Siri Ya Mfereji Wa Upendo Kuelekea Kwenye Bahari Ya Mafanikio

Upendo ni neno tunalolisikia kila mara. Upendo una nguvu zaidi ya nguvu ya kifo. Upendo kutafsiri n hauna ukuta. Upendo una sifa nyingi sana. Hauhesabu mabaya, haujivuni, husamehe, haulipizi kisasi, upendo hustahimili yote.
Kama ukipenda ukampenda mtu waswahili wanasema hata jalala lao utaliona zuri. Yaani hakuna ubaya utakaouona kwa mtu kama ukimpenda. Lakini hata akikuudhi kiasi gani utamsamehe kwakua unampenda sana.
Ukipenda wale wanaokuchukia, usipolipiza kisasi, usipowaonyesha ubaya wowote, kama wanakuchukia basi wanaweza kubadilika. Kama wasipobadilika basi wataondoka mahali ulipo. Upendo una nguvu sana.
Mahali palipo na upendo kuna maendeleo sana. Kama wanandoa, wanafamilia, wanaukoo au wanakijiji fulani wanapendana basi mambo yao mengi huenda vizuri. Kwakua kila mmoja yupo katika eneo lake kuhakikisha kuwa mwenzake anaishi kwa furaha. Ni rahisi kufanikiwa kama una upendo na hauna kinyongo na watu wengine.
Unawezaje kuwapenda hata wale wanaokuudhi?
“Kuna usemi wa Kiswahili unaosema “akuchomaye mchome” au “mpende akupendaye asiyekupenda achana naye” kuna baadhi ya watu hutafsiri vibaya usemi huu. Yaani mtu akimfanyia kitendo kibaya na yeye analipiza. Sio busara na sio jambo jema kumfanyia mtu ubaya hata kama yeye amekufanyia hivyo. Kwa kufanya hivyo utaongeza chuki na uadui.
Katika vitabu vya dini tunashauriwa kuwapenda wasiotupenda ili tupate thawabu. Kwakua kuwapenda wanaotupenda pekee kutawafanya wale wanaotuchukia wasibadilike kwakua sisi pia tunawachukia na hakutakuwa na mabadiliko hivyo hatupati thawabu kwa kuwachukia wanaotuchukia.
Lakini ukimpenda anayekuchukia basi ataona aibu tu. Sio kwa siku moja lakini baada ya muda mtu huyu anaweza kubadilika.
Naomba nikufundishe mbinu moja itakayopunguza kasi ya chuki na kuleta upendo ndani yako. Ukiamka tu, sema moyoni ninawapenda watu wote. Endelea kujikumbusha neno hili siku nzima. Kila unayeonana nae jiambie kuwa unampenda. Hata akiongea neno baya wewe jiambie moyoni kwa nguvu zote kuwa unampenda. Akikufanyia kitu kibaya, muhurumie huwezi kufahamu ana msongo wa mawazo kiasi gani. Badala ya kujenga chuki juu yake ambayo inaweza kukuletea madhara ya kiafya jiambie kuwa unampenda. Itakusaidia kupunguza vurugu na utaona moyoni mwako una amani.
Mara nyingi watu wenye chuki hupenda kupinga na kukebehi maneno au juhudi za mtu mwenye mawazo ya mafanikio. Watu hawa hufanya hivi mbele za watu ili kupata mashabiki na kukufanya wewe ujisikie vibaya. Hutamani ubishane nao na kugombana au baadae upate muda wa kutafakari yale unayotaka kufanya kuwa hayawezekani. Usiwape nafasi watu wa aina hii kukupotezea malengo yako. Usifanye mambo yako ili kuwaonyesha kama unaweza pia. Fanya kwaajili yako na kwaajili ya furaha ya moyo wako na ya wale ambao wako upande wako kuhakikisha unafikia pale unapotamani ufike. Kama hukufanikiwa kufikia pale ulipokusudia jipange vizuri na uendelee na mapambano. Lakini usimchukie mtu yeyote kwani ukiwa na chuki mafanikio kwako ni ndoto. Upendo na roho safi ni mfereji muhimu kuendea kwenye bahari ya mafanikio.
Makala hii imeandikwa na Esther Nguluwa.

0 comments: