Tabia Ya Mtu Ni Kama Kikohozi, Na Jinsi Ya Kujua Tabia Ya Mtu Kabla Hujamwamini.

Mara nyingi watu wengi hujaribu kuficha uhalisia wao kutokana na mazingira fulani ambayo wanaona wakikunjua makucha yao wataonekana vibaya, wengi wamefanikiwa kwenye eneo hili kwa kiasi fulani ila hushindwa kumaliza kama walivyotarajia. Katika maisha yangu nimefanikiwa kuishi na makundi ya aina mbalimbali nichukulie mfano mdogo wa kundi niliowahi kuishi nalo; wakati naanza maisha mapya kabisa ya jeshi la kujenga taifa 2009 wakati huo wanafunzi wa kidato cha sita walikuwa hawaendi tukiacha kipindi cha miaka ya nyuma na sasa wanavyoenda, na nakukumbuka majengo mengi yaliyajengwa tukiambiwa wanakuja kwa mjibu wa sheria wakati sisi tulikuwa wa kujitolea... wakati naingia kuna watu niliwaona hawezi kabisa kuongea na kuna watu walikuwa waongeaji sana, na kuna watu niliwaona kwa macho wana tabia nzuri na kuna watu niliwaona wana tabia mbaya lakini jinsi siku zilivyokuwa zinaenda wale niliowaona hawezi kuongea ndio walikuwa wasemaji wazuri kuliko wale walioonekana wanaweza kuongea na wale walioonekana wana wapole na tabia njema walikuja kuonekana ni wabaya kuliko wale walioonekana wabaya japo sio wote... nataka kusema nini hapa baada ya mfano huo japo umeanza kujiuliza sasa huyu Samson haya mambo ya Jeshi ameyatolea wapi TULIA KWANZA.
Tabia ya mtu nzuri haiwezi kufunikwa na tabia mbaya hata kama utachukua muda kumwelewa lakini matendo yake na zungumza yake itakuonyesha huyu ni mtu wa namna gani, anaweza akajitahidi kuendana na kundi alilolikuta lakini utashangaa ikifika eneo fulani anaonekana sio mwenzao, naona hujanielewa ni hivi kama umepanda gari na askari wa usalama barabarani amevaa tu kiraia halafu dereva/konda akaanza kufanya upuuzi utamwona akinyanyua mdomo yeye mwenyewe kumkemea hata kama mtakemea wote lakini kemea yake itakuwa tofauti.
SOMA; Matatizo Yote Ya Mahusiano Yanaanzia Hapa... Sehemu Ya Pili(2)
Tabia ya mtu mbaya pia huwezi kuifunika kwa tabia nzuri, japo utaweza kufanya mbinu ya kuiweka vizuri mwisho wa yote utabaki kuonekana wewe sio mtu mzuri maana ubaya wa mtu haupo kwenye macho bali ndani ya moyo wa mtu ndipo zinapotoka takataka zote hata akifanya nini ukweli utabaki palepale, ndio maana wengi wanasema aisee fulani nilimwona ni mpole na anajituma lakini siku hizi amekuwa ana tabia mbaya sio amekuwa na tabia mbaya ni kitu kilichokuwa ndani yake na kama hakuwa nacho ujue uharibu umeanza muda mrefu ndani ya moyo wake sasa hayo unayoyaona ni matokeo tu ya matunda ya kile kilichoanza siku nyingi kabla mwingine hajakiona.
Ukiona mtu uliyemwamini amebadilika ghafla jua sio ghafla ni katabia chake sema alivaa tu kasura cha uzuri wa nje ila ndani kwake sura halisi ndio hiyo tabia unayoiona, ni sawa na rafiki yako umempa taarifa kuwa utamtembelea kwake leo au wiki ijao nakwambia hata kama ni mchafu kiasi gani siku hiyo lazima ajitahidi kufanya usafi wa hali ya juu iwe kwa kufanyiwa ama kufanya yeye lazima ahakikishe mgeni wake aone hayo ndio maisha anayoishi.
SOMA; Maisha Ni Mchezo Na Sheria Za Kuushinda.
Unapata picha gani hapa? wengi kumbe maisha wanayoishi hawayapendi ila hawataki kuyaacha wameng'ang'ana kuishi maisha ya kinyonga lakini tatizo lao limebaki palepale. Kwa hiyo tunaona unaweza kujizua kukohoa (kubanja) kutokana na mazingira uliopo ila mwisho wa saa bila wewe kujua utaachia tu kikohozi chako tena kwa kishindo kikubwa kuliko awali.
Sasa basi mtu usiyemjua yaani mmefahamiana naye muda mfupi usipende kumwamini asilimia zote hata mimi usijilazimishe kuniamini hata kama unaniona naandika maneno mengi mazuri hii isikufanye ukaniamini haraka nenda taratibu mpaka uhakikishe moyo wako umeniamini, ndio maana wengi wakitokewa na jambo baya kuhusu mtu aliyemwamini kwa haraka utasikia aisee moyo wangu ulikuwa unakataa kabisa nisimpe kitu fulani ama nisimwambie kitu fulani, hivi hujawahi kuona unamuulizia mtu fulani kwenye makazi yake ama kazini kwake unatajiwa na alivyo, mfano; aisee unamuulizia yule kijana mwizi mwizi sana wa vitu vya watu, unamuulizia yule dada anayetoa sana mimba au unamuulizia yule kaka anayetembea sana na wadada yaani huyo kaka malaya sana jana tu ameingia hapa na mabinti wawili tofauti tofauti wa tatu wamegongana na mwenzake wameleteana fujo kweli... yaani badala ya kuelekezwa unapewa shutuma zake.. hiyo tunasema huwezi kuzuia kikohozi kwa kukibana muda mrefu hata kama mtu atavaa sura ya ubaya kama sio mbaya itajulikana tu.
Mwisho nikuase kwamba usihangaike kumjua mtu wala kumfuatilia sana habari zake... zipo nje nje tu ndio maana ukimgusia tu kwa kumsifia kitu fulani watu wanaguna wanajua unachoongea hujui chochote.
Makala hii imeandikwa na Samson Ernest, waweza wasiliana nami kwa njia ya WhatsApp 0759808081, email; samsonaron0@gmail.com
Nakutakia siku njema yenye mafanikio makubwa kiroho na kimwili.

0 comments: