Showing posts with label NILICHOJIFUNZA LEO. Show all posts
Showing posts with label NILICHOJIFUNZA LEO. Show all posts

Mambo 20 Niliyojifunza Kwenye Kitabu The One Thing.

Habari rafiki, ni matumaini yangu waendelea vizuri. Wiki hii tunaendelea na utaratibu wetu wa kushirikishana mambo 20 nilijifunza kwenye kitabu. Leo tunajifunza kutoka kwenye kitabu kinaitwa The ONE THING- the surprisingly truth behind the extraordinary results. Kitabu kimeandikwa na Gary Keller pamaoja na Jay Papasan.

Kwa ufupi kitabu hiki ni kizuri sana. Hupaswi kukosa mambo ya wiki hii. Karibu tujifunze.

1. Muda hausubiri mtu. Muda hauna cha VIP , maskini au tajiri hauna wa kumuogopa wala wa kumuonea huruma. Kwahiyo tunapaswa kuuthamini sana muda maana ni bidhaa hadimu sana na tumepewa bidhaa hii sawa kwa watu wote. Tofauti zetu zinatokana na jinsi tunavyotumia muda tulionao. Muda haukusubiri ufanikiwe kwanza ndio uzeeke, au hausubiri kwanza ustaafu ndo ukaanze biashara. Hata ukilala na usifanye chochote muda unayoyoma. Time waits for no one.

SOMA; Fanya Mambo haya matatu kuwa na maisha bora na yenye furaha.

2. Unapomuoana mtu ana maarifa mengi ujue imemchukua muda kujifunza kufikia hapo. Ukiona mtu amefanya vitu vingi au amefanikisha vitu vingi ujue kwamba alitumia muda fulani kuvifanikisha, na vilevile Ukiona mtu mwenye fedha nyingi ujue imemchukua muda kuzipata. Suala kubwa hapa ni muda. Kila kitu kinahitaji muda, hakuna kitu cha kulala usiku na kuamka asubuhi umekua tajiri hakuna kitu kama hicho. Mafanikio yeyote yanahitaji muda. Unaowaona wamefanikiwa iliwachukua miaka kadhaa kufika hapo walipo. Walikua na upeo wa mbali wa miaka kuanzia 20 mbele.. wakati wengi wetu hata mwakani hatujui tutakua wapi tunaishi maisha ya pata potea, kutafuta na kula kuoa au kuolewa na kujenga kanyumba kamoja na kagari kwisha kazi.. Halafu tunajiona vidume kweli.. na kukaa na kusema usiwaone wale kina Bill gates ni Freemason wale mali zao ni za kishetani… Tuna sahau kwamba wenzetu walikua na Malengo na mipango ya muda mrefu na kila siku walikua hawapotezi muda kuyafanyia kazi malengo yao. It’s just a matter of time

3. Kampuni nyingi zilizofanikiwa zinakua na bidhaa moja au huduma moja ambayo ndiyo inawafanya wajulikane na kuwatengezea fedha nyingi. Issue sio kua na bidhaa nyingi kama utitiri. Chagua kitu kimoja weka nguvu zako zote hapo lazma utaona mafanikio. Sasa kwetu unataka uuze mchele wewe, spear za pikipiki, duka la vyombo, sijui kibanda cha mpesa unataka. Fanya kitu kimoja kwanza kikishafanikiwa anza kingine. Success is sequential, not simultaneous.

4. Hakuna mtu anayefanikiwa peke yake. Kila mtu aliyefanikiwa katika Nyanja yeyote atakwambia kuna mtu aliyemshawishi, alimhamasisha au alimfunza hadi imepelekea kufika hapo alipo. Hata Albert Einstein mwanasayansi maarufu duniani, alikua akipata uongozi na maelekezo kutoka kwa bwana Max Talmud kwa muda wa miaka sita. Na ndio maana utasikia watu wakisema mentor wangu ni fulani, mentor wangu, mentor wangu.. je na wewe unayo mentor? Tafuta kocha na kaa chini ya kocha. Kumbuka No one is self-made. No one succeeds alone. No one.

5. Waliofanikiwa hawafanyi vitu tofauti la hasha wanafanya kwa utofauti. Wana jicho la umuhimu. Wanatulia na kuamua kipi ni cha muhimu katika maisha yao na ndicho wanachokipa nafasi kiendeshe maisha yao. Wanaofanikiwa Wanafanya kwanza vile vitu ambavyo wengine wanapanga kufanya baadaye, na ubaya ni kwamba hiyo baadaye hua haifiki inabaki tu baadaye. Achievers always work from a clear sense of priority.

SOMA; Kijana Punguza Mambo Haya Ili Uweze Kupata Mtaji Wa Kuanza Biashara -1

6. Orodha ya vitu vya kufanya (To do list) usipokua makini inaweza ikakupleka nje ya kuafanikiwa. Kwanza orodha ya mambo ya kufanya ni vitu vile tunavyodhani tunahitajika kufanya. Jambo la kwanza linalotokea kwenye orodha mara nyingi ni lile lililoanza kukujia kichwani. To do list nyingi ni kwa ajili ya kutufanya tuwepo tu(Survival list) , ni orodha ya kukufanya umalize siku yako na kujiona kwamba umefanya kazi..yani umeweza kufanya yote ulopanga kwenye orodha unajihisi umefanikisha mambo sana. Instead of a to-do list, you need a success list – a list that is purposefully created around extra ordinary results. Success list au orodha ya mafanikio ni ile inayojikita kwenye shughuli zenye matokeo makubwa na shughuli zenyewe ni chache tu. The majority of what you want will come from the minority of what you do. Kwisha habari

7. Kuwa bize au kua na mambo mengi ya kufanya hakumaanishi kufanikiwa. Mara nyingi tunapenda watu watuone kwamba tuko bize, tuna mabo mengi ya kufanya. Je umewahi kujiuliza toka uwe bize umepiga hatua gani ya maana kulingana na ubize wako? Don’t focus on being busy; focus on being productive. Allow what matters most to drive your day.

8. Jifunze kusema Hapana. Sio kila kitu unakubali tu, sio kila wakati unaawambiwa fanya hivi au vile na wewe unakubali tu. Mara nyingi vitu vya namna hiyo vinakujia ili kutimiza ndoto au mafanikio ya wengine. Jifunze kusema hapana, mpaka pale umemaliza kufanya jambo la muhumi kwanza. Mara nyingi hasa wafanyakazi walio ajiriwa wanadhani kukubali kila kitu kinachotoka kwa boss ndo unakua mfanyakazi bora au ndo utaambiwa uko flexible. Flexible wapi … wakati unajimaliza mwenyewe. utajikuta ni mtu wa kufanya vitu vya emergency tu… Usikimbilie kupata sifa za muda tu..ukaja kujutia maisha yako. Jifunze kusema hapana hata kwa boss wako. Mwanzoni ataweza asikuelewe lakin ipo siku utakua mfano, kwamba ni mtu unayejua kuweka vipaumbele mtu unayejua kusimimamia jambo lenye kipaumbele bila kujalisha ni dharura gani imetokea.

9. Kufanya vitu vingi kwa wakati mmoja (Multitasking) ni uongo. Hii imekua dhana kila sehemu, utasikia watu wakijivunia mimi nafanya multitasks. Imefika mahali mpaka kwa waajiri multitasking imekua ni moja ya sifa ya mtu anatakiwa awe nayo ili kuajiriwa. Yaani wakati unaandika ripoti muda huhuo uwe unamhudumia mteja na tena uwe unaongea na simu. Ukifanya hivyo lazima utashindwa kimoja wapo au vyote, au utaishia kuapata matokeo ya kawaida sana. Katika ulimwengu wa leo ambapo unapimwa kwa matokeo (results/impacts) na sio kwa kazi uliyofanya Multitasking inawazika wengi sana. Ili uwe na matokeo makubwa fanya jambo la muhimui kuliko yote weka nguvu na umakini wako hapo. Hakikisha umemaliza alafu nenda kwenye jambo lingine. It’s not that we have too little time to do all the things we need to do, it’s that we feel the need to do too many things in the time we have.

10. Hatupaswi kuogopa mambo makubwa. Kwa kujua au kutokujua wengi wetu tumekua tunaogopa mambo makubwa tukidhani ni mabaya kumbe sio kweli. Mfano mtu anaogopa kuwa na mawazo ya kumiliki ndege, kumiliki makampuni makubwa duniani, akidhani kwamba ni mbaya au atapata madhara mabaya. Utasikia mtu anasema sasa pesa zote hizo nipeleke wapi? Mimi nataka tu za kunitosha sitaki presha mimi. Ukiwa na mawazo hayo ujue wewe ni mbinafsi (selfish) maana unajifikiria wewe tu. Huwazi kupata zaidi ya unachohitaji ili kuwasaidia wengine, mwisho wa upeo wako ni wewe kupata tu. Angalia kina Bill gate fedha walizonazo asilimia kubwa wala hatumii yeye. Anatumia kuwasaidia wengine katika sekta ya afya, kilimo n.k Ana malengo ya kufuta kabisa baadhi magonjwa yaliyoitesa dunia kama polio, malaria, ebola n.k. Ipo miradi mingi sana ya kilimo inayofadhiliwa na Bill Gate, na kiu yake kubwa nikuona wakulima wadogo wakiongeza vipato vyao kaika hali endelevu, mimi mwenyewe nimekua nikisimamia moja ya miradi ya kilimo inayofadhiliwa na Bill Gate. Don’t fear big. Fear mediocrity. Fear waste. Fear the lack of living to your fullest. “People who are crazy enough to think they can change the world are the only ones who do.”

SOMA; Huu Ndio Ukomo Unaojiwekea Wewe Mwenyewe.

11. Usiogope kushindwa maana ni sehemu ya safari yako ya kufanikiwa . Tazama kushindwa kwako kama shule ya kujifunzia alafu songa mbele. Mtu mmoja aliwahi sema hivi “ if you want to double your success, then you have to double your failures”. Akimaanisha kwamba kama unataka kupata mafanikio mara dufu, uwe tayari kushindwa maradufu. Maana katika kushindwa ndio unajua ipi sio njia sahihi na kuanza kutafuta njia sahihi.

12. Ubora wa maisha yako utatokana na maswali unayojiuliza. Unaweza jiuliza kwanini tujikite kwenye maswali wakati kwa kawaida hua tunahangaikia kupata majibu. Ni kweli Wengi tunawaza kupata majibu. Na mimi nakuuliza majibu ya kitu gani? Kama huna mawasli? Ukweli ni kwamba ubora wa majibu unatokana na ubora wa maswali. Hata waliobadilisha maisha yao, au waliobadilisha ulimwengu walianza kwanza kwa kujiuliza maswali makubwa na wakaanza kuyatafutia majibu. Je hapo ulipo ndipo ulipaswa uwepo? Maisha unayoishi ni ya kwako? Je kusudi la wewe kuwepo hapa duniani ni nini? Je unafikiri kama pangekua hakuna kikwazo chochote, na una kila kitu ili kufanya chochote au kupata chochote ungefanya nini? Au Ungetamani kua na maisha gani? Anza kujiuliza maswali hayo na mengine. Ukiona umekerwa ujue somo limeingia na uwezo wa kupata majibu unao. Fanyia kazi uone kama maisha yako yatabaki kama ulivyo. Great questions are the path to great answers.

13. Maisha ndio mwajiri wako mkuu, utakachopatana nae ndicho atakachokupa.. Unapopatana mshahara na mwajiri wako ndicho atakachokupa. Sasa cha ajabu umepatana mshahara na mwajiri baada ya muda unalalama mshahara mdogo. Kwani hukulijua hilo wakati wa mapatano? Bahati nzuri nimewafanyia watu wengi mahojiano ya kazi (job interview), na mara nyingi swali la mshahara linaulizwa mwishoni, na lengo lake kubwa ni kutaka kujua huyu mtu anajitathimini vipi. Yeye mwenyewe anajithaminisha je? Sasa wengi wakiulizwa swali la mshahara anajibu kwamba nitakua tayari au nitaridhika kwa mtakachonipa. Au anataja kiwango cha chini sana. Mimi mwenyewe niliwahi kukosa kazi kwa kutaja mshahara mdogo. Nikidhani ndo nitaonekana ninafaa au nitakua nimeangukia kweny bajeti yao. Duuh kwa masikitiko ndo nikawa nimejimaliza mwenyewe. Sasa wanachojiuliza waajiri ni kwamba kama mtu huyu haoni thamani yake sisi je tutawezaje? Sasa turudi kwenye pointi yetu ya msingi, Maisha ndio mwajiri wako, utakachopatana nae ndicho atakachokupa. Usiyaambie maisha nitakubaliana na chochote utakachonipa. Tambua thamani yako patana na mwajiri wako (maisha) ubora wa vitu unavyotaka.

14. Maisha yenye kusudi (Life with purpose) ndio maisha yenye furaha. Kama hujui kusudi lako hata ufanikiwe vipi huwezi furahia. Live with purpose and you know where you want to go.

15. Kuishi Maisha yenye vipaumbele (Live by priority). Tunaweza kuwa na kusudi la maisha, lakini tukikosa vipaumbele itakua ni pata potea. Kipaumbele au priority ina tafsiri kadhaa kama “kitu cha muhimu zaidi”, “kitu cha msingi”, “kitu cha kwanza”, “kitu cha juu” kitu kikuu” n.k Unaweza kua na tafsiri nyingi lakin zote zitalenga kaitka kitu kimoja kinachopaswa kutangulia ili kurahisisha vingine au hata kufanya hivyo vingne visiwe vya muhimu kivile. Kua na ndoto au malengo makubwa mengi sio kwamba ndo kufanikiwa, la hasha. Wengine wanajiuliza sasa mbona nina vipaumbele vingi, lakin unasahau kwamba katika vipaumbele ulivyonavyo ikichimba ndani zaidi una kimoja ni cha muhimu zaidi. Anza nacho hicho. The purpose without priority is powerless

SOMA; Kama Hutaki Kuwa Na Maadui Fanya Kitu Hiki Kimoja.

16. Kusudi la furaha. Ukweli ni kwamba kila tunachofanya kwenye maisha ni ili tupate furaha. Furaha ndio bidhaa ambayo imekua ukitafutwa na watu wengi sana, lakin ndio bidhaa ambayo wachache sana wanafanikiwa. Tatizo ni kwamba tunafikri furaha ni jambo la kufikia, yaani pale tunapopata kitu fulani,( kama mke, mume, mototo, nyumba, gari au kufaulu) ndo tunatakiwa kufurahi. Ndio maana ukipata kitu kile unafurahia kwa muda kidogo tu halafu unaanza kutafuta kingine ili upate furaha tena. Unapaswa kufurahia kila hatua unayopita kuelekea mafaniko. Kuna mtu aliwahi kusema hakuna njia ya mafanikio, bali mafanikio ndio njia. Kama mafanikio ni njia, basi tunapaswa kuwa na furaha kwenye njia hiyo. Happiness happens on the way to fulfillment.

17. Weka malengo yako kwenye kataratasi na uyaweke karibu na wewe. Watu wengi hatuna utaratibu wakuandika malengo yetu, yaani malengo yanakua kichwani tu, tena malengo mengi yanawekwa kipindi cha mwaka mpya, mwezi January ukiisha ulishasahau ulipanga nini. Swali la kujiuliza ni vitu ngani viko karibu na wewe zaidi? Wengi wetu simu ndo vitu vya karibu, simu ndo kitu cha mwisho kua nacho kabla ya kulala na cha kwanza kukishika kabla ya kuanza siku. Malengo yako ndo yanapaswa kua karibu na wewe kuliko unavyodhani. Kabla ya kulala yasome, kabla ya kuanza shughuli nyingne yasome. Kufanya hivyo kunaweka akili yako kua kwenye mstari sahihi wa kuhakikisha unajikita kwenye vitu vyenye mchango kwenye malengo husika. Pia utavutia watu au mazingira ambayo yanaendana na malengo yako hata yale ulodhani ni magumu utashangaa fursa zinafunguka hatua kwa hatua. Fanya hivyo ujionee mwenyewe

18. Dereva wa maisha yako ni wewe chukua umiliki wa matokeo yako (Take ownership of your outcomes). Wengi wetu tunaishi kama abiria kwenye maisha, halafu tunashangaa tunakoelekea, au tunalaumu kwa yanayotokea. Sasa acha kua abiria wa maisha yako, nenda kwenye kiti cha dereva chukua usukani wa masiha yako. Wajibika kwa matokeo unayopata.

19. Vitu vinavyozuia mafaniko ya mtu mara nyingi sio vile asivyovijua bali ni vile anavyovijua ambavyo sio kweli. Cha ajabu tunafahamu vingi sana. Ila vingi kati ya hivyo ni vya uongo na ndivyo vilivyotufikisha hapa tulipo. Halafu cha ajabu kingine vile vya uongo ndo tumeweka imani yetu huko, na ndivyo vinaamua maisha yetu. Kabla hujangundua usijokijua, anza kugundua unachokijua ambacho sio sahihi.

20. Jitahidi kuzungukwa na watu watakao kunyanyua juu zaidi. Ukweli ni Wengi tunapenda kukaa na watu tunaowazidi ili watuone vichwa kwelikweli. Tunapenda makundi ambayo sisi ndo tunakua wazungumzaji wa kuu tunaomiliki mazungumzo, kila ukisema uantaka watu waseme ndio mzee. Sasa kuna habari sio nzuri kama unatabia kama hiyo. Maana wewe ni wastani wa watu 5 wanaokuzunguka. Kama umezungukwa na vilaza 9 wewe utakua wa 10. Njia pekee ya kutoka hapo ulipo ni kuzungukwa na watu waliofanikiwa kukuzidi wewe ambapo utajifunza mbinu walizotumia kufika waliko. Sio lazima ukamtafute Bill gate au Buffet, vipo vitabu vizuri vinavyoelezea walivyoanza mpaka waliko fika. Zungukwa na vitabu vya watu wakubwa waliofanikiwa. Chimbua maarifa ya watu hao na tendea kazi unachojifunza, uone kama utabaki ulipokua .

Asanteni sana tukutane wiki ijayo. Kama utapenda kupata kitabu hiki cha The ONE THING wasiliana nami. Nitakupatia bure kabisa.

Makala hii imeandikwa na Ndugu Daudi Mwakalinga mwandishi, mhamasishaji na mshauri katika masuala ya kilimo. Unaweza kuwasiliana nae kwa simu 0763 071007 au 0658 587029 au email daudimwakalinga@yahoo.com au dd.mwakalinga@gmail.com

SOMA; Karibu Kwenye Semina Ya Mafanikio Kwenye Biashara Mwaka 2015.

Maswali Matatu Kwa Anayetaka Kuwa Mjasiriamali Kujiuliza Kutoka Kwa Richard Branson.

Richard Branson ni bilionea mwingereza ambae anamiliki makampuni ya VIRGIN. Chini ya virgin kuna makampuni karibu 400 na yote yako chini ya Richard.

branson

Richard Branson ni mmoja wa mabilionea ninaowakubali sana kwa sababu pamoja na utajiri mkubwa alionao bado anapata muda wa kuwafundisha watu wengine kupitia makala zake na vitabu vyake.

Leo nakushirikisha maswali matatu ambayo Richard anasema kila anayetaka kuwa mjasiriamali ni lazima ajiulize ili aweze kuwa na safari yenye mafanikio.

1. Je elimu ya juu ni muhimu kwangu?

Richard anasema ujiulize swali hilo kwa sababu pamoja na kwamba elimu ni muhimu bado haiwezi kuchukua nafasi ya kazi kubwa unayotakiwa kufanya unapoanza ujasiriamali. Hivyo kama unaendelea na elimu ya juu ili kupata ujuzi zaidi ni vizuri ila kama unataka kurudi shule ili kukwepa maamuzi magumu unayotakiwa kufanya kama mjasiriamali unapoteza muda wako.

2. Je napenda kuwa na bosi?

Richard anasema alianza biashara biashara akiwa mdogo sana kwa sababu hakuwahi kufikiria kufanya kazi chini ya mtu. Hivyo kama unaona huwezi kufanya kazi chini ya mtu basi ujasiriamali ndio njia yako.

3. Wanaonizunguka wanafikiriaje?

Richard anasema kama huwezi kuamua, omba ushauri kwa wale wanaokuzunguka. Wanaweza kukupa ushauri mzuri sana wa nini unaweza kufanya.

Angalizo; kwa mazingira yetu kuwa makini sana maana watu wako wa karibu wanaweza kuwa nao ni waoga kwenye ujasiriamali hivyo wakakuogopesha na wewe.

Kwa msaada zaidi tafuta mlezi (mentor) ambaye amewahi kufanya unachotaka kufanya na yeye atakuongoza.

Jiulize na kujibu maswali hayo matatu ili uweze kufikia mafanikio makubwa kwenye ujasiriamali.

Nakutakia kila la kheri.

TUKO PAMOJA.

Hotuba ya Nyerere kuhusu Rushwa.

Katika kumbukumbu ya miaka 15 tokea kufariki kwa rais wa kwanza wa Tanzania, angalia na kusikiliza video hii ya hotuba yake kuhusu rushwa.
https://www.youtube.com/watch?v=92mpI-ablNM&feature=youtube_gdata_player

Watu Watatu(3) Waliofukuzwa Kwenye Kampuni Walizoanzisha Wenyewe.

Unaweza kufikiri kuingia kwenye biashara na kujiajiri mwenyewe ndio njia nzuri ya wewe kuwa na uhuru kwa kile unachofanya. Inaweza isiwe kweli kwa sababu kwa jinsi hali ya biashara za kisasa ilivyo unaweza kujikuta kwenye hali ngumu sana.

Tena pale unapofikia kampuni ikawa kubwa na kuanza kuuza hisa, wenye hisa nyingi wanaweza kufanya maamuzi hata ya kukufukuza wewe japo wewe ndiye uliyeanzisha.

Hapa ni orodha ya watu watatu ambao walifukuzwa kwenye kampuni walizoanzisha wenyewe;

1. Steve Jobs, Apple

Steve Jobs alianzisha kampuni ya apple ila baadae alifukuzwa kwenye kampuni hiyo. Alikuja kurudishwa kwenye kampuni hiyo na kuleta mapinduzi makubwa ya kiteknolojia.

2. Ted Tunner, CNN

Ted Tunner alianzisha CNN, shirika la habari la marekani lakini baadae alikuja kufukuzwa kwenye shirika hilo.

3. Jack Dorsey, Twitter

Jack Dorsey ni mmoja wa waanzilishi wa mtandao wa kijamii unaoitwa twitter ila kwa sasa anaonekana hayupo tena kwenye mtandao huo kwani ameanzisha kampuni nyingine ya teknolojia.

Kuwa makini pale unapoanzisha kampuni yako yasije kukutokea mambo ambayo hukutarajia.

Nakutakia kila la kheri.

PICHA; Nchi Zilizotawaliwa Na Uingereza Na Miaka Zilipopata Uhuru.

UK

NILICHOJIFUNZA LEO; Sababu Za Kihistoria Kwa Nini Scotland Ilitaka Kujitenga Na Uingereza.

Jana tarehe 18/09/2014 wananchi wa Scotland walipiga kura ya kuamua kama Scotland ijitenge na kuwa na mamlaka yake kamili au iendelee kuwa sehemu ya Uingereza(United Kingdoms). Matokeo ya kura hiyo yaliyotangazwa leo asubuhi yanaonesha kwamba asilimia 55.3 wamekataa kujitenga na asilimia 44.7 walipiga kura ya kutaka kujitenga. Kwa matokeo hayo Scotland inaendelea kuwa sehemu ya Uingereza.

 

Nilitaka kujifunza zaidi juu ya muungano huu wa Scotland na England.

Mwaka 1602 malkia Elizabert I wa England alifariki dunia bila ya kuacha uongozi kwa watu wa familia yake. Mfalme James I wa Scotland alikuwa msimamizi wa ncho zote mbili lakini kila nchi ilikuwa na uhuru wake.

Mwaka 1707 viongozi wa Scotland walikubali kuungana moja kwa moja na England kutengeneza United Kingdoms. Baadhi ya wananchi wa Scotland hawakufurahishwa na maamuzi haya ni hivyo yalitokea maandamano mengi kupinga muungano huo. Kwa miaka mingi baadhi ya wananchi wa Scotland wamekuwa wanajaribu kujitoa ila wanashindwa.

Mwaka 1999 Scotland waliweza kuwa na bunge lao. Uingereza waliruhusu Scotland kuweza kufanya maamuzi yao juu ya mambo kama afya, nyumba na elimu, lakini bajeti walipangiwa na Uingereza.

Bado wananchi wengi wa Scotland hawakufurahishwa na hili na hivyo manunguniko ya chini chini yalikuwa yakiendelea. Chama cha upinzani kiliposhika nafasi ya kuongoza bunge la Scotland viongozi wake walipendekeza ipingwe kura ya kuamua kuendelea kuwepo chini ya Uingereza au kujitegemea wenyewe.

Haya yote ndiyo yaliyopelekea kwenye kura iliyofanyika jana. Na kama tulivyoona kwenye matokeo asilimia 44 ya wanaotaka kujitenga sio ndogo na hivyo huenda chokochoko zikaendelea.

Tunaweza kujifunza nini hapa kwenye muungano wetu wa Tanganyika na Zanzibar? Karibu kwa maoni.

NILICHOJIFUNZA LEO; Viongozi Mashuhuri Walioibadili Dunia.

Karibu kwenye kipengele hiki cha mambo niliyojifunza kwa siku husika. Kwa siku zinazokuja nitakuwa nakushirikisha yale ninayojifunza kuhusu uongozi kupitia kitabu WORLD FAMOUS LEADERS WHO RESHAPED THE WORLD.

Hiki ni kitabu kilichoeleza kwa kifupi baadhi ya viongozi ambao walifanya mambo makubwa duniani. Unaweza kujipatia kitabu hiki na ukaendelea kujifunza zaidi. Kava lake naweka kwenye picha hapo chini;

viongozi

Viongozi hawa kuna waliofanya makubwa kwa wema kama Nelson Mandela na wengineo na kuna waliofanya makubwa kwa ubaya kama Adolf Hitler aliyesababisha vifo vya zaidi ya wayahudi milioni sita.

Kuna mengi ya kujifunza kupitia maisha na uongozi wa watu hawa.

Nakukaribisha katika safari hii ya kujifunza.

TUKO PAMOJA.

NILICHOJIFUNZA LEO; Vita Kubwa Kuwahi Kutokea Afrika Ukiacha Vita Vya Pili Vya Dunia.

Ukiacha vita vya pili vya dunia vita kubwa ambayo imewahi kutokea Afrika ni vita ya pili ya Congo(Second Congo War)
Vita hii ilianza August 1998 na kutangazwa kumalizika July 2003 baada ya serikali ya mpito kushika madaraka.
congo war
Pamoja na kutangazwa kumalizika kwa vita hii bado mapigano na choko choko zinaendelea katika majimbo ya Kivu na Ituri.
Ni katika vita hii ambapo raisi wa Congo Laurent Kabila aliuawa na mtoto wake Joseph Kabila kushika madaraka ya kuongoza nchi.
Vita hii ilihusisha mataifa tisa ya Afrika na vikundi zaidi ya 20 vya wapiganaji.

Sababu ya vita hii.

Sababu kubwa iliyochangia vita hii ni mgogoro wa kimaslahi katika uchimbaji na biashara ya madini.

Madhara ya vita hii.

Vita hii ndio vita kubwa zaidi kutokea barani Afrika ukiacha vita vya pili vya dunia. Mpaka kufika mwaka 2008 zaidi ya watu milioni 5.4 walikuwa wamepoteza maisha kutokana na vita hii. Vifo vingi vilitokana na mauaji ya kuvita, huduma mbovu za afya na ukosefu wa chakula.
Kuna mengi sana ya kujifunza katika vita hii. Kwa kifupi nimeweza kukuandalia haya kwa leo.
Tukutane tena wakati mwingine. Usisahau kuweka email yako ili upate makala hizi moja kwa moja.

Vyanzo;

WIKIPEDIA; Second Congo War.

Nilichojifunza Leo.

Nilichojifunza Leo ni kipengele kipya kitakachokuwa kinakujia mara kwa mara kupitia blog hii Makirita Amani. Ningependa kipengele hiki kiwe kinakujia kila siku ila siwezi kuahidi hilo kwa sasa.
Kupitia kipengele hiki utajifunza mambo mengi kuhusiana na UONGOZI, SIASA, UCHUMI, MAENDELEO na hata HISTORIA za nchi yetu Tanzania, bara letu Afrika na hata Dunia kwa ujumla.
Tutajifunza mambo mengi yatakayotusaidia kuelewa zaidi nchi yetu na dunia kwa ujumla wakati tunajiandaa kuwa viongozi bora wa nchi yetu.
Kupitia kipengele hiki mimi na wewe tutajifunza mambo yatakayotuandaa kuweza kuisaidia nchi yetu, wakati huo mimi naendelea kujiandaa kuwa raisi wa nchi yetu Tanzania.
Karibu sana katika blog hii maalumu kwa maswala ya uongozi na kuhakikisha hukosi machapisho yanayowekwa, weka email yako kwenye box hapo juu na utapokea makala moja kwa moja kwenye email yako kila zinapowekwa.
Naamini tutaendelea kuwa pamoja kwenye safari hii.
Nakutakia kila la kheri.