Tabia Mbaya KUMI(10) Zinazopunguza Ufanisi Wako.

Huenda unatamani kufanya zaidi ya unavyofanya sasa lakini kila ukijitahidi huoni mabadiliko. Huenda una ufanisi mdogo kiasi kwamba kila mtu anakuona wewe ni mvivu sana.

Sio kweli kwamba wewe ni mvivu bali kuna tabia ambazo zinakufanya ushindwe kutekeleza majukumu yako kwa wakati.

Leo utajiongeza na tabia kumi mbaya ambazo zinakufanya uwe na uzalishaji mdogo na ukiweza kuziepuka utaongeza uzalishaji wako.

1. Unzanza siku yako bila ya kuipangilia. Usipopangilia siku yako utafanya nini utajikuta unafanya chochote kinachotokea mbele yako.

2. Unaangalia facebook au email kila baada ya dakika kumi. Kama mawasiliano yako yanakufanya uwe na shauku kubwa ya kutaka kujua ni nini kinaendelea kwenye mitandao ya kijamii itakuwa vigumu sana kwako kukamilisha majukumu yako kwa wakati.

3. Unasubiri muda muafaka ndio ufanye ulichopanga kufanya. Kuna wakati unafikiri kama kitu fulani kikitokea basi nitafanya kitu fulani, mwishowe unaishia kutokufanya kabisa.

4. Unajaribu kufanya mambo mengi kwa wakati mmoja. Mwishowe unaishaia kushindwa kumaliza hata moja, kama mtu anayekimbiza sungura wawili, hakamati hata mmoja.

5. Unagoma kujifunza vitu vipya. Dunia ya sasa karibu kila kazi imerahisishwa sana. Kuna utaalamu mwingi ambao unaweza kuutumia kurahisisha kazi yako, ila unapogoma kujifunza unabaki nyuma.

6. Unasubiri mpaka dakika ya mwisho ndio ufanye jambo. Unapokuwa na muda wa kufanya jambo mara nyingi huwa unaona ni mwingi, ni mpaka muda unapokaribia kuisha unaona kwamba ulipoteza muda mwingi.

7. Unalaumu vifaa unavyofanyia kazi. Labda unasema kompyuta unayotumia ipo taratibu sana, mashine unayotumia inakurudisha nyuma. Hizi zote ni sababu ambazo hazina msingi.

8. Huna muda maalumu wa kula. Kama huna muda maalumu wa kula au wakati mwingine unaacha kula itakuwa vigumu sana kwako kuweza kuwa na nguvu ya kutekeleza majukumu yako.

9. Unatumia muda mwingi sana kupanga. Inawezekana unapanga, halafu unakaa unafikiria mipango yako, baadae unapanga tena. Kwa kupanga huwezi kutimiza chochote, unatakiwa kufanya kazi.

10. Huapati usingizi wa kutosha. Kama kila siku unachelewa kulala na kuamka umechoka ni vigumu sana kuweza kutekeleza majukumu yako.

Epuka tabia hizo kumi mwaka huu 2015 ili uweze kuongeza ufanisi wako.

0 comments: