Njia Kumu(10) Za Kupata Utajiri Na Mafanikio.

Fedha ni muhimu na kila mmoja wetu anakazana kila siku ili kupata fedha za kumtosha kuendesha maisha yake. Na pia tunakazana kupata fedha zaidi ili angalau kuwa na uhakika wa chochote kitakachotokea mbeleni.

Hivyo kujua njia za kupata fedha na hata kuwa tajiri ni muhimu ili usijikute ukihangaika sana na mwishowe kushindwa kupata unachotaka.

Katika kitabu cha RICH HABITS, The daily success habits of wealthy individuals, mwandishi Tom Corley amechambua tabia ambazo ameziona kwa watu matajiri na hata masikini katika utafiti aliofanya.

Zifuatazo ni tabia ambazo watu wenye mafanikio wanazo;

1. Kuweka malengo.

Watu wenye mafanikio wanaongozwa kwa malengo na mipango, watu hawa wana malengo ya muda mfupi na ya muda mrefu na kila siku wanafanyia kazi malengo yao.

2. Kujifunza kila siku.

Watu waliofanikiwa wana tabia ya kujifunza kila siku. Huangalia njia za kuongeza maarifa yao, hujisomea na kuhudhuria semina mbalimbali zinazowafanya kuwa bora zaidi.

3. Kujali afya.

Watu waliofanikiwa wanajali sana afya zao. Wanakula vizuri na kufanya mazoezi mara kwa mara. Pia huepuka vyakula ambavyo sio vizuri kwa afya.

4. Kuweka mbele vitendo.

Watu wenye mafanikio ni watu wa kujali vitendo zaidi kuliko maneno. Ni watu ambao wakishasema wanafanya jambo fulani basi wanalifanya mara moja na sio kuvuta muda mpaka kusahau wanachotaka kufanya.

5. Wana mtizamo chanya muda wote.

Watu wenye mafanikio ni watu ambao wana mtizamo chanya juu yao binafsi na hata kuhusu maisha. Wanaamini wanaweza kufanya kile wanachotaka kufanya na hii huwafanya wafanikiwe zaidi.

6. Kuweka akiba.

Watu wenye mafanikio ni watu ambao huwa wanaweka akiba katika kila kipato wanachopata. Watu hawa huweka akiba kwanza na ndio kufanya matumizi. Wanaweka akiba asilimia 10 mpaka 20 ya kipato chao.

7. Kudhibiti matumizi.

Watu wenye mafanikio huishi chini ya kipato chao. Ni watu ambao hudhibiti matumizi na kuweza kuishi chini ya kipato wanachopata, wakitaka kuongeza matumizi wanaongeza kwanza kipato. Kwa njia hii wanaepuka kuingia kwenye madeni.

8. Kutokupoteza muda.

Watu wenye mafanikio wanaepuka sana kupoteza muda bila ya kufanya jambo la msingi. Watu wengi wenye mafanikio wanaangalia tv sio zaidi ya saa moja kwa siku.

9. Kufanya zaidi ya wanavyotegemewa.

Watu wenye mafanikio hufanya zaidi ya wanavyotegemewa kufanya. Kama wanategemewa kutoa huduma kwa kiwango fulani wao hupitiliza na kuwafanya kuwa wa thamani sana.

10. Kutokata tamaa.

Watu wenye mafanikio wameshindwa mara nyingi sana ila hawakukata tamaa. Wamekuwa na uvumilivu na pia ni vinganganizi mpaka wameweza kufikia mafanikio makubwa.

Je wewe unataka kufikia utajiri na mafanikio? Njia ndio hiyo hapo, kazi ni kwako sasa.

Nakutakia kila la kheri.

0 comments: