Hiki Ni Kitu Muhimu Unachotakiwa Kuwa Nacho Ili Usishtukizwe Na Maisha.


Iwe ni kwenye biashara  au ni kazini kwako, umejiajiri au umeajiriwa na kwa sasa unaona kila kitu kinaenda sawa, ni muhimu kufikiria kuwa kuna siku mambo yanaweza yasiwe sawa kama yalivyo leo. Kuna siku hiyo ofisi inaweza ikaungua, hiyo biashara inaweza kuungua moto au hata kuibiwa na majambazi. Au pengine yule mtu unayemtegemea sana kuendesha hizo shughuli anaweza asiwepo tena au asiwe na uwezo wa kuendelea kutoa msaada au huduma anayokupatia sasa. Mtu mwingine anaweza asinielewe kwa nini nasema haya sasa maana anaona kila kitu kipo sawa na kila jambo linaenda kama anavyopenda liende na hataki hata kufikiria kwamba kuna siku inaweza kuwa kinyume. Mwingine anaweza asitake kufikiria au hata akawa anaogopa kuwaza vitu ambavyo pengine vyaweza kumuumiza au kumgharimu zaidi kwa sasa. Yaani kwa ufupi haoni umuhimu wa kuwa na mpango mbadala kwa kuwa sasa mpango huu unafanya kazi sawasawa.
Ndugu yangu hebu fikiria hata pale inatokea mtu ameondokewa na mtu aliyempenda au niseme aliyekuwa anamtegemea sana wengi hulia au kuumia na kukata tamaa. Ukifuatilia wengi hawalii kwa kuwa wanaumizwa sana na kifo cha mpendwa wao, wengi hulia kwa kuwa sasa wanawaza itakuwaje? Maisha yataendaje bila yule mtu? Maana walimtegemea yule kwa asilimia zote mia moja, hawakuwahi fikiri kinyume na kujipanga endapo itatokea hivyo. Ukiangalia mtu anapofariki wengi hulia sana na kuumia sana kwa kuwa wanaona ndoto zao zimekomea pale, maana waliweka matumaini kwa mtu yule, au mwingine ni biashara imeungua moto au ameibiwa , kila kitu huishia hapo maana hakuwahi kuwa na mipango endelevu ikiwa hali kama hiyo itatokea. Hakuwahi kuwaza hayo au pengine hakuwahi kukutana na mtu wa kumpa changamoto kama hizo, hakuwahi kuwa katika mazingira ya kumfanya awaze hivyo. Maana kuna watu wengine ukimwambia kuhusu haya mambo atakuambia kwa nini unawaza mabaya, ni kweli inaweza isikifurahishe kuwaza hivyo lakini kuogopa kwako kuwaza hivi haizuii hayo mambo kutokea, hivyo ni lazima uweke hofu pembeni na kufikiria nini kifanyike endapo yatakukuta hayo. 
Hebu jiulize hiyo biashara yako au ni hiyo nyumba  je,  umeikatia bima? Ndugu yangu unaweza ukaamua kukata bima kwa ajili ya hiyo biashara yako ili hata ilikotokea lolote basi usichanganyikiwe, usiwe mtu ambaye hujui uanzeje, usikimbilie kuangalia gharama ya hiyo bima au kusikiliza wanaokuambia kuwa unaweza kulipia na usikutwe na hayo matatizo na ukawa umepoteza pesa yako lakini ukikutwa je itakuwaje? Chukua hatua leo.   Ni ofisini kwako unatumia mifumo ya kompyuta kutunza taarifa nyingi kwa ajili ya shughuli zako za kila siku, hakikisha unatunza taarifa zako nje ya hapo ofisini kama mbadala ikitokea umevamiwa au jengo limeungua moto. Kama ni ofisi kubwa inabidi uwe hata na ofisi nyingine mahali pengine yenye kila kitengo maalumu ili shughuli nyingine ziendelee kama kawaida hata kama utapatwa na maafa makubwa.    Hakikisha unakuwa na utamaduni wa kutunza taarifa zako sehemu nyingine ambapo utaweza kuzipata kama hizi unazotumia sasa zitapotea au kuharibika.
Usiishi kwa kuweka matumaini kwa mtu mmoja tu, hata kama ni mtu unayeona ana uelewa mkubwa sana , hakikisha kama unaona ana uelewa wa vitu vingi basi hakikisha unahamisha uelewa alio nao kwa watu wengine pia ili hata asipokuwepo basi usiathirike na kutokuwepo kwake, ndio unamuamini sana lakini tambua huyo ni binadamu tu anaweza kuanguka tu na asiamke tena, utafanyaje?  Chukua hatua sahihi.  Wengine wameweka matumaini yao yote kwa wazazi au ndugu fulani wanaoona wana uwezo wa kuwasaidia katika maeneo fulani, ndugu yangu, imewafanya hata kubweteka kwenye shughuli zao kwa kuwa wanaamini wapo watu wa kuwatimizia mahitaji yao, ni wanadamu tu hao kesho anaweza asiwepo utaishije? Amka, jifunze kusimama na kufanya mambo yako mwenyewe leo ili hata siku hawapo usiyumbe uweze kuendelea, maana tambua kuwa haijalishi utakutana na nini maisha huwa ni lazima yaendelee, yataendeleaje kama haujajipanga sawasawa?   Unao uwezo wa kusimama mwenyewe , unao uwezo wa kufanya hiyo shughuli, komaa acha kujishusha na kusubiri wengine wakufanyie. Kama unadhani ni lazima umtegee mtu basi ni vyema kama utaweka tumaini lako kwa Muumba wako maana yeye hafi, yupo milele huyo hatakuangusha kamwe.
Makala imeandikwa na Beatrice Mwaijengo.
Mobile phone: +255755350772

1 comments:

anduliler@yahoo.com said...

Nimabarikiwa sana na makala hii, ni makala ambayo imejaa hekima nyingi na ushauri ambao mara nyingi kizazi chetu kinastahili kuuchukua na khutumia. Kuweka bima ya biashara, nyumba na vitu vingine mara nyingi tumezembea lakini pamoja na uzembe huo haijazuia madhara kutupata, tunahitaji kufanya mabadiliko. Mabadiliko yetu yalenge kwenye kubadilisha mitizamo na mazoea, maana si kwamba hatupendi kufanya hivyo la hasha bali mazoea na mitizamo ya kale imetuvuta kubaki katika maisha ya kale ambayo hayaendani na uhalisia wa sasa, imekuwa rahisi kwetu kukata bima za magari kwa sababu ya kuogopa kukamatwa na polisi , tuvaa mikanda kwenye magari siyo kwa uelewa wa usalama endapo ajali itatokea bali wengi hufanya kaa kuogopa polisi. Mitizamo ya kufanya jambo kaa sababu kuna mtu anafuatilia inastahili kuachawa bali tujifunze na kuzifanyisha mazoezi tashi zetu kufanya jambo kwa manufaa yake na siyo kwa sababu ya mtu fulani, vivyo hivyo tunatakiwa kujifunza kuweka bima za nyumba, elimu, afya nk. Tunatakiwa kufanya si kwa sababu tuambiwa tufanye la hasha bali tunastahili kufanya kwa sababu ni jambo jema na linastahkli kufanywa bila shuruti ya mtu yeyote. Nakushukuru dada Beatrice Mwaijengo tunaomba uendelee kutuelimisha zaidi na zaidi bila kuchoka kwa sababu tunahitaji kutiwa moyo katika mambo mengi ambayo hatukuyazoea katika maisha yetu.