Mambo 20 Niliyojifunza Kwenye Kitabu THE ART OF THE START.

Habari rafiki, ni matumaini yangu unaendelea vizuri. Wiki hii tunaendelea na utaratibu wetu wa kushirikishana mambo 20 nilijifunza kwenye kitabu. Leo tunaangazia kitabu kinachoitwa THE ART OF THE START. Kitabu kimeandikwa na Guy Kawasaki. Kwa ufupi ni kwamba kitabu hiki ni kizuri sana. Kama unayo mpango wa kuanza biashara yeyote hata kuanza kitu chochote, nakwambia kitabu hiki hakijaacha kitu, hupaswi kukosa. Hata wale ambao tayari wapo kwenye biashara kitabu hiki ni zaidi ya “Asset”.

art of start

Kitabu kianelezea mambo mengi sana, kuanzia jinsi ya kutengeneza jina la kampuni yako, jinsi ya kutengeneze mpango biashara (business plan), jinsi ya kupata mtaji kutoka kwa wawekezaji, jinsi ya kuanda presentation, jinsi ya kufanya branding za ukweli, jinsi ya kuwasiliana kwa njia ya email, jinsi ya kuajiri watu wenye uwezo wa kuiinua kampuni yako, jinsi ya kuanzisha ushirikiano wa kibishara (partnering) n.k, hayo ni baadhi tu. Hapa chini nimechukua vitu vichache sana, naona kabisa sijakitendea haki kitabu hiki. Mwishoni nimeweka anwani kwa atakayependa kukipata kitabu hiki nitampatia bure kabisa.

SOMA; Kanuni Sita(6) Muhimu Za Kushinda Tatizo Lolote Unalokutana Nalo.

Karibu tujifunze

1. Katika kutafuta jina la kuipa kampuni unayoanzisha, jaribu kutafuta jina rahisi na fupi ambalo linatamkika vizuri au pia lenye uwezo wa kua kitendo “VERB POTENTIAL." Mfano Google, mtu akitaka kukwambia ukatafute kwenye google, anakwambia …”nenda uka Google. Tengeneza jina ambalo litakua rahisi kutumiwa na watu mbalimbali kama vile wateja, washirika wako pamoja na wawekezaji

2. Ajiri watu wenye uwezo mkubwa kuliko wako na mwenye kuamini kwamba kampuni au shirika lako linaweza kuibadili dunia

3. Kuajiri mtu mwenye uzoefu kutoka kwenye shirika au kampuni kubwa iliyofanikiwa sio kigezo kwamba na kampuni yako inayooanza itafanikiwa. Maana pengine mtu huyo hata hakua na mchango wowote kwenye mafanikio ya shirika hilo lililofanikiwa. Chunguza zaidi

4. Ujasiriamali sio vita. Lengo la biashara yako sio kuua biashara ya mwingine, kuwa chanya.

5. Mjasiriamali sio cheo cha kazi, bali ni hali ya akili/ufahamu wa watu wenye kutaka kuleta mabadiliko

6. Mwanzoni kuelekea kwenye ujasiriamali kila mjasiriamali huogopa. Wewe sio wa kwanza kuogopa, kufanikiwa kwako kutategemea unaikabili vipi hofu hiyo na kuishinda. Bila hivyo utakua mtu wa kusubiri kuanza kesho, na kesho ndo hiyoo unajikuta miaka 60..ukisubiri kesho

7. Wanaofanikiwa sana, hua wana madhaifu makubwa tu. Watu wasio na mapungufu yeyote hua huishia kua watu wa kawaida tu. Maana wale wasiokua na madhaifu huridhika na hali waliyonayo wakiona kua wamekamilika.

8. Shirika au kampuni inafanikiwa kutokana na utekelezaji mzuri na sio mpango mzuri wa biashara. Unaweza kua na business plan nzuri sana, lakini usikufikishe mahali. Hakikisha utekelezaji unakua mzuri.

SOMA; Kitu Pekee Unachoweza Kukidhibiti Kwenye Maisha Yako.

9. Unapofanya ushirikiano wa kibiashara (Business partnership) usifanye ili kufurahisha watu, hakikisha kuna maslahi pande zote (Win-win situation)

10. Haijalishi unajua nini au unamjua nani, bali kinachojalisha ni nani anakujua. Mfano Unaweza ukawa unamjua Reginald mengi, lakini yeye hakujui, uwezekano wa kusaidika ni mdogo.

11. Saidia watu wengi kadri uwezavyo. Msaada wa kweli ni ule ambao unatoa kwa watu ambao hawana uwezo wa kukurudishia msaada baadaye. Na unapomsaidia mtu usitegemee kurudishiwa fadhila, maana ukitegemea kupata kitu baadaye utakua hujasaidia bali unafanya biashara.

12. Unapofanikiwa katika biashara tenga fungu kwa ajili ya kurudisha kwenye jamii, hii ni njia moja wapo ya kujitangaza

13. Sababu kubwa na nzuri ya kuanzisha biashara ni kutengeneza maana, kutengeneza bidhaa au huduma ambazo zitaifanya dunia kua sehemu pazuri zaidi ya mwanzo. Kazi yako ya kwanza ni kuamua ni jinsi gani utakavyo tengeneza maana.

14. Mfumo wa biashara ni muhimu sana. Haijalishi ni biashara kubwa kiasi gani unaanzhisaha, ni lazima uweze kutengeneza njia kutengengeneza pesa. Mfumo mbovu utapelekea biashara kua na maisha mafupi. Katika kufanya hili unahitaji kujiuliza maswali haya muhimu:

· Nani mwenye pesa zako mfukoni mwake?

· Jinsi gani utazichukua pesa hizo kuja mfukoni mwako?

15. Usisubiri mpaka uwe na bidhaa au huduma iliyokamilika kabisa ndio upeleke sokoni, la hasha, muda upo wa kurekebisha kadri siku zinavyokwenda na uhitaji wa soko.

16. Haijalishi umenazaje bali inajaslisha umemalizaje. Unaweza anza vizuri ukamaliziia kwa udhaifu au vibaya, unaweza pia kuanza kwa udhaifu ukamaliza kwa nguvu. Usivunjike moyo unapoanza kitu kwa udogo au kwa hali chini, unayo nafasi ya kufanya mageuzi mbele ya safari.

SOMA; USHAURI; Kuhusu Kujiunga Na Biashara Ya Mtandao(Network Marketing) Na Mambo Muhimu Ya Kuzingatia.

17. Tafuta mshirika wa kibiashara (Business partner). Mabilionea unaowaona kwenye dunia hii hawakuanza peke yao, walitafuta washirika sahihi wa kibiashara. Hata wavumbuzi wakubwa kama Thomas Edison walianza na ni timu nzuri. Unaweza kusema “sasa nikitafuta mtu wa kushirikiana kibiashara si itabidi tugawane mapato yatokanyao na biashara, sasa si bora tu ni miliki mwenyewe kampuni ili chote kiwe changu” . Kumbuka Ni afadhali kumiliki kampuni kubwa kwa aslimia 50, kuliko kumiliki kampuni ndogo kwa asilimia 100.

18. Jikite katika kuwaelewesha wateja wako kwanini wanunue kwako na si kwa washindani wako, wateja wako wanachotaka kujua ni faida gani zaidi ziko kwako, hawajalishwi na jinsi gani unavyotaka kuharibu uhsindani uliopo. Kwa hiyo unapozungumza na wateja wako usilogwe ukaishia kupondea washindani wako, wewe elezea ubora wa bidhaa au huduma unayotoa na uwe specific.

19. Katika kuandaa mpango wa biashara (Business plan) nguvu kubwa weka katika muhtasari mkuu (executive summary) , maana hapo ndipo patapelekea mtu aendelee mbele au aishie hapohapo. Ukweli ni kwamba hata kama mpango biashara wako ni mzuri kiasi gani, ukishindwa kuonyesha hapo mwanzoni ndo basi tena. Hakikisha executive summary inashiba kiasi cha kumshawishi mwekezaji aendelee kupekua kurasa za mbele.

20. Soma kwa bidii sana. Wajasiriamali wa viwango vya dunia (world-class), wansoma sana, kusoma kutafanya uwe mbunifu zaidi ya wengine. Soma tena na tena, usomee tena

Asanteni sana tukutane wiki ijayo. Kama utapenda kupata kitabu hiki cha THE ART OF THE START wasiliana nami. Nitakupatia bure kabisa. Mwisho wa ofa hii ni tarehe 30 May 2015.

Makala hii imeandikwa na Ndugu Daudi Mwakalinga mwandishi, mhamasishaji na mshauri katika masuala ya kilimo. Unaweza kuwasiliana naye kwa simu 0763 071007 au barua pepe daudimwakalinga@yahoo.com au dd.mwakalinga@gmail.com

0 comments: