Njia KUMI Za Kuboresha Maisha Yako Ya Kibiashara.

Ili kuweza kufanikiwa kwenye biashara na hata kwenye maisha unahitaji kuwa na malengo na mipango, kufanya kazi kwa bidii na maarifa na hata kuwa na mtizamo chanya kwenye kile unachofanya na hata maisha yako kwa ujumla.

Hakuna kitu kinachowarudisha watu nyuma kama kutokuwa na malengo, uvivu na mtazamo hasi.

Pamoja na mambo hayo muhimu kuna njia kumi unazoweza kuzitumia na ukaboresha maisha yako ya kibiashara kwa kiasi kikubwa sana.

1. Kubali changamoto.

Hakuna barabara iliyonyooka, hivyo hivyo biashara yoyote utakayofanya, hata kama ingekuwa rahisi kiasi gani ina changamoto zake. Unapokutana na changamoto, ikubali na kisha anza kuitatua. Ukianza kuikimbia unajijengea matatizo makubwa baadae.

SOMA; Wajasiriamali Wenye Mafanikio Hufanya Mambo Haya Matano Kila Siku.

2. Jitegemee.

Ili uweze kufikia mafanikio kwenye biashara unayofanya, kuna wakati utahitaji kufanya maamuzi magumu na uweze kuyasimamia. Maamuzi hayo yanaweza yasiwe mazuri au yasiwapendeze wengi. Ni lazima uweze kujtegemea na kujisimamia kwenye biashara yako. Kama utaendesha biashara kwa kutegemea wengine wanafanya nini ndio uige, huwezi kufanikiwa.

3. Zione fursa.

Katika kila hali unayokutana nayo kwenye biashara, zione fursa mbalimbali zinapokuzunguka. Unapopata changamoto angalia ni fursa gani unayoweza kuitoa kwenye changamoto hizo. Kuwa na kiu ya kuangalia fursa na utaanza kuziona nyingi sana zinazokuzunguka.

4. Cheka.

Hata kama unafanya biashara inayokuhitaji uwe makini kw akiasi gani, unahitaji muda wa kucheka. Unahitaji muda ambao unawez akufanya utani wa hapa na pale na ukafurahia na kucheka. Kuna faida kubwa sana kwenye kucheka, inakuongezea kujiamini na kinga ya mwili pia.

SOMA; Njia KUMI Za Kubana Matumizi Yako Mwaka Huu 2015.

5. Wasaidie wengine.

Utapata chochote unachotaka kwenye maisha kama utaweza kuwasaidia watu wengi zaidi kupata kile wanachotaka. Ifanye biashara yako kuwa sehemu ambayo watu wanajua matatizo yao yatapata suluhisho na utapata wateja wengi sana.

6. Kuwa na dhumuni la maisha yako.

Mbali na malengo na mipango ya kibiashara na hata maisha, kuwa na dhumuni kubwa la maisha yako. Hiki ni kitu ambacho utakiishi na ndio kitakusukuma wewe kuweka juhudi zaidi ili kuweza kufikia dhumuni hilo.

7. Kuwa tayari kubadilika.

Unachoamini leo, kesho kinaweza kisiwepo kabisa. Biashara inayolipa leo, miaka michache inaweza isiwepo kabisa. Hivyo wakati wowote kuwa tayari kubadilika. Soma alama za nyakati na kuwa tayari kuchukua hatua kabla mambo hayajakwenda hovyo.

8. Zungukwa na watu chanya.

Hakikisha unazungukwa na watu ambao wana mtizamo chanya kama ulivyo wewe. Hawa watakuwezesha wewe kuendelea na mtizamo wako. Ila kama utazungukwa na watu wenye mtizamo hasi, ni vigumu sana kuweza kuendelea na mtizamo wako.

SOMA; Hii Ni Kazi Yenye Malipo Makubwa Sana Ambayo Unaweza Kujifunza Kuifanya

9. Fanya kazi kwa juhudi na maarifa.

Hili ndio hitaji la msingi kabisa, maelezo yanajitosheleza. Kama haupo tayari kufanya kazi kwa bidii na maarifa, achana na biashara, kafanye vitu vingine, na sina wazo ni kitu gani hakihitaji kazi. Kama utakipata tushirikishe.

10. Acha kuwa mwathirika.

Kama unataka kukuza biashara yako unahitaji kuacha kuwa na mawazo ya kiathirika. Pale jambo lolote linapotokea, acha kufikiri kwamba kwa nini limetokea kwako, au kwamba una bahati mbaya. Badala yake chukua hatua ya kubadili mambo. Kama umefanya makosa jifunze na usirudie tena.

Mafanikio kwenye biashara sio kitu rahisi sana ila pale unapojipanga vizuri utaona yanakuja yenyewe bila ya wewe kuteseka sana. Fanya mambo yale ya msingi na jali sana biashara yako na wale wanaokuzunguka. Bila kusahau, jifunze sana, wekeza sana kwenye rasilimali muhimu kwako ambayo ni akili yako.

SOMA; Kurasa 365 Za Mwaka 2015, Fursa Muhimu Kwako Kujifunza.

0 comments: