Huu Ndio Uwekezaji Bora Zaidi Unaoweza Kuufanya.

Uwekezaji kama tunavyofahamu ni njia ya kupata kipato ambayo imekuwa ikihubiriwa na watu wengi sana kuanzia mashuleni, vyombo vya habari na hata mitaani. Lakini watu wengi wamekuwa wakitaja vitu vya kufanya hasa katika kuwekeza pesa kama mtaji. Sipingani nao katika hilo lakini kabla ya kuwekeza katika pesa lazima kwanza uwekeze katika hili. Najua utashangaa sana na kudhani kuwa ningekutajia eneo la kuweka pesa zako, la hasha.

Ukweli ni kwamba kabla hujawekeza katika pesa wekeza katika akili yako. Ukiwekeza katika akili yako kamwe hutafilisika, kwa sababu kuwekeza kwingine kabla ya akili ni sawa na kucheza masumbwi bila kujiandaa, ni lazima tu utashindwa tena katika mizunguko ya awali kabisa. Ubongo wako ndio kompyuta yenye nguvu na kasi zaidi kuliko zote hapa duniani. Lakini kama vile kompyuta inavyofanya kazi kwa kuelekezwa ndivyo na akili yako inavyofanya kazi kwa kuelekezwa pia. Kama utaelekeza akili yako ikuletee utajiri italeta utajiri, kama utaelekeza ikuletee umasikini vile vile itafanya hivyo. Kama utahitaji huzuni ndivyo na akili yako itakavyokuletea. Kila kitu kinaanza katika akili yako. Kila utakachowaza ndivyo utakavyokuwa.

SOMA; Hii Ni Kazi Yenye Malipo Makubwa Sana Ambayo Unaweza Kujifunza Kuifanya

Namna ya kuwekeza katika akili

Waza katika uwezekano (possibility thinking)

Ili uweze kufanikiwa ni lazima ujaze akili yako na vitu vizuri vyenye kukujenga na si kinyume chake. Huhitaji mtu kuwekeza katika akili yako kama hujaamua mwenyewe moyoni mwako kuwekeza. Kwanza kabisa ondoa takataka zote zilizopo akili mwako kwa kuwaza uwezekano wa kufanikiwa yaani kuwaza katika mambo chanya zaidi na kuachana na mambo hasi. Pili tafuta marafiki ambao watakujenga katika kukukosoa kwa mazuri, kukutia moyo pale unapokuwa katika hali ngumu au unapotaka kujaribu jambo jipya. Kama marafiki ulio nao ni wale wa kukurudisha nyuma basi unakosea sana na inakubidi ubadili jeshi lako la marafiki. Bila kufanya hivyo akili yako itajazwa kukata tamaa, kukwazwa na hata kurudishwa nyuma na mafanikio kuwa ndoto za Ali Nacha kwako.

SOMA; Watu Hawa Wanakurudisha Nyuma.

Hudhuria semina za kuelimisha

Jitahidi kuhudhuria semina za uwekezaji na za kujenga tabia. Jitahidi kuhudhuria semina za kujenga tabia kwanza kabla hujaanza kuhudhuria za kuwekeza katika fedha kwani kama hujawekeza katika kubadili baadhi ya tabia ambazo ni adui kwa mwekezaji kama nidhamu ya fedha na uongozi, utakuwa sawa na kujenga nyumba nzuri bila msingi imara.

Jifunze kwa watu waliofanikiwa

Hakuna mtu aliyefanikiwa kwa kufanya kila kitu peke yake. Unahitaji kujifunza kutoka kwa watu waliofanikiwa hasa kwenye fursa, changamoto, biashara na hata tabia zao. Usiende kwa mtu aliyefanikiwa ili ukaombe fedha kwani tatizo lako sio pesa bali elimu kuhusu pesa (financial education). Watu wengi waliofanikiwa ni watu ambao wako tayari kusaidia watu wengine waweze kufanikiwa. Watu waliofanikiwa huonekana kuringa ama kujisikia lakini sababu kubwa ni kutingwa kwao na vitu vingi vya kufanya. Kama wapo wanaoringa basi ni tabia zao tu hivyo usiogope kuwafuata ili ujifunze kutoka kwao.

SOMA; Kozi 1100 Unazoweza Kujifunza Bure Kupitia Mtandao.

Soma sana vitabu

Kama kuna njia ya nzuri na ya kwanza kukushauri katika kujenga akili yako ni kusoma vitabu. Narudia tena soma vitabu sana kadiri unavyoweza. Kwa mara ya kwaza itaonekana ni kazi ngumu lakini ukiwa na nia ya dhati ya kujenga akili yako basi hili litakuwa rahisi na ukizoea itakuwa rahisi zaidi. Soma vitabu vya uwekezaji, tabia, uongozi na hata vitabu vya kutia moyo (inspirational books). Soma kila siku na kufanyia kazi ulivyosema. Matatizo yote ya dunia hii siyo mapya na karibu yote yashapata utatuzi na watu wakaandika katika vitabu. Kumbuka pia ‘’Mtu anayetoa vya mfukoni kwake na kuwekeza katika akili yake hatafilisika kamwe’’. Naamini na wewe utafanya hivyo, watu waliofanikiwa husoma sana vitabu na kusikiliza ‘’vitabu sauti’’ (audio books) kila siku. Anza leo na utaona mafanikio mlangoni kwako. Kumbuka hakuna njia ya mkato ya kufanikiwa na kila kitu kina gharama zake ambazo lazima uwe tayari kuzilipa ili ufanikiwe.

Nakutakia kila la kheri na uwekezaji mwema.

Makala hii imeandikwa na Nickson Yohanes ambae ni mjasirimali na mhamasishaji. Unaweza kuwasiliana na naye kwa: simu: 0712 843030/0753 843030 Barua pepe: nmyohanes@gmail.com Pia unaweza kutembelea blogu yake: www.lifeadventurestz.blogspot.com kujifunza zaidi.

Imesahihishwa kwa kiswahili sanifu na Rumishael Peter ambaye ni Mhariri wa vitabu/makala za Kiswahili na Mjasiriamali barua pepe: rumishaelnjau@gmail.com simu 0713 683422.

0 comments: