NENO LA LEO; Kuhusu Kufanya Mambo Mengi.

It's important to focus on one thing at a time. Even in the Roman times they understood this with their Proverb; "The man who chases two rabbits catches none."

 

Ni muhimu kufanya jambo moja kwa wakati. Hata wakati wa Roma walielewa hili kwa msoemo wao; mtu anayekimbiza sungura wawili, hushindwa kumsiha hata mmoja.

Chagua mambo machache na uyafanye kwa ufanisi mkubwa na utapata mafanikio makubwa sana.

TUKO PAMOJA.

Hili Ndilo Kosa Kubwa Tunalokwenda Kufanya Watanzania 2015.

Mwaka 2015 ambao ulikuwa ukisubiriwa kwa hamu sana na watanzania wengi umekaribia kabisa kufika. Huu ni mwaka ambao uchaguzi mkuu wa nchi yetu utakwenda kufanyika na hivyo wananchi kupata nafasi ya kuchagua diwani, mbunge na raisi ambaye tunaona anatufaa.

Mwaka 2015 umekuwa ukisubiriwa kwa muda mrefu kwa sababu wananchi wengi tumeaminishwa na kuamini kwamba baada ya uchaguzi wa mwaka 2015 na chama tawala kuondoka madarakani maisha yetu yatakuwa mazuri sana. Ni imani nzuri sana ambayo tumekuwa nayo hasa ukizingatia hali ya nchi kiuchumi ipo chini sana ukilinganisha na rasilimali tulizonazo.

Pamoja na kuwa na imani hii nzuri, kuna kosa kubwa sana ambalo watanzania tutakwenda kulifanya mwaka huo 2015. Kosa hili litatugharimu tena miaka mingine mitano au hata zaidi ya hapo kama hatutaendelea kujifunza.

Kosa hili kubwa ni kutokuwa na vigezo vya kiongozi tunayemtaka sisi wananchi. Na kwa kukosa vigezo hivi tutarudia makosa ambayo tuliyafanya nyuma kwa kuchagua watu kutokana na umaarufu wao. Kutokana na kuangalia umaarufu tumechagua viongozi wengi ambao wameishia kutuangusha na kushindwa kutimiza ahadi zao wenyewe.

Ni lazima sisi kama wananchi bila hata ya kuambiwa na wanasiasa, tuwe na vigezo vya aina ya kiongozi tunayemtaka. Na hii ni kuanzia udiwani, ubunge na uraisi. Lazima sisi tuwe na vigezo vyetu kisha wale watakaojitokeza kuomba nafasi hizo tuwachuje kwa kutumia vigezo vyetu.

SIASA

Ilivyo sasa ni kwamba wananchi hatuna vigezo vyetu, ila tunatumia vigezo vya wagombea watakavyotuletea na hivyo tunaweza kulinganisha baina ya mgombea na mgombea na kuamua kumchagua mmoja wao. Hapa ina maana kama wagombea wote ni wabovu tutamchagua ambaye ni ahueni. Na hapa ni kwa sehemu ndogo, shemu kubwa itatumia kigezo cha umaarufu.

Ni kigezo hiki cha umaarufu ambacho kinawafanya watu sasa hivi kuitisha mikutano ya waandishi kila kukicha kutangaza nia zao za kugombea uongozi. Ni kigezo hiki cha umaarufu ambacho kinawafanya watu kuzunguka huku na kule kutoa misaada ili waonekane wanajali sana.

Sasa watanzania tuache kufanya kosa hili ambalo litaendelea kugharimu maisha yetu.

Katika makala zijazo tutazungumzia ni vigezo gani tunaweza kuvitumia katika kila nafasi ya uongozi ili tuweze kupata viongozi bora.

Tanzania ni nchi yetu sote, unapopata ujumbe huu wajulishe na wenzako wote unaowafahamu ili tuweze kuleta mabadiliko kwenye nchi yetu.

Usisahau kuweka email yako ili upate makala hizi moja kwa moja kwenye email yako.

TUKO PAMOJA.

NENO LA LEO; Kuhusu Yasiyowezekana.

“Most things that we think are impossible in life, is because we have never tried them. So go for every dream and opportunity before making a judgement.”

“Mambo mengi tunayofikiri hayawezekani ni kwa sababu hakuna aliyewahi kujaribu kuyafanya, hivyo fanyia kazi kila ndoto yako kabla ya kujihukumu kwamba haiwezekani”

Nakutakia siku njema.

NENO LA LEO; Kuhusu upatikanaji wa FURSA

"Opportunities are found by those who look for them! The bee has a sting but honey too... so look at every negative and make a positive out of it."
"Fursa zinapatikana kwa wale wanaozitafuta, nyuki anauma ila ana asali pia.... hivyo angalia kwenye kila tatizo kuna njia ya kutokea"
Nakutakia siku njema.

NILICHOJIFUNZA LEO; Viongozi Mashuhuri Walioibadili Dunia.

Karibu kwenye kipengele hiki cha mambo niliyojifunza kwa siku husika. Kwa siku zinazokuja nitakuwa nakushirikisha yale ninayojifunza kuhusu uongozi kupitia kitabu WORLD FAMOUS LEADERS WHO RESHAPED THE WORLD.

Hiki ni kitabu kilichoeleza kwa kifupi baadhi ya viongozi ambao walifanya mambo makubwa duniani. Unaweza kujipatia kitabu hiki na ukaendelea kujifunza zaidi. Kava lake naweka kwenye picha hapo chini;

viongozi

Viongozi hawa kuna waliofanya makubwa kwa wema kama Nelson Mandela na wengineo na kuna waliofanya makubwa kwa ubaya kama Adolf Hitler aliyesababisha vifo vya zaidi ya wayahudi milioni sita.

Kuna mengi ya kujifunza kupitia maisha na uongozi wa watu hawa.

Nakukaribisha katika safari hii ya kujifunza.

TUKO PAMOJA.

NENO LA LEO; Kuhusu Hazina Ya Mwanadamu.

“More gold has been mined from the thoughts of men than has been taken from the earth. So dust off the cobwebs and use all those great ideas you have!”

“Dhahabu nyingi imechimbwa kwenye mawazo ya wanadamu kuliko iliyochimbwa ardhini. Hivyo futa futa utando uliokinga mawazo yako na anza kuyatumia mawazo yako kuleta mabadiliko.”

Nakutakia siku njema.

Je Vijana Wanaoingia Kwenye Siasa Wanaweza Kuwa Wakombozi Wetu?

Kumekuwa na wimbi kubwa la vijana hapa Tanzania ambao wanaingia kwenye siasa. Na kwanzia uchaguzi mkuu wa mwaka 2010 ambapo baadhi ya vijana waliogombea ubunge walipata kuchaguliwa kumekuwa na mwamko mkubwa sana wa vijana kuingia kwenye siasa.

Na hata kwenye uchaguzi mkuu ujao wa mwaka 2015 vijana wengi wameonesha nia ya kugombea nafasi mbalimbali za udiwani na ubunge katika maeneo mbalimbali. Na kwa kuwa mpaka sasa hatuna sheria inayoruhusu mgombea binafsi, vijana hawa wote ambao wana nia ya kugombea inawalazimu kupitia vyama vya siasa. Kwa sasa tuna vijana wengi sana ambao wameingia kwenye vyama mbalimbali vya siasa na wengine wamepata nafasi kubwa kwenye vyama hivi.

siasa

Swali kubwa la kujiuliza ni je vijana wengi kuingia kwenye siasa wanaweza kuwa wakombozi wa nchi yetu Tanzania? Natumia neno ukombozi kwa sababu naamini nchi yetu inahitaji ukombozi ili kutoka hapa ilipo. Inahitaji ukombozi kwa sababu tumefika hapa tulipo kutokana na uongozi mbovu na siasa na sera mbovu zilizowekwa na viongozi hawa wabovu. Na ukiangalia viongozi hao umri wao umekwenda sasa na hivyo vijana ndio watakwenda kuchukua nafasi zao siku za mbeleni.

Najiuliza swali hili kwa sababu tumeona baadhi ya vijana ambao wameingia kwenye siasa hizi wakiishia kutumiwa na baadhi ya watu na hivyo kujikuta wakishindwa kuleta mabadiliko yoyote. Tumeona baadhi ya vijana ambao walikuwa wakilalamikia uongozi mbovu ila wamepewa uongozi kwenye sehemu mbalimbali na kushindwa kuleta mabadiliko yoyote. Na vibaya zaidi wanaishia kuwa sehemu ya kitu walichokuwa wanakipinga.

Sina tatizo na kijana ambaye ameingia kwenye chama chochote cha siasa alichopenda yeye. Iwe ameingia CCM, CHADEMA, CUF au hata CHAUSTA. Kikubwa ambacho wananchi wanataka kuona ni mabadiliko ya kweli katika siasa zetu na hatimaye uongozi wa nchi yetu. Naamini mabadiliko haya yanawezekana kupitia vijana kama watajua ni kitu gani wanakwenda kufanya kwenye siasa hizi na kuepuka kutumika na wale ambao wapo kwenye mifumo hii kwa muda mrefu.

Wewe kama ni kijana ambaye umeingia kwenye siasa jiulize swali hili mara kwa mara na hakikisha unakuwa sehemu ya mabadiliko popote unapokuwepo.

Nakutakia kila la kheri katika harakati za kuleta mabadiliko katika taifa letu Tanzania.

TUKO PAMOJA.

Hakikisha hukosi makala mpya kila inapowekwa kwenye blog hii. Weka email yako hapo juu ili upate makala moja kwa moja kwenye email yako.

NILICHOJIFUNZA LEO; Vita Kubwa Kuwahi Kutokea Afrika Ukiacha Vita Vya Pili Vya Dunia.

Ukiacha vita vya pili vya dunia vita kubwa ambayo imewahi kutokea Afrika ni vita ya pili ya Congo(Second Congo War)
Vita hii ilianza August 1998 na kutangazwa kumalizika July 2003 baada ya serikali ya mpito kushika madaraka.
congo war
Pamoja na kutangazwa kumalizika kwa vita hii bado mapigano na choko choko zinaendelea katika majimbo ya Kivu na Ituri.
Ni katika vita hii ambapo raisi wa Congo Laurent Kabila aliuawa na mtoto wake Joseph Kabila kushika madaraka ya kuongoza nchi.
Vita hii ilihusisha mataifa tisa ya Afrika na vikundi zaidi ya 20 vya wapiganaji.

Sababu ya vita hii.

Sababu kubwa iliyochangia vita hii ni mgogoro wa kimaslahi katika uchimbaji na biashara ya madini.

Madhara ya vita hii.

Vita hii ndio vita kubwa zaidi kutokea barani Afrika ukiacha vita vya pili vya dunia. Mpaka kufika mwaka 2008 zaidi ya watu milioni 5.4 walikuwa wamepoteza maisha kutokana na vita hii. Vifo vingi vilitokana na mauaji ya kuvita, huduma mbovu za afya na ukosefu wa chakula.
Kuna mengi sana ya kujifunza katika vita hii. Kwa kifupi nimeweza kukuandalia haya kwa leo.
Tukutane tena wakati mwingine. Usisahau kuweka email yako ili upate makala hizi moja kwa moja.

Vyanzo;

WIKIPEDIA; Second Congo War.

Nilichojifunza Leo.

Nilichojifunza Leo ni kipengele kipya kitakachokuwa kinakujia mara kwa mara kupitia blog hii Makirita Amani. Ningependa kipengele hiki kiwe kinakujia kila siku ila siwezi kuahidi hilo kwa sasa.
Kupitia kipengele hiki utajifunza mambo mengi kuhusiana na UONGOZI, SIASA, UCHUMI, MAENDELEO na hata HISTORIA za nchi yetu Tanzania, bara letu Afrika na hata Dunia kwa ujumla.
Tutajifunza mambo mengi yatakayotusaidia kuelewa zaidi nchi yetu na dunia kwa ujumla wakati tunajiandaa kuwa viongozi bora wa nchi yetu.
Kupitia kipengele hiki mimi na wewe tutajifunza mambo yatakayotuandaa kuweza kuisaidia nchi yetu, wakati huo mimi naendelea kujiandaa kuwa raisi wa nchi yetu Tanzania.
Karibu sana katika blog hii maalumu kwa maswala ya uongozi na kuhakikisha hukosi machapisho yanayowekwa, weka email yako kwenye box hapo juu na utapokea makala moja kwa moja kwenye email yako kila zinapowekwa.
Naamini tutaendelea kuwa pamoja kwenye safari hii.
Nakutakia kila la kheri.

Sababu Mbili Kwa Nini Tanzania Ni Nchi Masikini.

Kwa nini Tanzania ni nchi masikini? Pamoja na rasilimali nyingi tulizonazo, mlima mrefu, mbuga za wanyama, madini na hata ardhi kubwa kwa nini tunaendelea kuwa masikini?
Hili ni swali gumu sana maana hata raisi wa nchi mheshimiwa Jakaya Kikwete alikiri kwamba hajui kwa nini nchi yetu ni masikini. Sasa leo nataka tujadiliane nini kinatufanya tuendelee kuwa kati ya nchi masikini sana duniani licha ya rasilimali nyingi tulizonazo.
Katika moja ya vitabu vyake Mwalimu Nyerere aliwahi kuandika kwamba ili tuendelee tunahitaji vitu vinne. Vitu hivyo ni WATU, ARDHI, SIASA SAFI na UONGOZI BORA. Katika vitu hivi vinne kuna viwili ambavyo tunavyo vya kutosha na viwili ambavyo tumekosa na ndio maana tunaendelea kuwa masikini.


Vitu viwili tulivyonavyo.

Katika vitu hivi vinne tunavyohitaji ili kuendelea, viwili tayari tunavyo, vitu hivyo ni;
1. Ardhi. Tunayo ardhi kubwa sana ya kutosha. Sehemu kubwa ya ardhi ya tanazania bado haijatumika kabisa. Na sehemu kubwa ya ardhi yetu ina rutuba na hivyo inafaa kwa kilimo cha kila aina. Nenda katika kila mkoa utakuta kuna mazao fulani yanayokubali sana. Hata maeneo ya katikati ya nchi ambayo yana asili ya ukame bado kuna mazai yanakubali vizuri.
Lakini ardhi hii sasa iko hatarini kutoweka kutokana na ukosefu mwingine tutakaouona baadae.
2. Watu. Katika sensa ya mwaka 2012 tanzania ina watu zaidi ya milioni 45. Na wengi katika watu hawa ni vijana. Kwa watu wote hawa tulionao, kama wangeweza kutumiaka vizuri tungeweza kufikia maendeleo makubwa sana.

Vitu viwili ambavyo tumekosa.

1. Siasa safi. Kila nchi duniani inaendeshwa kwa siasa. Tanzania tuliwahi kuwa na siasa ya UJAMAA NA KUJITEGEMEA, ambayo ilikwenda vizuri sana mpaka pale ilipouliwa, tumewahi pia kuwa na SIASA NI KILIMO ambapo kilimo kilipewa kipaumbele kwa sababu ndio sehemu kubwa ya wananchi wanategemea kilimo. Lakini nayo haikudumu muda mrefu. Tuliwahi pia kuwa na SIASA YA UWEKEZAJI NA UBINAFSISHAJI ambapo tulishuhudia mashirika ya umma yakipewa watu binafsi na wengi wao kutoka nje ya nchi. Sasa hivi sina hakika tunaendeshwa na siasa gani.
Tumekosa siasa safi na ndio maana tumeshindwa kutumia rasilimali zetu na hata watu wengi tulionao kuweza kufikia maendeleo kama taifa.
2. Uongozi bora. Hili ndio tatizo kubwa sana na ndio linazaa matatizo mengine yote. Tumekosa uongozi bora ambao unaweza kuwatengeneza na kuwatumia watu tulionao kuweza kufikia mafanikio. Tumekosa uongozi bora ambao utatengeneza siasa safi ambayo itatuwezesha kutumia watu wetu na rasilimali zetu vizuri.
Tunao watu wengi ambao wanashikilia nafasi za uongozi ila wamekosa sifa za uongozi. Watu hawa ndio wanafanya maamuzi mabovu na hivyo kutufanya tuendelee kuwa masikini.
Hii ndio sababu kubwa iliyonifanya niwe naandika kuhusu uongozi kwenye blog hii kila siku ya jumapili. Kama umekosa kusoma makala za uongozi zilizopita, bonyeza maandishi haya ili uweze kuzisoma.

Tufanye nini ili kuondoka kwenye umasikini huu?

Kwa kuwa tumeshajua mambo mawili muhimu tunayokosa ili kufikia maendeleo na kwa kuwa tumeshajua ukosefu wa uongozi bora ndio tatizo kubwa zaidi nashauri sisi wananchi tuchukue hatua ya kujua na kuchagua viongozi bora. Na nashauri hasa vijana tujifunze sana kuhusu uongozi na kisha tugombee nafasi mbalimbali za uongozi ili tuweze kuleta mabadiliko kwenye nchi yetu.
Kukaa tu na kulalamika kila siku hakutakuwa na msaada kwetu binafsi na hata kwa vizazi vijavyo. Kuna chaguzi zinakuja mwaka huu na mwaka ujao, tutumie nafasi hii kujua ni viongozi wapi wanaotufaa na wapi wasiotufaa. Tukiendelea kufanya makosa haya katika uchaguzi wa viongozi tutaendelea kuwa masikini siku zote.
TANZANIA NI NCHI YETU SOTE, TUSHIRIKIANE KUIJENGA.

Mambo Matano Ambayo Viongozi Bora Hufanya Kila Siku.

Karibu tena ndugu msomaji kwenye mtandao huu ambao umejikita kwenye kukujenga wewe kuwa kiongozi bora. Kwa siku za hivi karibuni hakujakuwa na makala mpya hapa kutokana na mambo yaliyoingiliana kidogo. Hata hivyo napenda nikukaribishe tena katika shule hii ya uongozi na kila jumapili utaendelea kupata makala za mambo ya uongozi.
Kama tulivyoona kwenye moja ya makala zilizopita kiongozi anatengenezwa na sio kuzaliwa. Ile dhana kwamba viongozi bora wanazaliwa sio kweli, bali viongozi bora hutengenezwa na mazingira waliyozaliwa na hata kukulia na pia elimu wanayoipata. Hivyo kama kuna mtu alikwambia wewe huwezi kuwa kiongozi kuanzia leo usikubali tena kauli hiyo.
Pia tuliona ni muhimu sana kila mtu kuwa kiongozi kwa sababu viongozi ndio wanaopata mafanikio makubwa kwenye jambo lolote linalofanyika na binadamu. Iwe kazi, biashara na hata familia, unapokuwa na tabia za uongozi bora unapata mafanikio makubwa zaidi.
Leo tutaona mambo matano ambayo viongozi bora hufanya kila siku, anza kufanya mambo haya ili uweze kuwa na uongozi bora kwenye jambo lolote unalofanya.
1.  Kujifunza.
Viongozi bora hujifunza kila siku na hii huwasaidia kujua mambo mengi na hivyo kuwasaidia katika kufanya maamuzi. Kama hujifunzi kila siku ni vigumu sana kuwa kiongozi bora. Viongozi bora hujifunza kwa kujisomea na pia hujifunza kutokana na uzoefu wao na uzoefu wa watu wengine.


2. Kupangilia siku yao.
Viongozi bora hupangilia siku yao kabla hawajaianza. Hujua watafanya kitu gani na katika muda gani. Kupangilia siku humwezesha kiongozi bora kukamilisha majukumu yake muhimu na kuweza kuwa na matumizi mazuri ya muda.
3. Kugawa majukumu kwa wengine.
Viongozi bora wanajua hawawezi kufanya kila kitu wao wenyewe, hivyo kila siku hutafuta njia za kugawa majukumu kwa watu wengine. Hii huwawezesha viongozi kubaki na majukumu machache ya msingi ambayo huyatekeleza kwa ufanisi mkubwa. Ili kuwa kiongozi bora acha kung'ang'ania kufanya kila kitu mwenyewe.
4. Kutengeneza viongozi wengine.
Viongozi bora hutambua kwamba kutengeneza viongozi wengine ni jukumu lao. Hivyo kila siku wanatengeneza viongozi wengine kwa kuwa washauri wazuri wa watu waliochini yao ili waweze kujiongoza na kuongoza wengine.
5. Huwasiliana vyema.
Viongozi bora hufanya mawasiliano mazuri kila siku kwa sababu wanajua mawasiliano yanaweza kuwajenga au kuwabomoa kama viongozi. Mawasiliano haya bora huyafanya wakati wanakutana na wengine, wakati wanaendesha vikao au mikutano na hata wakati wanafanya mawasiliano kwa simu. Viongozi bora hujua ni lugha ipi ya kutumia ili kuweza kufikisha ujumbe na ujumbe huo uwe na ushawishi mkubwa.
Mpaka sasa wewe ni kiongozi kwa sababu umeonesha nia ya kujifunza zaidi sasa unaelekea kwenye uongozi bora. Ongeza mambo hayo matano kwenye maisha yako ya kila siku na utaona mafanikio makubwa ya uongozi.
Kama una maoni yoyote tafadhali tushirikishe kwenye sanduku la maoni hapo chini.
Usisahau kuweka email yako kwenye box hapo juu ili kupata makala mpya kwenye email yako kila zinapochapishwa.
Nakutakia kila la kheri katika uongozi wako.
TUKO PAMOJA.

Uongozi Ni Watu, Na Sio Vinginevyo.

Kama nikikuuliza swali ni nani muhimu kati ya kiongozi na mwananchi anayeongozwa?

Kwa hali ya kawaida na mazoea tuliyonayo sisi, unaweza kufikiri kiongozi ni bora zaidi ya mwananchi. Lakini huu sio ukweli hata kidogo.

Sio ukweli kwa sababu bila ya mwananchi anayeongozwa hakuna kiongozi, kiongozi ni mwakilishi wa wale waliompa nafasi ya kuwawakilisha. Sasa inakuwaje mtu huyu aliyepewa nafasi awe bora zaidi ya wale waliompa nafasi hiyo?

Kuna utamaduni ama mazoea mabaya ambayo yamejengeka kwenye jamii yetu yanayowafanya viongozi kujiona ni bora kuliko wale wanaowaongoza. Au kujiona ni muhimu zaidi ya wale ambao wamewapa nafasi ya kuwawakilisha.

Haya ni mazoea mabaya sana ambayo yalipata nafasi kutokana na watu wengi kutokuwa na uelewa mzuri kwenye mambo ya uongozi. Ila kwa sasa asilimia kubwa ya watu wana uelewa mzuri sana juu ya wajibu wao na wajibu wa viongozi wao.

Hivyo kwa kizazi kipya cha viongozi ni vyema tukafahamu huu mtazamo wa zamani wa uongozi umekufa na hautoweza kukusaidia. Wewe kama kiongozi unayejitengeneza jua watu ni muhimu kama ulivyo wewe kiongozi. Watu wana nafasi kubwa sana kwenye mafanikio ya uongozi wako.

Ule utamaduni wa viongozi kutaka kupata huduma bora kwa sababu wao ni viongozi hauwezi kukujenga na kukupa mafanikio. Kwa kusema hivi pia sisemi kiongozi apate huduma mbovu ili aonekane yuko na wananchi. Bali kiongozi ahakikishe wananchi wanapata huduma bora kama anazopata yeye.

Lakini hili halitokei kwa sababu baada ya kiongozi kupata huduma bora anasahau kwamba wananchi wanapata huduma mbovu. Na hata akiambiwa haoni uzito sana kwa sababu huduma hizo mbovu hazimuumizi moja kwa moja.

Ni mara ngapi tumeona mtu akiwa na uchungu sana kabla ya kuwa kiongozi ila anapokuwa kiongozi anasahau yale aliyokuwa anayalalamikia? Wanasema madaraka matamu, ila usianguke kwenye shimo hili. Jua watu unaowaongoza ni muhimu sana kama ulivyo wewe na baada ya kujua hili hakikisha unafanya kila juhudi kulinda umuhimu wao.

Karibu katika darasa letu la uongozi ambapo kila jumapili unapata makala nzuri inayohusu uongozi. Tembelea mtandao huu kila mara ili kujifunza mengi zaidi. Karibu tujenge kizazi kipya cha uongozi ambao utaleta tija kwenye nchi yetu Tanzania.

Dalili Kumi Kwamba Tayari Wewe Ni Kiongozi.

Kwenye makala zilizopita tumeona ni muhimu sana kwa kila mmoja wetu kuwa kiongozi. Pamoja na umuhimu huo sio watu wote ni viongozi na sio watu wote wataweza kuwa viongozi. Na hata ambao ni viongozi sio wote ni viongozi bora wanaotoa matokeo mazuri.

Pia tumejifunza kwamba kiongozi anaweza kuzaliwa au kutengenezwa. Kutegemea na mazingira na uhitaji wa mtu, mtu yeyote anaweza kuendeleza tabia za uongozi ndani yake.

Leo tutaona dalili kumi za sifa ya uongozi. Kama wewe una sifa hizi tayari wewe ni kiongozi na unahitaji kujiendeleza zaidi ili kuweza kufanya makubwa zaidi kwenye uongozi wako. Kama huna dalili hizi kuna habari nzuri na mbaya kwako.

Habari mbaya kwako ni kwamba utaendelea kuwa mfuasi maisha yako yote na kwa nafasi kubwa utashindwa kuonesha uwezo wako wa kweli na kuleta tofauti kubwa kwenye jamii yako na dunia kwa ujumla.

Habari nzuri ni kwamba unaweza kujifunza tabia hizi na ukawa kiongozi bora sana. Uzuri ni kwamba kila kitu unaweza kujifunza, ni utayari wako na juhudi zako ndivyo vitakufanya uweze kujua kile unachotaka kujua. Njia bora ya kujifunza uongozi ni kujua vitu na kuvifanyia kazi. Hutakuwa kiongozi kwa kusoma tu hapa, bali soma na utumie yale unayojifunza kwenye maisha yako ya kila siku.

Kwa kifupi sana naomba nitaje dalili kumi zinazoonesha kwamba wewe ni kiongozi. Kwa maelezo zaidi tunaweza kujadiliana kwenye maoni hapo chini.

1. Unapenda kuleta mabadiliko.

2. Una ndoto kubwa sana mpaka wengine wanaona haziwezekani.

3. Husubiri kuambiwa nini cha kufanya,

4. Unapenda kutatua matatizo yanayowasumbua wengine.

5. Hupendi kulalamika au kulaumu wengine.

6. Unajali sana na kukuza mahusiano.

7. Matendo yako na maneno yako vinaendana.

8. Hukubaliani na mifumo isiyo na tija.

9. Uko tayari kukiri makosa na kuomba radhi.

10. Unapenda kujifunza mambo mapya na kuhusu uongozi.

Kama una dalili hizo kumi hongera wewe ni kiongozi. Kama huna usikate tamaa bado una nafasi kubwa ya kujijengea uongozi.

Uongozi unaanza na kuchagua kuwa kiongozi, baada ya hapo unaendelea kujifunza na kupata uzoefu. Karibu kwenye mafunzo ya kuongozi kupitia blog hii. Ili kuhakikisha hukosi mafunzo haya weka email yako hapo juu kwenye blog ili upate makala hizi moja kwa moja kwenye email yako.

TUKO PAMOJA.

Makosa Makubwa Matano Yanayoweza Kukuharibu Wewe Kama Kiongozi.

Ili uweze kufanikiwa kwenye uongozi kuna mambo muhimu unatakiwa kuwa unafanya na pia kuna mambo mengine unatakiwa kuepuka kufanya.

Katika makala zilizopita tumekuwa tukiangalia mambo muhimu ya kufanya ili kuweza kufanikiwa kwenye uongozi. Ili kuwa kiongozi mzuri ni muhimu kuwa na maono, ushawishi, ushirikiano na uadilifu. Kuwa na mpango mikubwa na kuweza kuwashawishi wengine kuifikia ili kuboresha maisha yako ni tabia moja inayoweza kukutengeneza kuwa kiongozi bora.

Pamoja na hayo kuna mambo ukiyafanya unaweza kuharibu sana uongozi wako bila ya kujali umeutengeneza kwa muda gani. Mambo haya yamekuwa yakifanywa na watu wengi na ndio sababu kubwa ya wao kushindwa kuwa viongozi wazuri. Kwa kuwa wewe unajifunza kuwa kiongozi bora, ni muhimu sana ukayajua mambo haya ili usije kuyafanya na ikakugharimu kwenye maisha yako na uongozi wako.

Hapa nitaongelea makosa kubwa matano unayoweza kufanya yakaharibu kabisa uongozi wako. Makosa hayo ni kama ifuatavyo.

1. Kutaka kupendwa badala ya kuheshimika.

Ni rahisi sana kwa kiongozi kutaka watu wampende yeye kutokana na uongozi wake. Ili kutimiza hilo anajikuta anafanya mambo ya kuwafurahisha watu badala ya kufanya mambo yatakayowasaidia watu. Katika uongozi kuna maamuzi unaweza kufanya watu wasikuelewe kwa sababu wewe una maono, baadae mafanikio yanapoonekana watu hukuheshimu sana kama kiongozi. Ila ukitaka kuwafurahisha watu hutoweza kufanya mambo ya kuwasaidia. Usitake kupendwa na watu bali jenga kuheshimiwa na watu kutokana na maamuzi unayofanya yenye manufaa kwenye maisha yao.

2. Kutochukua ushauri na msaada wa wengine.

Kuna wakati kiongozi anaweza kuona yeye yupo juu ya wengine hivyo ushauri wake ndio sahihi. Pia anafikiri hahitaji msaada wowote kutoka kwa anaowaongoza. Hili ni kosa kubwa sana unaloweza kufanya wewe kama kiongozi. Bila ya kujali ngazi yako ya uongozi ni muhimu sana kuchukua ushauri kwa unaowaongoza. Wakati mwingine kuna mawazo mazuri sana kutoka kwa unaowaongoza, pia unaweza kupata msaada mkubwa kutoka kwa unaowaongoza.

3. Kutokujali na kuendeleza vipaji vya wengine.

Watu unaowaongoza wana vipaji na uwezo mkubwa sana. Kazi yako kama kiongozi ni kuendeleza vipaji hivi ili kuwawezesha kufikia malengo makubwa kwenye maisha yao. Kama kiongozi hutothamini vipaji na uwezo wa watu wako itakuwa vigumu sana kwao kukufuata na hii itaathiri uongozi wako.

4. Kushindwa kupanga majukumu vizuri kwa unaowaongoza.

Kama wewe ni kiongozi wa timu au kikundi ambacho kinatakiwa kukamilisha jukumu fulani ni muhimu sana kila mtu kujua jukumu lake ni nini na anawezaje kulitimiza. Kushindwa kupanga na kueleza vizuri majukumu ya kila mtu ni chanzo kikubwa cha kupungua kwa uzalishaji kwenye maeneo mengi ya kazi. Wewe kama kiongozi hakikisha wafuasi wako wanajua majukumu yao na njia za kuyatimiza.

5. Kushindwa kutoa taarifa kwa watu.

Ni muhimu sana kutoa taarifa kwa wale unaowaongoza. Watu wanataka kujua ni mafanikio kiasi gani yamefikiwa na ni changamoto gani zinawarudisha nyuma. Wewe kama kiongozi unajukumu la kutoa taarifa sahihi na kwa muda sahihi kwa watu unaowaongoza. Hii itawafanya kuwa sehemu ya uongozi wako na kuufurahia.

Kama ukiweza kuepuka mambo haya matano, utafanikiwa sana kwenye uongozi wako. Kumbuka ni muhimu sana kwako kuwa kiongozi kwenye maisha yako. Na unaweza kujifunza kuwa kiongozi bora. Weka email yako hapo juu(kwenye blog) ili kupata makala hizi za mafunzo ya uongozi moja kwa moja kwenye email yako.

Karibu sana.

Siri Kumi za Mafanikio Kwenye Uongozi.

Katika watu wengi wanaopewa nafasi za kuongoza kuna wachache sana ambao wanakuwa ni viongozi bora. Wengine wanaishia kuwa tu na majina ya uongozi ila wanashindwa kufanya mambo makubwa kupitia nafasi zao za uongozi.

Mpaka unasoma hapa naamini unataka kuwa kiongozi bora. Ili uweze kupata mafanikio kwenye uongozi, kuna tabia kumi muhimu unatakiwa kuwa nazo na kuziendeleza. Tabia hizo ziko wazi kabisa ila kutokana na watu wengi kutozipa mkazo zimegeuka na kuwa siri kubwa.

Leo tutazungumzia tabia kumi muhimu za kufanikiwa kwenye uongozi. Tabia hizi zinafanya kazi bila ya kujali wewe ni kiongozi wa aina gani. Uwe ni kiongozi usiyekuwa na cheo, kiongozi wa wananchi, kiongozi wa shughuli zako au hata kiongozi wa maisha yako ni vyema ukaanza kutengeneza na kuendeleza tabia hizi.

1. Mfano.

Ili uweze kufanikiwa kama kiongozi ni lazima uwe mfano bora kwa wale unaowaongoza. Utatengeneza mfano mzuri pale ambapo utakuwa unatenda yale unayohubiri. Lazima wewe uwe wa kwanza kuonesha mwendo ili wafuasi wako nao wafuate. Ile kauli kwamba “fuata maneno yangu, usifuate matendo yangu” imesababisha watu wengi sana kushindwa kwenye uongozi. Watu wanapenda kumfuata na kumheshimu mtu ambae anaonesha mfano wa vitendo kwao.

2. Nguvu,

Mafanikio katika uongozi yanategemea sana nguvu ya kiongozi. Naposema nguvu simaanishi nguvu za kimwili pekee bali hata nguvu za kihisia, nguvu za kiakili na nguvu za kiimani. Kiongozi unapokuwa na nguvu hizi inakuwa rahisi kuzitoa kwa wale unaowaongoza.

3. Shauku.

Viongozi wanaofanikiwa sana ni wale wenye shauku kubwa kwenye kazi zao na kwenye maendeleo ya watu wanaowaongoza. Kwa kuwa na shauku kunawafanya wafanye mambo bora zaidi. Pia shauku inaambukizwa mpaka kwa wafuasi.

4. Uvumilivu.

Bila ya uvumilivu huwezi kuwa kiongozi bora, hakuna zaidi ya hapo. Viongozi wengi waliofanikiwa sana walipitia mambo magumu sana kwenye maisha yao. Hata wewe utapitia mambo magumu sana kwenye uongozi wako na maisha yako kwa ujumla. Kuna wakati utashindwa, kuna wakati utakosea sana, tumia nyakati hizi ngumu kujijenga na kuwa imara. Unapovumilia na kuvuka nyakati hizi ngumu unatoa imani kubwa kwa wafuasi wako.

5. Uelewa wa kihisia.

Hisia ni moja ya vitu vinavyoweza kumjenga kiongozi au kumbomoa ndani ya muda mfupi sana. Ili kuwa kiongozi bora ni lazima uzijue hisia zako na ujue ni jinsi gani ya kuzimiliki. Usikubali hisia zako zikutawale mwishowe uanze kufanya mambo yatakayoharibu sifa zako. Pia ni muhimu kuweza kusikiliza na kuelewa hisia za wafuasi wako na kuweza kuwasaidia kupata mtazamo sahihi.

6. Uwezeshaji.

Kiongozi bora ni yule anayewawezesha wafuasi wake kuchukua hatua na kufanya mabadiliko kwenye kazi zao na maisha yao. Katika uwezeshaji kiongozi anawapa watu nguvu na mamlaka ya kufanya mambo ambayo yatakuwa na manufaa kwenye maisha yao. Unapowawezesha watu kuchukua hatua, unawajengea ujasiri ambao baadae utawapelekea kuwa viongozi bora.

7. Ufanisi.

Viongozi bora huwa na ufanisi kwenye utekelezaji wa majukumu yao. Katika ufanisi viongozi huwa na mipango mizuri ambayo itawasaidia kufikia malengo waliyojiwekea. Viongozi bora hufanya jambo sahihi na sio kufanya jambo kwa usahihi. Uongozi bora unapimwa kutokana na majibu anayozalisha kiongozi na sio kwa hotuba nzuri.

8. Kuchukua hatua.

Viongozi bora wanajua ni wapi walipo na pia wanajua ni wapi wanataka kwenda na huchukua hatua mara moja ili kufika wanakotaka kwenda. Hapa ndipo viongozi wanapobadili maono kuwa uhalisia. Kama kiongozi una ahadi na maneno mengi mazuri ila huwezi kuchukua hatua ya kuyatekeleza hufai kuwa kiongozi bali muigizaji.

9. Mafanikio.

Mafanikio ni nguzo muhimu sana kwa viongozi waliofanikiwa. Kiongozi lazima awe amefanikiwa kwenye shughuli zake ili aweze kupata wafuasi wanaotaka kufanikiwa kama yeye. Viongozi bora hupanga kuwa bora kwenye shughuli zao na hivyo kukazana kila siku kutoa majibu yenye ubora.

10. Maadili.

Tabia hii imekuja mwisho ila ilipaswa kuwa ya kwanza kabisa. Huwezi kufanikiwa kwenye uongozi wa aina yeyote ile kama huna maadili. Watu wanapenda kumfuata mtu ambaye anajiheshimu na hivyo kuamini atawaheshimu. Kama kiongozi una skendo chafu ni vigumu sana watu kukupa imani ya kweli kutoka ndani ya mioyo yao. Tatizo kubwa tunalolipata kwenye uongozi hapa Tanzania ni maadili mabovu ya viongozi. Kuwa kiongozi wa mfano kwa kuwa na maadili mazuri kwenye maisha yako.

Kwa kujijengea na kuendeleza sifa hizo kumi utajijenga kama kiongozi wa mfano na mwenye mafanikio makubwa sana. Kumbuka wewe ni kiongozi, hivyo endeleza uongozi wako ili uweze kuwasaidia watu wengi zaidi.

Kama una jambo lolote unaona ni zuri kutushirikisha tafadhali weka maoni yako hapo chini. Kwa kuweka maoni yako hapo chini ni dalili nzuri kwamba unaelekea kuwa kiongozi bora na wa mfano.

Karibu kiongozi tujadiliane yaliyo mema kwenye uongozi.