Sehemu 7 Ambazo Unatumia Kupoteza Rasilimali Muda Wako

Muda au wakati ni rasilimali ambayo ikipotea hairudi tofauti na rasilimali fedha ambayo ukipoteza utaitafuta lakini ukipoteza muda huwezi kuupata hata kwa fedha. Mtunzi wa kitabu cha The Secret Code of Success ambaye ni Noah St. John anasema muda ni rasilimali ambayo huwezi kununua hata mabilioni ya Bill Gates hayawezi kununua hata dakika moja ya jana.
Hivyo basi, kumbe muda ni rasilimali muhimu ambayo hatuwezi kununua. Utajiri ambao tumepewa duniani bure kwa watu wote matajiri na masikini ni rasilimali muda. Wote tuna wakati sawa wa masaa 24 kwa siku. Kwa hiyo kila mtu duniani ni Tajiri wa muda au wakati. je unautumiaje utajiri wa rasilimali muda wako hapa duniani?
Zifuatazo ni Baadhi ya Sehemu Ambazo Unatumia Kupoteza Rasilimali Muda
1. Kuangalia Tv
Watu wengi wamekuwa wakipoteza muda sana kuangalia tv, mtu anapoteza masaa matatu mpaka matano kuangalia tv akifuatilia tamthilia kwenye tv. Kuangalia vipindi ambavyo havina tija kwako vipindi ambavyo havina matokeo chanya kwako, kiongozi wa kanisa Katoliki duniani papa francis, ana miaka 25 sasa hajawahi kuangalia tv yaani luninga mara ya mwisho kuangalia tv ilikuwa ni tarehe 15 mwezi saba mwaka 1990. Je tunajifunza nini kutoka kwa kiongozi huyu? Kama yeye ni kiongozi mkubwa wa kanisa hilo duniani mbona hajapungukiwa wala hajapitwa kwa nini wewe usiweze?
2. Kufuatilia Udaku
Unapoteza muda kumfuatilia msanii Fulani leo amefanya nini badala ya kutumia muda huo kuboresha maisha yako. Watu wengi ni wazuri kufuatilia magazeti ya udaku, habari za udaku, mitandao au blog za udaku kuliko kufuatilia blog nzuri zinazotoa elimu ya jinsi kuboresha maisha yako moja wapo ni hii unayosoma makala hii nzuri. Utumie muda wako kufuatilia vitu vya maana ambayo vinabadili fikra yako acha kuwa mtumwa wa kila siku wa kufuatilia habari za udaku.
SOMA; MUDA–Kitu Chenye Thamani Kubwa Ila Kisichothaminika Na Wengi.
3. Kufuatilia Mitandao ya Kijamii kwa Faida Hasi
Kuwa katika mitandao ya kijamii kama vile facebook, twitter, na kadhalika siyo mbaya, je uko katika mitandao hiyo ya kijamii kwa malengo gani? Unatumiaje muda wako katika mitandao hiyo ya kijamii kila dakika uko online kwenye mtandao zaidi ya mmoja unapata muda wapi wa kufanya kazi yako kwa ufanisi? Tenga muda wako vizuri kataa kabisa kuwa mtumwa wa kisaikolojia ukikaa kidogo bila kuingia unahisi unapitwa na habari wenzako wanaingiza siku wewe unafuatilia habari.
4. Kukaa Vijiweni
Wimbi la watu kukaa vijiweni na kupoteza muda linaongezeka kila siku ukipita kona hii utakuta watu wamekaa makundi vijiweni wakijadili serikali pengine sijui chama Fulani wamefanya hivi ni mambo mengi yanayojadiliwa kwenye magenge ya watu. Watu hawana kazi za kufanya wanapoteza muda bure na wala hajutii kwa muda anaoupoteza. Tumia muda huo kujifunza namna gani unaweza kubadili maisha yako. Acha kauli hizi za kusema ngoja niende kwa Fulani au kijiweni nikapoteze muda kidogo.
5. Kubishana
Hii ni sehemu moja wapo ambayo watu pia wanapoteza rasilmali yao nzuri ya muda katika kubishana. Watu wanabishania vyama vya siasa, timu za mipira kuna wengine wanabishana katika mpira mpaka wanapigana hii ni kwa sababu kila mmoja anataka asikilizwe kile anachosema yeye katika timu yake ndio sahihi. Unapoteza muda kushabikia vitu wakati huna hata hisa moja katika vitu hivyo unavyobishania ambavyo havikusaidii kuboresha maisha yako kabisa zaidi ya kukusababishia hasara ya kuendelea kuwa mtumwa wao.
SOMA; Lakini Nitapitwa.... (Sababu Ya Kijinga Inayokufanya Upoteze Muda)
6. Umbea na Majungu
Unapoteza muda kuongea maneno ya uchonganishi juu ya mtu Fulani unapiga umbea na majungu. Unaongea maneno ambayo yanaleta majeraha katika maisha ya watu, unapandikiza chuki kwa watu kwa kupiga majungu unapoteza muda wako bure kupiga umbea na majungu bila malipo yoyote ni hatari sana tumia muda wako kujenga na kuongea thamani yako katika jamii ya yako na acha kuwa mtu wa umbea na majungu kila siku.
7. Kuhudhuria Vikao au Mikutano Ambayo Haikupi Faida
Kuna vikao vingi sana katika jamii zetu, mikutano mingi ya kila siku ambayo haina matokeo chanya kwetu bali ni kupoteza wakati wako. Leo nakuomba sema HAPANA kwa vikao au mikutano ambayo haikupi faida yoyote ambavyo vinakula muda wako bure ambao muda huo ungeweza kutumia vizuri kuboresha maisha yako au hata kuongeza thamani katika jamii yako.
Hivyo basi, acha kutumia muda wako kudhurura ovyo yaani kutembea bila sababu ya msingi, tumia muda wako vema, muda ni mali katika karne hii usikubali mtu akupotezee muda kwa kitu ambacho hakina manufaa kwako fanya kile ambacho unatamani kufanya kwa muda huu katika Nyanja zote usisubiri ruhusa ukiendelea kusubiri ruhusa ndio unazidi kupoteza muda na umri pia unakwenda omba samahani kuokoa muda, Muda siyo rafiki na maisha ni mafupi .
Makala hii imeandikwa na Deogratius Kessy ambaye ni mwandishi, mhamasishaji na mjasiriamali, unaweza kuwasiliana naye kupitia namba 0717101505 au kwa barua pepe deokessy.dk@gmail.com au unaweza kutembelea tovuti yake www.actualizeyourdream.blogspot.com

0 comments: