Huu Ndio Mtaji Mkubwa Ambao Tayari Unao.

Labda niane kwa kueleza kuwa hakuna mtu ambae hana mtaji huo. Mtaji wenyewe unautengeneza mwenyewe kuweza kuwa bora kwani tayari unao. Mtaji wenyewe ni watu. Watu wanaweza kukuwezesha au kukuangusha kutegemea na unavyowatumia. Wanasiasa, walimu, wanasheria, wafanyabiashara huhitaji watu ili kuweza kufanikisha malengo yao. Hakuna kiongozi yeyote wa siasa ambaye amewahi kufanikiwa bila kuwa na watu. Hakuna mfanyabiashara aliyefanikiwa bila kuwa na mtaji wa watu. Ili uweze kufanikiwa ni lazima uweze kuwa na watu wa kufanya nao kazi, kukutia moyo, kukufariji na hata wa kukupa changamoto zitakazokuimarisha.

SOMA; Kila Suluhisho Linatengeneza Tatizo, Chagua Ni Tatizo Gani Unataka.

Ukihitaji mafanikio utahitaji watu ambao utafanya nao kazi, utahitaji watu wa kununua bidhaa zako, utahitaji watu wa kukukopesha, utahitaji watu wa kukufanyia kazi, utahitaji watu wa kukushauri na kwa vyovyote vile huwezi kufanikiwa bila kuwa na watu. Hayati Nelson Mandela aliwahi kusema kwamba ‘’ukitaka kutembea haraka tembea mwenyewe, lakini ukitaka kutembea umbali mrefu basi tembea na watu’’. Jaribu kuutumia msemo huu katika maisha yako ya kawaida na utaona uhalisia wake. Jaribu kujijengea watu wa kukuinua na sio wa kukuangusha. Jaribu kujijengea mtandao bora ambao utakufaa. Ukijenga mtandao mbovu utakuangusha sawa na kujenga nyumba yenye msingi mbovu, Itaanguka siku moja. Je kuna ulazima wa kuwa na watu wengi? Jibu linaweza kuwa ndiyo au hapana. Kuwa na watu wengi wenye lengo la kukuangusha au kukurudisha nyuma si mali kitu. Ni bora kuwa na watu wawili watakaokusaidia. Laini pia kama kuna ulazima wa kuwa na watu wengi jifunze namna ya kuwapata kwa kujifunza kupata na kukaa na watu.

SOMA; Mipango Sio Muhimu Kama Kitu Hiki.

Kwa kuhitimisha nitumie fursa hii kukuambia kuwa na watu halafu usishirikiane nao utaukuwa hujafanya chochote. Jifunze kushirikiana na watu. Usimdharau yeyote bali muheshimu kila mtu kwa nafasi yake kwani hujui atakuja kukufaa lini. Nakushauri pia uondoe watu wanaokuletea mawazo hasi na kukuaminisha kuwa huwezi. Hao watakufanya usifikie malengo yako. Usipende kukaa na watu ambao wataupoteza muda wako kwa vitu visivyokujenga. Bali tumia kila sekunde moja ya masha yako kukujenga na tumia watu waliofanikiwa kuweza kujifunza kutoka kwao.

Nakutakia heri ya pasaka na mapumziko mema ya siku ya kumbukumbu ya Karume. Tukutane wiki ijayo siku ya leo kwa makala nyingine ya kukujenga.

Makala hii imeandikwa na Nickson Yohanes ambae ni mjasirimali na mhamasishaji. Unaweza kuwasiliana na nae kwa kwa: simu: 0712 843030/0753 843030 e-mail: nmyohanes@gmail.com

Pia unaweza kutembelea blog yake: www.lifeadventurestz.blogspot.com kujifunza zaidi.

0 comments: