Jambo Moja Muhimu Unalotakiwa Kujua Kuhusu Miasha Na Kulitumia Kila Siku Ili Kufanikiwa.

Ndugu msomaji wa JIONGEZE UFAHAMU napenda nikushirikishe jambo moja la muhimu sana katika maisha yako na maisha ya kila binadamu. Kama unaweza kukumbuka miaka kadhaa nyuma ulipokuwa mdogo na usiyejua mambo mengi kama ilivyo sasa hivi. Ulipokuwa mdogo sana ulikuwa hujui kusoma wala kuandika. Lakini unaposoma hapa sasa hivi ni ushuhuda tosha kwamba sasa hali ni tofauti kwani umeweza kusoma nilichokiandika. Pengine kuna vingi sana unavyojua na bado unaendelea kuvijua kadiri siku zinavyosonga mbele. Ulikuwa hujui kuendesha baskeli au gari lakini sasa unajua. Naomba uelewe kwamba ulizaliwa bila kujua chochote na kila kitu umejifunza hapa duniani. Ni ushahidi tosha kwamba kama ukiamua kujifunza kitu chochote hapa duniani utaweza kwani hakuna jambo lisilowezekana wala jambo jipya chini ya jua.

SOMA; Kozi 1100 Unazoweza Kujifunza Bure Kupitia Mtandao.

clip_image002

Ushauri wangu kwa leo basi ni kuhusu kujielimisha. Waswahili walisema elimu ni kama bahari na haina mwisho. Maana yake ni kwamba kujifunza na kujielimisha ni mambo ambayo yanatokea kila siku katika siku zote za maisha yako. Jaribu kujitathmini na kujiuliza kwa siku ya leo umejifunza kitu kipi kipya ambacho ulikuwa hukijui na kitakusaidia katika kusonga mbele kuelekea katika mafanikio yako. Ninaposema mafanikio sizungumzii mafanikio ya kipesa au kiuchumi peke yake bali mafanikio katika ujumla wake kuanzia afya, mahusiano, kielimu, kimaisha na yanayofanana na hayo. Hivyo basi kwa kila siku iendayo kwa Mungu kaa chini na ujitafakari ni kwa kiasi gani umeweza kujifunza kitu kipya. Kuna mtu aliwahi kusema kwamba ‘’Mtu yeyote asiyejifunza ni mzee hata kama ana miaka 20, na mtu yeyote anayejifunza ni kijana hata kama ana miaka 100’’. Maana yake ni kwamba muda na siku yoyote ambayo utaacha kujifunza unaanza kuhesabiwa kama mzee. Epuka uzee kwa kuwa tayari kujielimisha na kujifunza.

SOMA; UKURASA WA 13; Jifunze Kila siku.

Vitu vya kujifunza katika maisha ni vingi mno kiasi kwamba mpaka unafikia mwisho wa maisha yako utakuwa hujavimaliza. Kuna vyenye faida na visivyo na faida. Nakushauri ujifunze vile ambavyo unavihitaji katika maisha yako na si kujifunza vitu ambavyo vitakupotezea muda wako bure. Jifuze vitu vya kukujenga kama namna ya kuwa tajiri, namna ya kuwa na afya bora, namna ya kutumia vifaa vya teknolojia ya kisasa, namna ya kuwa bora katika fani yako na namna ya kuwa na uhusiano mzuri, namna ya kujenga familia bora na vingi vinginevyo.

Unaweza ukajiuliza kama umechelewa kujifunza au huwezi tena kujifunza. Kumbuk hakuna mtu yeyote aliye mkubwa kuweza kujifunza mambo mapya na hakuna umri wa ukomo wa mafanikio. Anza leo na utaona mafanikio yake kesho. Pia unaweza kujiuliza ni wapi unapoweza kujifunza vitu hivi. Jibu ni rahisi sana, unaweza kujifunza kutoka kwa watu wengine;kwa waliofanikiwa utajifunza mbinu walizotumia kufikia mafanikio makubwa na hivyo na wewe uzitumie na kwa watu walioshindwa utatumia makosa wanayofanya kama funzo kwako ili usiyarudie. Pia unaweza kujifunza kwa kusoma vitabu mbalimbali. Watu wengi hawasomi hata angalau kitabu kimoja kwa mwaka.

SOMA; Uwekezaji Muhimu Kwako Kufanya Na Unaolipa Sana.

Unaweza kuanza kusoma kitabu kimoja kwa mwezi na baadae vitabu kadhaa kwa mwezi. Watu wengi waliofanikiwa ni wasomaji wazuri wa vitabu kwani vitabu ni hazina isiyofilisika. Pia unaweza kujifunza kwa kutumia mtandao wa internet. Tumia mtandao kwa faida yako kwani ukiutumia vibaya utageuka adui wako, kwani utapoteza muda wako mwingi ambao ungeutumia kuzalisha au kujifunza. Pia unaweza kujifunza kwa kufanya mwenyewe kitu fulani na kupitia makosa utajifunza kitu na siku ukikifanya tena kitu hicho utakuwa bora zaidi. Pia unaweza kujifunza kupitia vyombo vya habari kama televisheni,magazeti na hata redio. Kama utaona inafaa unaweza pia kuingia darasani uliweze kujifunza mambo mapya au kuongeza ujuzi kwa kile unachikifahamu. Kumbuka hakuna njia moja iliyo sahihi zaidi na hakuna njia moja ya kujifunza. Jua kuwa njia hizo na zingine ambazo sijazitaja zinaweza kufanya kazi kwa pamoja ama kwa kushirikiana.

Kumbuka kuwa huwezi kuwa bora kama hujielimishi. Jifunze na jielimishe kila siku.

Makala hii imeandikwa na Nickson Yohanes

Unaweza kuwasiliana na nae kwa kwa: simu: 0712 843030/0753 843030

e-mail: nmyohanes@gmail.com

Pia unaweza kutembelea blog yake: www.lifeadventurestz.blogspot.com kujifunza zaidi

0 comments: