Hivi Ndivyo Unavyodhulumu Maisha Yako Wewe Mwenyewe.

Umezaliwa uishi wewe kama ulivyokusudiwa kuishi na kuwa. Usiishi maisha kufurahisha au kuwapendeza wengine tambua kwamba wewe ulivyozaliwa ulipewa uwezo wa kufanya kitu kilichokuleta hapa duniani. Acha kuishi ukitamani kuwa kama mtu fulani, acha kuigiza kuwa kama mtu fulani, acha kufanya mambo kama wengine wanavyofanya, unayo namna yako ya kufanya, unayo namna yako ya kuishi kama ulivyokusudiwa kuwa.

Huenda tangu uzaliwe umekuwa ukisikia sauti nyingi zikikuambia kuwa hauwezi kufanya kitu fulani kwa ajili ya sababu fulani, wengine wametumai mwonekano wako, umri wako kupima kwamba kuna vitu huwezi kufanya na wamekuambia sana habari hizo nawe umezipokea na kuziweka akilini mwako, umeamini hivyo na unaona huwezi kufanya jambo lolote kama walivyokuambia. Ndugu tambua hauwi kama watu wanavyokuambia upo, pengine unapenda kuimba sana lakini jamii yako imekuaminisha kuwa hauna sauti nzuri ya kuimbia nawe umekubali hilo hata ukijaribu kuimba unasikia sauti ikakuambia una sauti mbaya sana, hauwezi kuimba nawe unaiamini hiyo, unaacha kuimba.

SOMA; Kama Unataka Maisha Yako Yawe Bora Na Yenye Mafanikio, Acha Kufanya Kitu Hiki Kimoja.

Ndugu hatuendi hivyo hata kama kila mtu anaona hauwezi , hata kama hakuna hata mtu mmoja anayekuamini kuwa unaweza fanya jambo hilo, kama wewe mwenyewe unaamini kwamba unaweza, unajiamini, endelea kufanya hicho kitu, hata wasipokuelewa leo, wataelewa baadaye sana. Usiache kufanya jambo fulani kwasababu watu wamekuambia huwezi, usiache kufikia ndoto zako kwa kuwa tu umekutana na wasioielewa ndoto yako wakakukatisha tama, ndugu tambua ni wewe umeota/unaota hiyo ndoto hivyo usitegemee mwingine aielewe sana . Umeota wewe, ukiielewa iweke kwenye matendo, ndoto inaweza isieleweke sana lakini ukishaifanyia kazi watakuelewa tu.

Wengi wetu tumeishi maisha yetu tukijitahidi kuwa kama fulani kwa kuwa kuna vitu huyo mtu anavifanya na tunatamani kuvifanya bila kujali kama ndivyo vinavyotupa amani mioyoni mwetu, maana hata kama unapenda hicho kitu kama unakifanya kwa kuwa tu fulani anakifanya huwezi furahia na utatumia nguvu nyingi sana kukifanya, wengine wanafanya vitu fulani kwa kuwalabda wazazi wametaka ufanye , au jamii imemlazimisha afanye au pengine kwa kuwa atapata pesa, lakini hafanyi kwa kuwa ndicho kitu anatakiwa kukifanya, hafanyi kwa kuwa ndicho kitu ameumbwa akifanye na kwa kufanya hivyo wengi wamekuwa wakipata ugumu sana kufanya vitu hivyo kwa ukamilifu maana havipo ndani mwao, nguvu ya kufanya hivyo vitu inatokea nje na si ndani, hivyo lazima waumize akili sana kuweza kupata kitu kipya kila leo.

SOMA; Hivi Ndivyo Unavyoweza Kuishi Maisha Yako Kwa Ukamilifu.

Wewe kama ulivyo una uwezo wa kufanya hicho kitu unachopenda na unachotaka kufanya bila kuangalia kinakulipa nini, kile kitu ambacho ukifanya unafurahia, basi amini unaweza kukifanya bila kusikiliza sauti na kelele zinazokuambia kinyume, zipuuze, chagua na amua usikie sauti gani maishani mwako ili iwe rahisi kwako kufanya kile umeletwa kufanya kwa ukamilifu na kuishi maisha yale umekusudiwa uishi, yaani kuishi wewe na si mwingine.

Angalia ni watu gani wamekuzunguka na maneno yao yamejaa nini? Je ni watu wanaokufanya ujione duni zaidi, ujione huwezi kufanya hilo? Kuwa na marafiki wenye mitazamo sahihi maana mtazamo chanya tu hautoshi, wale ambao wanakukubali na kuamini kuwa nawe una kitu cha kuwaambia, wanaamini kuwa nawe unacho kitu cha maana cha kuwafaa maishani mwao, wanaoweza kukaa chini kukusikiliza na kuona thamani yako, wale watu wanaokufanya uzidi kujikubali kujiamini na kufanya kile unafanya kwa ujasiri zaidi. Watu wenye mitazamo isiyo sahihi si salama sana kwa afya yako labda kama unakaa nao kwa ajili ya wewe kuwasaidia nao waweze kuishi maisha yao, waweze kuwa wao.

SOMA; Karibu Kwenye Semina Ya Mafanikio Kwenye Biashara Mwaka 2015.

Jambo la msingi ili uweze kuwa wewe maishani mwako ni pamoja na wewe kuwa na muda wa kutosha wa kuwa na wewe ili uweze kujielewa zaidi. Wengi wetu tuna muda wa kutosha kukaa na watu wengine, kuangalia televisheni, kusikiliza radio au kukaa kwenye mitandao ya kijamii lakini hatuna muda na sisi wenyewe, hakikisha unapata muda wa kuwa na wewe kwanza ndipo utakapoweza kujielewa zaidi na hata watuwa je watakuona wewe halisi ukiishi.

Makala hii imeandikwa na Beatrice Mwaijengo Mawasiliano; 0755350772/bberrums@gmail.com Pia unaweza kutembelea blog yake www.jitambueunani.blogspot.com kujifunza zaidi.

Makala imeangaliwa muundona lugha fasaha na Rumishael Peter ambaye ni Mhariri wa vitabu/makala za Kiswahili na MjasiriamaliEmail: rumishaelnjau@gmail.com simu 0713 683422.

0 comments: