugu zetu wa karibu, marafiki na hata majirani zetu.
Niwape pole wale ambao kwa namna moja au nyingine waliguswa na matukio haya.
Lakini pole kwa Watanzania wote kwakua tumepoteza nguvu kazi kwa taifa letu.
Inawezekana hata wewe msomaji ni mmojawapo wa watu ambao
wamewahi kupata ajali katika chombo chochote kile cha usafiri, naomba upokee
pole yangu pia. Kupata ajali husababisha hofu kwa mhusika na hivyo kumfanya
kila mara akitaka kusafiri akose raha. Wakati mwingine ukiwa safarini unakuwa
na wasiwasi wa hali ya juu mpaka unapomaliza safari, kutokana na hofu uliyonayo
kichwa kinakuuma kupita kiasi.
Unaweza kuondokana na hofu ya kupata ajali kwa kufanya haya
yafuatayo
1.
HAKIKISHA UNATUMIA USAFIRI IMARA
Ni vizuri kutumia usafiri ambao hata
wewe mwenyewe unakuwa na amani moyoni kuutumia. Kama utakosa amani kwa mwonekano
wa gari tu basi ujue kama ukipanda hata likikwepa jiwe tu lazima roho yako
itaruka na kukukosesha amani. Sasa kama unasafiri safari ndefu mpaka unafika
hofu inakuwa imeongezeka maradufu.
Kwa utaratibu wetu watanzania hata
kama wewe ni mgeni mahali fulani na unahitaji usafiri watu hufahamu sifa za
magari. Unaweza kuwauliza watu unaowaamini katika eneo hilo gari lipi ni imara
na lipi ni bovu lakini. Kuwa makini usiwaulize wapiga debe kwakua watakudanganya.
2.
USISHABIKIE MWENDO KASI
Madereva wengi sana hupenda kuendesha
magari kwa mwendo wa kasi sana. Mara nyingi abiria huwa mashabiki na kuwafanya
madereva kuendesha magari kwa vurugu sana. Usijaribu kushabikia mwendo wa kasi
kwani ni rahisi kupata ajali kama mwendo wa gari sio mzuri lakini pia madhara
ya gari linalopata ajali kwa kua na mwendo wa kasi ni makubwa kuliko gari
ambalo liko katika mwendo wa kawaida.
3.
USIWAZE MAWAZO HASI
Jitahidi kuwaza mawazo chanya kila
wakati. Usifikirie kupata ajali kila mara unaposafiri. Mara nyingi unaloliwaza
ndilo linalotokea. Waswahili wana usemi wao kuwa ”aliwazalo mjinga ndilo
limtokealo” Jitahidi usiwaze mawazo hasi katika akili yako. Fikiria ni mara
ngapi umekuwa na wasiwasi wa kupata ajali na hakuna lililotokea zaidi ya wewe kufika
salama. Kuwaza mawazo hasi hakuwezi leta unafuu wowote au kusitisha lile lililopangwa
kutokea. Kama umekuwa na wasiwasi kutokana na mwendo kasi basi toa taarifa
mahali panapohusika. Na jambo zuri ni kwamba katika vyombo vya usafiri wameweka
namba za mawasiliano kama kutakuwa na tatizo lolote katika chombo cha usafiri
ulichopo.
4.
MUNGU ANAJAMBO ANATAKA UJIFUNZE
KATIKA KILA LITOKEALO.
Kuna baadhi ya vitu vingi vinatokea katika maisha
yetu hata kama tutachukua tahadhari kiasi gani moja ya vitu hivyo ni ajali.
Katika kila litokealo basi usijilaumu na usijute. Kuna kitu Mungu anataka
kukufundisha kwakua kama kuna kitu Mungu amepanga kitokee huwezi kuzuia.
Unaweza kupoteza baadhi ya viungo au kupoteza ndugu wa karibu. Inasikitisha
sana na ni inaleta uchungu mno. Kuwa na hofu, kuwa na majonzi wakati wote na
kushindwa kuendelea na maisha mengine hakusaidii zaidi ya kukupa uchungu zaidi.
Ni vizuri kukubali hali iliyotokea na
kuendelea tena na maisha ya kila siku.
5.
KUFA NI LAZIMA
Inawezekana kauli hii ya KUFA NI LAZIMA imekushitua kidogo.
Lakini ukweli ni kwamba kama tulizaliwa basi lazima siku moja tutakufa. Kila
mmoja ana namna yake ambayo Mungu amempangia kifo chake lakini pia yeye
anafahamu ni siku gani ya mwisho sisi kuwepo hapa duniani. Tunatofautiana nyakati
za kuaga dunia na namna ambavyo tunaiga dunia hii. Hivyo kwa kufahamu hili basi
ni vyema kujiandaa wakati wote, lakini kuendelea kutimiza majukumu yetu ili
siku ikifika tuwe tumekamilisha yale tuliyopaswa kuyafanya hapa duniani.
Ni imani yangu kuwa haya uliyoyasoma
yatasaidia kuondoa hofu ya kupata ajali ambayo inakuzonga. Au hata
kumshirikisha mtu mwingine mwenye hofu ya namna hii ili umsaidie kuwa makini
lakini awe na amani pindi anapokuwa akisafiri.
Kama una swali, maoni au ushauri
usisite kuwasiliana nami.
MWANDISHI: ESTHER NGULWA
MAWASILIANO: 0767 900 110 / 0714 900 110
6/12/2015 07:31:00 AM
|
Labels:
MBINU ZA MAISHA
|
This entry was posted on 6/12/2015 07:31:00 AM
and is filed under
MBINU ZA MAISHA
.
You can follow any responses to this entry through
the RSS 2.0 feed.
You can leave a response,
or trackback from your own site.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 comments:
Post a Comment